CAF yatangaza tarehe ya Super Cup, Mamelodi kuivaa USM Alger
Muktasari:
- Katika pambano hilo, mabingwa wa Ligi ya Mabingwa Afrika, Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini, watachuana na mabingwa wa Kombe la Shirikisho Afrika, USM Alger ya Algeria, kuwania taji la Super Cup.
Shirikisho la Soka Afrika (CAF) limetangaza rasmi kuwa Novemba 8, 2026 ndiyo tarehe ya mchezo wa CAF Super Cup, utakaowakutanisha mabingwa wa mashindano makubwa mawili ya ngazi ya klabu barani Afrika.
Katika pambano hilo, mabingwa wa Ligi ya Mabingwa Afrika, Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini, watachuana na mabingwa wa Kombe la Shirikisho Afrika, USM Alger ya Algeria, kuwania taji la Super Cup.
Hata hivyo, CAF bado haijaweka wazi uwanja utakaotumika pamoja na muda rasmi wa kuanza kwa mchezo huo.
Licha ya ukimya huo, taarifa mbalimbali zinaeleza kuwa mechi hiyo huenda ikafanyika jijini Pretoria, Afrika Kusini, katika Uwanja wa Loftus Versfeld, ambao ni uwanja wa nyumbani wa Mamelodi Sundowns.
Iwapo taarifa hizo zitathibitishwa, Sundowns itakuwa na faida ya kucheza mbele ya mashabiki wake katika pambano linalotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kati ya mabingwa hao wa Afrika Kusini na Algeria.