Siri ya bao la Miquissone hii hapa
BEKI wa Simba, Erasto Nyoni ameweka wazi siri ya bao lililofungwa na Luis Miquissone kwenye mechi ya nusu fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) dhidi ya Azam FC akifunga dakika ya 87, kwenye Uwanja wa Majimaji, Songea.
Luis alifunga bao hilo baada ya Bernard Morrison kuchezewa rafu na wachezaji wa Azam, na wakati wachezaji wa Azam wakizozana na mwamuzi Morrison aliuanza mpira haraka kwa Luis ambaye alipiga shuti la moja kwa moja nyavuni.
Nyoni alisema waligundua makosa waliyofanya kipindi cha kwanza na yaliwapa nafasi kubwa ya kujirekebisha kile cha pili kutokana na udhaifu ulioonyeshwa na wapinzani wao. “Kipindi cha kwanza tulikuwa taratibu sana kutengeneza nafasi za kufunga kwa haraka, hali ambayo ilitupa wakati mgumu kupenya ngome ya Azam, jambo ambalo kocha na wachezaji tuliliona na kulifanyia kazi mara moja kipindi cha pili kwa kubadilika na kushambulia kwa haraka zaidi tukipata mpira,” alisema
Nyoni alisema walijituma dakika zote kwa kuanzisha mashambulizi ya haraka pindi wanapopata nafasi katika kulishambulia lango la wapinzani wao.
“Baada ya kuingia Morrison mchezo ulikuwa wa tofauti kabisa, kufanyiwa madhambi na Bruce Kangwa alianzisha shambulizi la haraka sana ambalo kwa hali ya kawaida lazima liliwachanganya kwa kiasi kikubwa na tuliweza kunufaika nalo na likatupa matokeo chanya yaliyotupeleka fainali,” alisema. Simba itacheza na Yanga kwenye fainali za ASFC, Julai 25.
IMEANDIKWA NA DAUD ELIBAHATI