Mtunisia afichua siri ya Simba, Singida Black Stars
Muktasari:
- Jamus imekuwa gumzo kwenye michuano hiyo baada ya kukusanya pointi nne katika mechi mbili za kwanza za Kundi B, iliianza safari yake kwa kuichapa Singida Black Stars mabao 2-0, kabla ya kutoka suluhu dhidi ya Simba kwenye Uwanja wa Kigali Pele na kujikita kileleni mwa kundi hilo.
KOCHA Mkuu wa Jamus SC ya Sudan Kusini, Saber Ben Jabria amefichua kuwa maandalizi ya mwezi mmoja kabla ya kuanza kwa michuano ya CECAFA Kagame ndiyo siri kubwa iliyowasaidia kuibuka na matokeo mazuri dhidi ya Simba na Singida Black Stars.
Jamus imekuwa gumzo kwenye michuano hiyo baada ya kukusanya pointi nne katika mechi mbili za kwanza za Kundi B, iliianza safari yake kwa kuichapa Singida Black Stars mabao 2-0, kabla ya kutoka suluhu dhidi ya Simba kwenye Uwanja wa Kigali Pele na kujikita kileleni mwa kundi hilo.
Ben Jabria amesema tofauti kubwa iliyopo kati ya timu yake na wapinzani wao wa Tanzania ni muda wa maandalizi.
Wakati Jamus ilifanya kambi ya mwezi mmoja ikiwa na kikosi kamili, Simba na Singida Black Stars zilifika Kagame zikiwa bado zinaendelea na maandalizi ya msimu, huku baadhi ya wachezaji wao wapya wakiwa hawajafikia kiwango bora cha utimamu wa mwili na uelewano.
Kocha huyo raia wa Tunisia amesema kambi hiyo iliwapa nafasi ya kuwajenga wachezaji katika maeneo yote muhimu ikiwemo utimamu wa mwili, mbinu, nidhamu ya kucheza pamoja na kuongeza uelewano ndani ya kikosi, jambo lililoonekana wazi walipokutana na wapinzani wao.
“Tulikuwa kambini kwa mwezi mmoja kabla ya mashindano. Hilo limetupa faida kubwa kwa sababu wachezaji walipata muda wa kuelewana na kufahamu mfumo tunaotaka kucheza. Huwezi kupata mafanikio kama haya bila maandalizi mazuri,” amesema Ben Jabria.
Kocha huyo aliongeza kuwa hakushangazwa na ushindani kutoka kwa Simba na Singida kwa kuwa anafahamu ubora wa timu hizo, lakini aliamini maandalizi bora ndiyo yaliyobadili mizani ya mechi hizo.
Kwa upande wa Simba na Singida Black Stars, michuano ya Kagame imekuwa sehemu ya maandalizi kuelekea msimu wa 2026/27, ambapo makocha wao wamekuwa wakitumia mechi hizo kuwapa nafasi wachezaji wapya kuzoea mifumo ya uchezaji na kujenga muunganiko ndani ya vikosi.