Man city haijamalizana na Enzo Fernández
Muktasari:
- Chelsea iliweka muda wa mwisho wa saa 11:00 jioni kwa saa za Uingereza, Ijumaa Agosti 14, kwa klabu yoyote inayomtaka Fernández kuwasilisha ofa ya takribani Pauni 120 milioni. Hata hivyo, muda huo ulipita bila Chelsea kupokea ofa rasmi kutoka Manchester City.
MANCHESTER City bado haijaachana na mpango wa kumsajili kiungo wa Chelsea, Enzo Fernández, licha ya kushindwa kuwasilisha ofa rasmi kabla ya muda wa mwisho uliowekwa na Chelsea.
Chelsea iliweka muda wa mwisho wa saa 11:00 jioni kwa saa za Uingereza, Ijumaa Agosti 14, kwa klabu yoyote inayomtaka Fernández kuwasilisha ofa ya takribani Pauni 120 milioni. Hata hivyo, muda huo ulipita bila Chelsea kupokea ofa rasmi kutoka Manchester City.
Baada ya muda huo kupita, masharti ya awali ya makubaliano ya mdomo yaliyokuwa yametolewa kwa wawakilishi wa Fernández yameondolewa, hivyo Chelsea sasa iko katika nafasi nzuri zaidi ya kuamua mustakabali wa nyota huyo.
Pamoja na hali hiyo, Manchester City bado imeendelea kuwasiliana na kambi ya Fernandez katika siku za hivi karibuni, huku klabu hiyo ikijadili uwezekano wa kurejea mezani na pendekezo jipya lenye masharti tofauti.
Chelsea kwa sasa inashikilia udhibiti kamili wa suala hilo, huku ikionekana kutokuwa na haraka ya kumuuza mchezaji huyo ambaye bado ni sehemu muhimu ya mipango ya kikosi hicho kwa msimu mpya.
Kocha wa Manchester City, Enzo Maresca, anatajwa kumhitaji Fernandez katika kikosi chake, huku akiamini uwezo na uzoefu wa kiungo huyo wa Argentina unaweza kuongeza ubora kwenye safu ya kati ya Manchester City.
Hata hivyo, uwezekano wa City kurejea kwenye mazungumzo unategemea pia mustakabali wa Rodri, ambaye amekuwa akihusishwa na uwezekano wa kuondoka kwenda Barcelona.
Kwa sasa, ofa ya Pauni 120 milioni iliyokuwa sehemu ya mpango wa awali haipo tena mezani, lakini hilo halimaanishi kuwa Manchester City imefunga kabisa mlango wa kumsajili Fernández.
Endapo City itaamua kuendelea na mpango huo, klabu hiyo inaweza kurejea na ofa mpya yenye masharti tofauti kabla ya dirisha la usajili kufungwa, huku hatma ya nyota huyo ikiendelea kusubiriwa kwa hamu na mashabiki wa soka.