Neuer atajwa kikosi cha awali Ujerumani Kombe la Dunia
Muktasari:
- Uamuzi huo unakuja baada ya kuwepo kwa mazungumzo ya siri na ya kina kupitia simu katika siku za karibuni yaliyofanikisha kumshawishi nahodha huyo wa zamani kubadili msimamo wake wa awali wa kuachana na soka la kimataifa.
Kipa nguli wa Bayern Munich, Manuel Neuer anaripotiwa kuwa mbioni kukatisha kustaafu kwake ili kurejea kuitumikia timu ya taifa ya Ujerumani katika michuano ya Kombe la Dunia.
Kocha Mkuu Julian Nagelsmann amemjumuisha kipa huyo mwenye uzoefu mkubwa kwenye orodha yake ya awali ya wachezaji 55 waliochaguliwa kwa ajili ya maandalizi ya michuano hiyo mikubwa duniani.
Uamuzi huo unakuja baada ya kuwepo kwa mazungumzo ya siri na ya kina kupitia simu katika siku za karibuni yaliyofanikisha kumshawishi nahodha huyo wa zamani kubadili msimamo wake wa awali wa kuachana na soka la kimataifa.
Kama Neuer atafanikiwa kuingia kwenye kikosi cha mwisho cha Ujerumani atakuwa anaweka rekodi ya kushiriki michuano ya tano ya Kombe la Dunia.
Hata hivyo, bado haijafahamika kama atarejea kikosini kama chaguo la kwanza langoni au atakubali jukumu la kuwa msaidizi wa makipa wengine chipukizi.
Kwa sasa, Neuer ni mmoja wa makipa watano waliopo kwenye rada za Nagelsmann, ambapo kocha huyo anatarajiwa kupunguza idadi hiyo na kubakiza watatu watakaosafiri kwenda kwenye fainali hizo.