Malengo ya Raskazone Ligi Kuu Zanzibar
Muktasari:
- Kocha huyo alisema Agosti Mosi 2026, timu hiyo inatarajia kuanza mazoezi ya kujiandaa na msimu wa 2026-2027 ambapo Ligi Kuu Zanzibar itaanza rasmi Agosti 29.
LICHA ya kwamba Raskazone inakwenda kushiriki Ligi Kuu Zanzibar msimu wa 2026-2027 kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa timu hiyo mwaka 2013, lakini kocha Haji Kombo Haji, amesema hawataingia kinyonge.
Kocha huyo alisema Agosti Mosi 2026, timu hiyo inatarajia kuanza mazoezi ya kujiandaa na msimu wa 2026-2027 ambapo Ligi Kuu Zanzibar itaanza rasmi Agosti 29.
Haji alisema, bado wanaendelea na maboresho kwa kusajili wachezaji wenye uwezo wa kupambana na mikiki ya Ligi Kuu huku wakiwa na malengo ya kufanya vizuri zaidi ya ilivyokuwa Ligi Daraja la Kwanza Kanda ya Unguja.
“Kwa sasa ni mapema kutoa idadi ya wachezaji waliosajiliwa lakini tumeacha nane kati yao wawili wameuzwa, hivyo timu inaendelea kusajili.
“Licha ya kwamba ni mara ya kwanza timu kucheza ligi kuu lakini si sababu ya kushindwa kusimamia malengo yetu,” alisema.
Alisema, kutokana na malengo ya kufanya vizuri zaidi baada ya msimu uliopita kumaliza nafasi ya pili Ligi Daraja la Kwanza Unguja na kupanda daraja, ndiyo maana wanasajili kwa umakini mkubwa.
“Niseme tu kwamba, Raskazone itakuwa miongoni mwa timu bora msimu ujao kwani tumejipanga kuhakikisha tunaleta mabadiliko,” alisema.
Timu hiyo ni miongoni mwa nne zilizopanda daraja sambamba na Black Sailors kutoka Unguja, huku Mwenge na Wembe zikitokea Pemba.