Bellingham aweka rekodi mpya England
Muktasari:
- Kiungo huyo wa Real Madrid alikuwa akilingana na rekodi ya mabao sita iliyowekwa na Gary Lineker katika Kombe la Dunia la Mexico 1986, pamoja na nahodha Harry Kane aliyefunga mabao sita katika Kombe la Dunia la 2018 nchini Russia na mashindano ya mwaka huu.
ATLANTA, MAREKANI: KIUNGO Jude Bellingham ameandika historia kwa kuwa Mwingereza wa kwanza kufunga mabao saba katika Kombe la Dunia moja, baada ya kufunga bao la mwisho katika ushindi wa mabao 6-4 dhidi ya Ufaransa kwenye mechi ya kusaka nafasi ya tatu.
Kiungo huyo wa Real Madrid alikuwa akilingana na rekodi ya mabao sita iliyowekwa na Gary Lineker katika Kombe la Dunia la Mexico 1986, pamoja na nahodha Harry Kane aliyefunga mabao sita katika Kombe la Dunia la 2018 nchini Russia na mashindano ya mwaka huu.
Bellingham mwenye umri wa miaka 23 aliingia uwanjani dakika ya 79 akitokea benchi, kabla ya kufunga bao la mwisho la mchezo katika sekunde za mwisho. Alianza shambulizi la kushtukiza kutoka katikati ya uwanja, akapenya hadi ndani ya eneo la Ufaransa, akampita beki mmoja na kuupachika mpira kona ya chini ya lango.
Akizungumza kupitia BBC One, kiungo wa zamani wa England, Danny Murphy, alimpongeza Bellingham kwa kiwango chake. “Ana imani kubwa na uwezo wake. Uvumilivu, ufundi na umaliziaji wake vilikuwa vya kiwango cha juu. Hilo ni bao la mchezaji bora wa England kwa sasa,” amesema Murphy.
Dakika 12 kabla ya kufunga bao hilo, Bellingham alionekana kuwa tayari kupiga penalti ambayo England ilipata, lakini alimkabidhi mpira Bukayo Saka ili akamilishe hat-trick yake.
Baada ya mchezo, Saka alifafanua kilichotokea akisema:”Hapana, Jude hakuwa anataka kupiga penalti. Yeye ndiye alikuwa wa kwanza kuniambia niende nikakamilishe hat-trick yangu. Hakuna aliyekuja kunivuruga, tangu mwanzo nilikuwa nitaipiga mimi.”