Saliboko ni mali ya Dodoma Jiji
Muktasari:
Chanzo kutoka Dodoma Jiji kimesema Saliboko amesaini mkataba wa miaka miwili, baada ya kufuata utaratibu wa kumalizana na KMC kwani mchezaji huyo bado alikuwa na mkataba, hivyo wasingeweza kumchukua kihuni kisa timu imeshuka daraja.
DODOMA Jiji imekamilisha usajili wa kiungo mshambuliaji Darueshi Saliboko kutoka KMC, ambako msimu uliopita alimaliza akiwa kinara kwa mabao kwenye timu hiyo akifunga matano.
Chanzo kutoka Dodoma Jiji kimesema Saliboko amesaini mkataba wa miaka miwili, baada ya kufuata utaratibu wa kumalizana na KMC kwani mchezaji huyo bado alikuwa na mkataba, hivyo wasingeweza kumchukua kihuni kisa timu imeshuka daraja.
“Ingawa KMC imeshuka daraja, haimaanishi wachezaji si wazuri, wakati mwingine kunakuwa na sababu mbalimbali, kwa upande wetu tunaamini Saliboko ana uwezo mkubwa wa kufunga mabao na ataisaidia timu,” kilisema chanzo hicho na kuongeza;
“Saliboko tayari ameishajiunga katika mazoezi na wachezaji wenzake katika kambi tuliyoweka jijini Arusha kujiandaa na msimu mpya unaoanza Agosti 14, 2026.”
“Ukiachana na mabao matano aliyomaliza nayo msimu uliopita, 2024/25 alikuwa na mabao mawili na alikaa muda mrefu nje ya uwanja kutokana na kusumbuliwa na majeraha na 2023/24 alimaliza na mabao manne.
Alipotafutwa Saliboko ili kuthibitisha hilo amesema: “Timu ambayo itanisajili ndiyo itanitangaza, kikubwa najua msimu ujao nitacheza Ligi Kuu na sitaacha kuwashukuru mashabiki wa KMC ambao walikuwa na sisi nyakati zote.”
Kabla ya Saliboko kumalizana na Dodoma Jiji, timu zingine zilizokuwa zinafukuzia saini yake ilikuwa ni TRA United na Coastal Union ya Tanga.