Prime
Jinsi mtindo wa Rushine unavyomtesa kinyozi Simba
KABLA ya mastaa kama Kylian Mbappe, Jude Bellingham na Erling Haaland kuonekana kwenye kamera wakiwa wamependeza, kuna wakati wanakaa kwenye kiti cha kinyozi na kumkabidhi mtu mwingine jukumu la kuhakikisha kichwa chao kiko katika hali wanayoitaka.
Mmoja wa watu hao ni Ahmed Alsanawi, maarufu kama A Star Barber, kinyozi mwenye jina kubwa nchini England ambaye amewahi kushughulika na nywele za baadhi ya mastaa wakubwa wa soka.
Kazi yake imefika hatua ya kusafiri kwenda kwenye hoteli na maeneo ambayo wachezaji wanakuwa badala ya kusubiri mastaa hao wafike saluni.
Sasa geuza kamera kutoka London ipeleke Mbezi jijini Dar es Salaam, hakuna taa kubwa za London hapa, hakuna mastaa wanaocheza soka la kulipwa Ulaya wanaosubiri mbele ya kamera lakini kuna mashine, viti vitatu vya vinyozi na mtu ambaye kazi yake imeanza kuchukua nafasi inayofanana na hiyo ndani ya soka la Tanzania.
Majina yake ni Kilama Saidi. Kwa zaidi ya miaka 15, amekuwa akifanya kazi ya kunyoa na kutengeneza nywele lakini leo hii si kinyozi anayesubiri mteja aje kwenye saluni yake pekee, bali anamfuata mchezaji nyumbani, ofisini, hotelini na hata mkoani pale anapohitajika.
Ndani ya Simba, anasema karibu asilimia 90 hadi 95 ya wachezaji pamoja na baadhi ya makocha wamewahi kupita mikononi mwake.
Hii ina maana kwamba kabla ya mashabiki kumuona mchezaji wa Simba akiingia uwanjani akiwa na nywele mpya, rangi iliyopangiliwa au ndevu zilizokaa sawasawa, kuna uwezekano mkubwa tayari Saidi alikuwa ameshika mashine yake.
SIMBA ILIVYOANZA
Kupata kwake fursa ya kufanyakazi na Simba hakukuwa jambo lililopangwa, Saidi anaeleza kwamba ilikuwa ni mlango uliofunguliwa na mmoja wa makocha wa kigeni ambaye alimtafuta kupitia ujumbe wa simu.
“Wa kati wa Mungu ni wa kati sahihi. Nili pok ea DM kutoka kwa mmoja wa makocha wa kigeni akahitaji nimfanyie huduma, haikuwa yeye tu, akaniambia pia kuna kocha mwingine na baadhi ya wachezaji, hapo ndipo ulikuwa mwanzo wangu,” anasema na kuongeza.
“Sio kwamba naitwa na timu kwamba niende kuwanyoa wachezaji wote, unakuta nikipokea labda DM za wachezaji wanne, watano, natakiwa niwapate wote, naenda narudi.”
ALIKUTANA NA MASWALI SIMBA
Saidi anasema alipoanza kuhusishwa na Simba, kulikuwa na maswali ambayo alipaswa kuyajibu ili watu wafahamu yeye ni nani na anaingia kwenye mazingira hayo kwa sababu gani lakini kwake kulikuwa na jambo moja lililorahisisha kila kitu alikuwa tayari ni shabiki wa Simba.
“Kwanza kabisa mimi ni shabiki pia wa Simba, kabla ya kuanza kufanya kazi nao nilikuwa shabiki kwa hiyo imekuwa rahisi kwangu kwa sababu ni shabiki na pia nafanya nao kazi,” anasema.
Ushabiki huo, hata hivyo haujampa ruhusa ya kuvuka mipaka ya kazi yake.
Saidi anaeleza wazi kwamba anapokuwa na mchezaji, yeye ni mtoa huduma, mazungumzo yanaweza kuwepo, urafiki unaweza kujengwa lakini mambo ya ndani ya klabu na taarifa ambazo hazihusiani na kazi yake si sehemu ya biashara yake.
KABLA YA DAKIKA 90
Mchezaji anaweza kuja na picha ya staili anayotaka, mwingine anaweza kueleza kwa maneno, mwingine anasema anataka rangi fulani, mwingine anataka ‘dreadlocks’, mwingine anahitaji ndevu ziwekwe sawa, hapo ndipo uzoefu wa miaka 15 unapokuwa silaha yake.
“Hiyo yote ni kwa sababu ya uzoefu wa muda mrefu, mteja anapokuwa anaelezea kwamba nataka staili hii au nataka kuweka rangi hii, kwangu sio ngumu, kulingana na uzoefu wa muda mrefu atanielezea kidogo, nitakuwa nishamwelewa kazi yake vile vile anavyohitaji, kama ana picha anaweza akanionyesha, namfanyia,” anasema.
Picha ambazo amekuwa akionyeshwa imekuwa ikirahisisha kazi yake kutokana na klabu hiyo kuwa na wachezaji kutoka mataifa mbalimbali.
Kuna wanaotoka DR Congo, Senegal, Mali, Ivory Coast, Tanzania na wachezaji kutoka Afrika Kusini. Lugha tofauti zinaweza kuwa kikwazo, lakini Saidi amejifunza namna ya kuvuka changamoto hiyo.
STAA WA KWANZA KUMNYOA
Said anaeleza kwamba mchezaji wa kwanza kwake kumnyoa alikuwa ni kiungo wa Simba, Deborah Fernandez ambaye baadaye akamvuta Elie Mpanzu kwenye huduma hiyo.
“Mchezaji wa kwanza kabisa kumpa huduma hii ya kunyoa alikuwa Deborah Fernandez, nakumbuka alikuja hapa nikamuhudumia akafurahi.
“Baadaye alikuja na Mpanzu, Mpanzu wakati anafika alikuwa anajua Kifaransa na Kilingala tu sasa msaada wangu ulikuwa ni Deborah, yeye alikuwa anajua Kiingereza kidogo na Kifaransa akatusaidia.
FADLU NA WASAIDIZI WAKE, BARKER NAYE
Sikuanza sasa kuwanyoa watu wa Simba nakumbuka kocha wa Simba Fadlu na wasaidizi wake nao nilikuwa nawanyoa mimi kuna wakati walikuwa wanakuja hapa au wakati mwingine nakwenda wanapokaa.
“Baada ya kumnyoa Fadlu mpaka alipoondoka, akafuata huyu kocha wa sasa Steve Barker naye amekuwa akija hapa, anapata huduma na wakati mwingine wasaidizi wake nao wananiita kwahiyo maisha yameendelea
RUSHINE NA “FIRST TOUCH” ILIYOMPA TABU
Katika kazi yake, Saidi anasema hakuna staili ya wachezaji wa Simba ambayo ameshindwa kuifanya, ingawa baadhi zilimpa changamoto mwanzoni, mfano anaoutoa ni wa Rushine De Reuck ambaye alikuja akiwa na staili ambayo ilimuhitaji Saidi kuizoea zaidi.
“Staili anayonyoa Rushine mwanzo ilikuwa inanipa tabu kidogo, lakini kwa sasa imekaa sawa, changamoto hiyo haikunifanya nikate tamaa, nilipopata nafasi nyingine ya kumhudumia, nilitumia uzoefu wa kazi ya kwanza kuboresha ile ya pili na akaridhika,” anasema.
Saidi anasema wakati mwingine kinyozi anaweza kuona kuna sehemu haijakaa kama alivyokusudia, wakati mteja mwenyewe akawa ameridhika. “Kwangu mimi nilikuwa naona ina mapungufu ila kwake yeye alikuwa anaona kazi iko sawa. Kwa hiyo nilipopata nafasi ya pili tena, ikabidi nifanye bora zaidi na akawa yuko fresh.
DREADLOCKS? MDOGO WAKE NDIYE MTAALAMU
Si kila huduma ya nywele anafanya Saidi mwenyewe. Kwa upande wa dreadlocks, anasema mdogo wake ndiye anayeshughulika zaidi na kazi hiyo. Baada ya kumaliza, Saidi huingia kufanya kile kinachoitwa ‘finishing’ hatua ya mwisho inayofanya nywele zikae katika mwonekano unaotakiwa.
“Mdogo wangu ambaye nipo naye, yeye ndio anadili na hizo dread. Akimaliza mimi nakuja kumalizia,” anasema.
DOUMBIA LUGHA NI MOJA TU
Saidi anamtaja Ibrahim Doumbia kama mmoja wa waliompa changamoto zaidi upande wa mawasiliano.
“Doumbia sasa changamoto pale ni lugha, yule anaongea Kifaransa tu, hana lugha mbadala labda Kiingereza kidogo sana tena kwa mbali,” anasema.
Hata hivyo, changamoto hiyo haikuonekana kuwa kubwa katika utekelezaji wa staili aliyohitaji. Doumbia alimwelekeza kwa namna aliyoelewa huku picha na muonekano alioutaka vikisaidia zaidi. “Alikuwa anahitaji ile staili ilikuwa inaonekana pale pale pia ni kuiweka tu vizuri. Alinionesha... nikamweka sawa pale akafurahi. Halafu na ile rangi tuliweka,” anasema.
SH150,000 KICHWA
Gharama ya huduma kwa mchezaji haibaki kwenye kunyoa pekee, bali rangi, mapambo, aina ya staili na muda unaotumika vinaweza kufanya bei ipande. Saidi anasema baadhi ya huduma zinaweza kufika hadi Sh150,000 huku Rushine akiwa miongoni mwa wachezaji wanaoweza kutumia zaidi kutokana na aina ya huduma anayohitaji.
“Hata kwenye Sh150,000 hivi nafika, au Sh100,000, huyu ndio mtu anayetumia gharama kubwa, kwa sababu kuna zile rangi na kuziweka vile vibambucha-bambucha, zinachangamsha kidogo.”
USALAMA NA USAFI
Nyuma ya mitindo yote hiyo kuna jambo ambalo Saidi analipa kipaumbele ambalo ni usafi kwa kuwa anaweza kumhudumia mchezaji mmoja na muda mfupi baadaye akamfuata mwingine, vifaa vinapaswa kuwa safi kabla ya kuanza kazi mpya anasema mashine husafishwa na kupigwa dawa, huku nyembe zikitumika kwa mteja mmoja pekee. “Kwenye suala la usafi tuko vizuri, kabla ya kumpata mchezaji mwingine lazima mashine ihakikishe iko safi, nyembe kutumia huwezi ukarudia mteja mara mbili, ni mteja mmoja nyembe yake.” Anaongeza: “Mashine lazima nipige spiriti na kuna dawa lazima nizipige mashine inakuwa smart. Vitambaa pia natumia visafi, lazima tishu muda wote.”
MBEZI HADI ARUSHA
Saidi ameitaja Arusha kama moja ya maeneo aliyowahi kuwafuata wachezaji kwa ajili ya huduma.
“Gharama inakuwa ni kwa unayemfanyia kazi. Kwa mfano kama wachezaji watatu ndio wamekuita, gharama zinakuwa juu yao.”
Kwa upande wa usafiri, anasema inategemea anakoelekea. “Inategemea na wapi naenda, karibu karibu hapa basi tunaenda haraka na hata Arusha fresh nafika.”
Kilichobaki sasa ni hatua ambayo bado hajaifikia kuwafuata wachezaji nje ya Tanzania. “Ah, nje ya nchi bado bado, inshallah.”
NEO MAEMA FRESH
“Mchezaji ambaye ukipata nafasi ya kumnyoa utafurahia ni Neo Maema, jamaa ni mcheshi sana wakati wote akifika au ukimfuata wakati wote yupo kwenye vaibu anapiga nyimbo za kwao sauz anaimba kidogo, kwahiyo kazi inakwenda huku mnafurahia hizo nyimbo.”
YANGA FRESH TU
Licha ya kwamba Said ni shabiki wa Simba, lakini amekiri kwamba bado hajapata nafasi ya kumnyoa mchezaji yoyote wa Yanga lakini pia hana shida akipata nafasi hiyo.
“Unajua kaka hii ni taaluma yangu, natakiwa kuwa na weledi katika kuifanya, leo nafanya kazi na wachezaji wa Simba haimaanishi kwamba siwezi kumnyoa mchezaji wa Yanga, ikitokea nafanya kazi.