Raskazone yajipanga upya ikiokota nne Pemba
Muktasari:
- Raskazone ilicheza na wenyeji wao timu ya Fufuni ikitoka bila kufungana (0-0) na mchezo wa pili ikiichapa Mwenge mabao 2-1.
TIMU ya Raskazone imefanikiwa kuondoka na alama nne ugenini katika michezo yake miwili ya Ligi Kuu Zanzibar iliyocheza kisiwani Pemba.
Raskazone ilicheza na wenyeji wao timu ya Fufuni ikitoka bila kufungana (0-0) na mchezo wa pili ikiichapa Mwenge mabao 2-1.
Matokeo hayo yameifanya Raskazone kuwa timu ya kwanza kati ya nne zilizopanda daraja kupata ushindi katika Ligi Kuu Zanzibar msimu huu.
Akizungumza na Mwanaspoti, Kocha Mkuu wa Raskazone, Salum Ali Haji, amesema kwanza anashukuru kwa kufanikiwa kupata alama hizo ugenini kwani haikuwa rahisi.
Kocha huyo, amesema siri ya kufanikiwa ni kuwaheshimu wapinzani na kutumia nafasi walizozipata ndiyo maana walipata matokeo hayo.
Amesema dhamira yao ilikuwa ni kuondoka na alama zote sita, lakini hata nne walizozipata siyo mbaya, hivyo wanakwenda kujipanga kwa ajili ya michezo mingine kisiwani Unguja.
"Tunarudi nyumbani, tulipoishia ugenini ndicho tutakachokiendeleza, tutafanya bora zaidi kwa sababu tuna malengo yetu na hayawezi kukamilika zaidi tunatakiwa tushinde michezo yetu," amesema.