Ujenzi wa viwanja Pemba wafikia pazuri
Muktasari:
- Kamishna wa Idara ya Michezo Zanzibar, Ameir Mohamed Makame amesema muda si mrefu viwanja hivyo vitakuwa na utaratibu wa kukabidhiwa. Amesema, Serikali imepanga viwanja hivyo vitumike kuwanufaisha wanafunzi na vijana kufanya mazoezi.
WAZIRI wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo Zanzibar, Riziki Pembe Juma amesema ameridhishwa na hatua ya ujenzi wa viwanja kisiwani Pemba.
Ameyasema hayo baada ya kukagua viwanja vya Wilaya ikiwemo Mkoani kilichopo Ukutini na Wete kilichopo Pandani.
Ameeleza, viwanja hivyo vipo katika hali nzuri na miundombinu rafiki kwa kila mtu kuanzia watoto, vijana na wenye ulemavu.
“Viwanja hivi vitatumika kukuza vipaji vya michezo mbalimbali na dhamira ya serikali vinufaishe wananchi kisiwani hapa,” amesema na kuwataka wananchi kuvitunza na kuvienzi ili vitumike kama ilivyokusudiwa na sio kinyume cha hapo.
Kamishna wa Idara ya Michezo Zanzibar, Ameir Mohamed Makame amesema muda si mrefu viwanja hivyo vitakuwa na utaratibu wa kukabidhiwa. Amesema, Serikali imepanga viwanja hivyo vitumike kuwanufaisha wanafunzi na vijana kufanya mazoezi.