Ballon d'Or: Messi, Lamine, Rodri, Kane au Mbappe?
Muktasari:
- Tuzo hiyo ya mchezaji bora duniani inayotolewa na jarida la France Football itakabidhiwa Oktoba 26 jijini London, huku ushindani ukiwa mkali zaidi kutokana na athari kubwa ya Kombe la Dunia katika maamuzi ya washindi wa miaka yenye fainali za dunia.
MADRID, HISPANIA: KOMBE la Dunia la 2026 limefikia tamati na sasa macho ya mashabiki yanaelekezwa kwenye msimu mpya wa klabu wa 2026-27.
Hata hivyo, kabla ya msimu huo kushika kasi, kuna tukio moja ambalo tayari limeanza kutawala mijadala duniani ni suala la kumpata mshindi wa tuzo ya Ballon d'Or 2026.
Tuzo hiyo ya mchezaji bora duniani inayotolewa na jarida la France Football itakabidhiwa Oktoba 26 jijini London, huku ushindani ukiwa mkali zaidi kutokana na athari kubwa ya Kombe la Dunia katika maamuzi ya washindi wa miaka yenye fainali za dunia.
Gazeti la Marca limewachambua nyota watano wanaopewa nafasi kubwa zaidi ya kutwaa tuzo hiyo.
Messi bado ana hoja nzito
Lionel Messi anaendelea kuwa mmoja wa wagombea wakuu baada ya kuiongoza Argentina hadi fainali ya Kombe la Dunia.
Nahodha huyo mwenye miaka 39 alifunga mabao nane na kutoa pasi nne za mabao, akimaliza kama mfungaji wa pili bora wa mashindano hayo.
Licha ya Argentina kupoteza taji kwa Hispania, kiwango chake kilithibitisha kuwa bado ni mmoja wa wachezaji bora duniani.
Iwapo atashinda, itakuwa Ballon d'Or yake ya tisa na atakuwa mchezaji mwenye umri mkubwa zaidi kuwahi kutwaa tuzo hiyo.
Lamine Yamal, nyota wa sasa
Kwa wengi, hasa baada ya Hispania kutwaa Kombe la Dunia, Lamine Yamal ndiye anayestahili zaidi kushinda.
Ingawa hakung'ara sana binafsi kwenye fainali hizo, mchango wake katika mafanikio ya Hispania ulikuwa mkubwa.
Katika ngazi ya klabu, kijana huyo aliiongoza Barcelona kutwaa LaLiga na Spanish Super Cup, akifunga mabao 24 na kutoa pasi 17 za mabao.
Akiwa na umri wa miaka 19 pekee, tayari ameonyesha uwezo wa kuwa mmoja wa mastaa wakubwa wa soka duniani.
Kane amefanya kila kitu
Mshambuliaji Harry Kane pia ameingia kwenye mjadala baada ya msimu mwingine bora akiwa Bayern Munich.
Nahodha huyo wa England alifunga mabao 36 akiwa na Bayern na kuisaidia klabu hiyo kutwaa mataji ya Bundesliga na Kombe la Ujerumani.
Katika Kombe la Dunia alifunga mabao sita na kuvunja rekodi ya Gary Lineker katika michuano hiyo.
Kane mwenyewe amesema huu ndio ulikuwa msimu bora zaidi katika maisha yake ya soka.
Rodri moyo wa Hispania
Kiungo wa Manchester City, Rodri Hernandez, naye anaungwa mkono kwa nguvu.
Alikuwa mmoja wa wachezaji bora wa Hispania katika safari ya kutwaa Kombe la Dunia, akitoa kiwango cha hali ya juu kuanzia hatua ya makundi hadi fainali.
Mbali na mafanikio hayo, Rodri aliisaidia Manchester City kurejea kwenye mbio za ubingwa wa Ligi Kuu baada ya kupona jeraha ya goti lililomsumbua mwishoni mwa mwaka 2024.
Wapo wanaoamini ushindi wake ungekuwa heshima pia kwa Hispania, ambayo kwa sasa inaonekana kuwa timu bora zaidi duniani.
Mbappe ana takwimu zinazotikisa
Mshambuliaji Kylian Mbappe anabaki kuwa mgombea mwenye takwimu bora zaidi za kibinafsi.
Alimaliza akiwa mfungaji bora wa Ligi ya Mabingwa Ulaya, LaLiga na pia Kombe la Dunia.
Zaidi ya hayo, alivunja rekodi ya Lionel Messi na kuwa mfungaji bora wa muda wote katika historia ya Kombe la Dunia.
Ingawa hakufanikiwa kutwaa mataji makubwa akiwa na klabu yake wala Ufaransa, kiwango chake binafsi kimeendelea kuwa cha kipekee.
Nani ataibeba Ballon d'Or?
Ushindani wa mwaka huu unaonekana kuwa mkali kuliko miaka ya karibuni.
Messi ana hoja ya Kombe la Dunia na rekodi zake, Lamine ana mafanikio ya klabu na timu ya taifa, Rodri ameiongoza Hispania kutwaa ubingwa wa dunia, Kane amekuwa mashine ya mabao na kutwaa mataji, huku Mbappe akiwa na takwimu bora zaidi za kibinafsi.
Mpaka sasa hakuna mgombea anayejitenga waziwazi, jambo linaloashiria kuwa Ballon d'Or ya 2026 inaweza kuwa moja ya tuzo zenye ushindani mkubwa zaidi kuwahi kushuhudiwa.