Bruno afikiria kuchapa lapa Manchester Utd
Muktasari:
- Staa huyo wa Ureno alihusishwa na mpango wa kuondoka dirisha lililopita baada ya klabu za Saudi Arabia kudaiwa kupeleka ofa nono ya kumsajili, lakini aliamua kubaki Man United kwa msimu mwingine zaidi kupambana kuirudisha kwenye makali yake.
NAHODHA wa Manchester United, Bruno Fernandes ameripotiwa kufikiria mpango wa kuachana na miamba ya Old Trafford kwenye dirisha lijalo la majira ya kiangazi.
Staa huyo wa Ureno alihusishwa na mpango wa kuondoka dirisha lililopita baada ya klabu za Saudi Arabia kudaiwa kupeleka ofa nono ya kumsajili, lakini aliamua kubaki Man United kwa msimu mwingine zaidi kupambana kuirudisha kwenye makali yake.
Fernandes ameendelea kuwa mchezaji muhimu kwenye kikosi cha Man United msimu huu, akicheza mechi tisa, amefunga mara mbili na asisti moja, ikiwamo ile ya kibabe dhidi ya Liverpool alipopiga pasi matata kwa Harry Maguire katika ushindi wa 2-1 uwanjani Anfield. Mkataba wa Fernandes, 31, utafika tamati Juni 2027, licha ya kuwapo na kipengele cha kuongeza miezi 12 zaidi.
Marcus Rashford
MSHAMBULIAJI wa Manchester United, Marcus Rashford, 27, ambaye anacheza kwa mkopo Barcelona ameripotiwa kuwaambia wawakilishi wake kwamba anataka kusaini mkataba wa kudumu wa kuitumikia kwa muda mrefu zaidi. Katika makubaliano kati ya Barca na Man United kuna kipengele kinaeleza anaweza kusaini mkataba wa moja kwa moja mwisho wa msimu kwa kiasi kinachotajwa kufikia Pauni 30 milioni.
Nick Woltemade
MSHAMBULIAJI wa Newcastle United, Nick Woltemade ambaye ni raia wa Ujerumani anadaiwa kuwa na ndoto ya siku moja kuvaa jezi ya Bayern Munich. Woltemade, ambaye alijiunga na Newcastle United akitokea Werder Bremen katika dirisha lililopita la majira ya kiangazi, amekuwa na kiwango bora tangu ajiunge na timu hiyo jambo ambalo lililosababisha vigogo wengi Ulaya waanze kumtazama kwa jicho la tatu.
Richarlison
EVERTON iko tayari kufanya mazungumzo kumsajili mshambuliaji wa Tottenham Hotspur, Mbrazili Richarlison ambaye amekuwa hapati nafasi ya kutosha tangu kuanza kwa msimu huu na kumekuwa na taarifa kwamba Spurs itakuwa tayari kumuuza Januari, mwakani. Richarlison, 28, aliwahi kucheza Everton kati ya 2018 hadi 2022, kabla ya kujiunga na Spurs.
Marc Guehi
BEKI wa kati wa Crystal Palace na timu ya taifa ya England, Marc Guehi, 25, anatajwa kuwa miongoni mwa wachezaji wanaowindwa na Bayern Munich. Mbali ya Guehi Bayern pia inamfuatilia kwa karibu Nico Schlotterbeck, 25, wa Borussia Dortmund. Mabeki hao wanaweza kusajiliwa ili kuchukua nafasi ya Dayot Upamecano 26 na Kim Min-jae, 28, ambao wanaweza kuondoka mwisho wa msimu.
Ter Stegen
KIPA wa kimataifa wa Ujerumani, Marc Andre Ter Stegen huenda akaondoka Barcelona dirisha lijalo la majira ya baridi. Staa huyo, 33, amekuwa na panda shuka nyingi kwa miaka ya hivi karibuni kutokana na majeraha ya mara kwa mara. Kwa sasa haonekani kuwa na nafasi ya kwanza katika kikosi cha wababe hao wa Nou Camp. Timu mbalimbali za Saudi Arabia na England zinadaiwa kutaka kumsajili.
Mateo Kovacic
AC Milan, Aston Villa na West Ham United zimeonyesha nia ya kumsajili kiungo wa Manchester City na timu ya taifa ya Croatia, Mateo Kovacic, mwenye umri wa miaka 31. Kovacic, aliyesajiliwa na Man City kutoka Chelsea 2023, amekuwa na wakati mgumu tangu wasajiliwe Matheus Nunes na Marco Lewis ambao ndio wanaonekana kupewa nafasi kubwa zaidi ya kucheza.
Joshua Zirkzee
MSHAMBULIAJI wa Manchester United na timu ya taifa ya Uholanzi, Joshua Zirkzee anadaiwa kuomba kuondoka katika dirisha la usajili la Januari na West Ham United inaonekana kuwa mbele katika mbio za kumsajili mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 24. Zirkzee, aliyesajiliwa kutoka Bologna inaelezwa staa huyo anahofia kussalia Man United kwani anataka kucheza Kombe la Dunia 2026.