Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Filamu uhamisho wa Mwalimu Yanga, chanzo ni hiki!


USAJILI wa mshambuliaji Selemani Mwalimu kutoka Wydad Casablanca kwenda Yanga ni kama filamu ambayo kila mmoja anatamani kuitazama, shabiki wa Simba anataka kuitazama, wakati huohuo shabiki wa Yanga naye anataka kuitazama.


Kiuhalisia filamu hii imejaa visa, mikasa, matukio ya kushangaza na mengine unaweza kusema ni fedha nyingi ilitumika kuhakikisha kipengele fulani kinarekodi.

Mwalimu siyo mchezaji mkubwa sana kwenye macho ya wengi, mashabiki wa Simba msimu uliopita pamoja na kwamba aliwafungia mabao 10 bado walikuwa wakimlaumu mara kwa mara kuwa alikuwa anakosa mabao ya wazi, lakini filamu hii inakwenda kumtambulisha kivingine kabisa kwenye soka letu, kama akishindwa kuwika basi Simba watashangilia, lakini akiwika Simba watakaa kimya na Yanga watashangilia, msimu ujao unaoanza leo ndiyo unaweza kujibu maswali hayo yote kwa kuwa soka halijifichi.


FILAMU YENYEWE

Kabla msimu uliopita haujamalizika Mwanaspoti liliuripotia umma Yanga wamepeleka ofa ya kumtaka Mwalimu kwa mkopo kutoka kwenye klabu yake ya Wydad, walifanya hivyo kwa kuwa mkataba wa Simba na Mwalimu wa mkopo wa msimu mmoja ulikuwa unamalizika mwishoni mwa msimu wa 2025/2026 na haukuwa na kipengele cha kuongeza mwingine, Yanga ilijibiwa Mwalimu ambaye ni mchezaji wa zamani wa Fountain Gate, hauzwi.

Mara baada ya msimu kumalizika, Simba ilipeleka ombi Wydad la kumtaka mchezaji huyo kwa mkopo tena wa msimu mmoja, mabosi wa Wydad wakawaambia Simba tutazungumza, lakini mchezaji anatakiwa kurudi kwanza Morocco na taratibu nyingine zifuate.

Baada ya hapo Mwalimu alirejea kwenye kikosi chake na mazungumzo kati ya Simba na Wydad yaliendelea, huku mabosi hao wa Morocco wakipandisha dau la usajili huo wa mkopo kutoka Dola 50,000 za awali na kwenda hadi Dola 70,000 hata hivyo, Simba walikubali na kuahidi wapo tayari kutoa fedha hizo, wakamtangaza mchezaji akiwa na jezi ya Simba kuwa na mali yao mpya kwa ajili ya msimu ujao.

Muda mchache baada ya kutangazwa Wydad wakaja juu na kusema hawajamalizana na Simba kuhusu mchezaji huyo na kitendo cha kumtangaza kabla hakikubaliki, bado ni mchezaji wao halali, Simba wakarudi mezani kujadiliana, Wydad wakawaeleza wapo tayari kuwaachia mchezaji huyo, lakini mahitaji yamebadilika na sasa ni Dola 120,000 (sawa na shilingi milioni 317 za Kitanzania).

Baada ya majadiliano ya mabosi wa Simba kulikuwa na ukimya kidogo, Mwalimu ambaye alikuwa amekubaliana na mabosi hao gharama zake za kusaini mkataba ni milioni 160, aliwasiliana na Simba kwa kuwa alitaka kucheza hapo na kuwaeleza yupo tayari kupunguza kiasi cha fedha kwake ili Simba wafanikishe dili hilo.

Bila kumjibu chochote, mabosi wa Simba walikubali kulipa kitita hicho na wakataka mchezaji huyo apande ndege kuja Dar es Salaam. Kumbuka baada ya makubaliano hayo Wydad walikuwa wameshamaliza dili na Simba na wanachosubiri ni kiasi cha cha fedha kiwekwe kwenye akaunti yao, maisha mengine yaendelee.

Makubaliano binafsi ya Simba na Mwalimu ni kulipwa milioni 160 na mshahara wa milioni 12 kwa mwezi, haya hayakuwa na mabishano makubwa kwenye vikao vyao.

Agosti 9, 2026, saa 4:00 asubuhi siku ya Kileleni cha Mwananchi, Yanga wakawa wamepata mchongo mzima kuhusu dau la Mwalimu, mshahara na kila kitu kuhusu mkataba wake, pia wakagundua Simba hajawalipa fedha yoyote kwa Wydad. Kosa kubwa. Wakatumia mwanya huo na kutuma ofa Wydad ya Dola 200,000, wakaongeza mshahara wa mchezaji na dau la kusaini mkataba. Kumbuka dau la mwisho Simba ni Dola 120,000.

Hata hivyo, baada ya Mwalimu kutua Dar es Salaam alitakiwa na mabosi wake kuzungumza na Simba kuhusu kukamilisha dili hilo na alifikisha taarifa.

Juzi Jumatatu mchana mchezaji huyo tegemeo kikosi cha timu ya Taifa, Taifa Stars aliondoka saa 6:00 na kutua Zanzibar na alijiunga na kambi ya Simba akipokea kwa furaha na wachezaji wenzake pamoja na benchi la ufundi, jioni alienda mazoezini lakini baada ya kumaliza mazoezi mambo yakabadilika.


APEWA UJUMBE WA SIMBA

Mara baada ya Mwalimu kumaliza mazoezi, alikutana na email kutoka kwenye klabu yake ya Wydad ikimtaka kuwafikisha Simba ujumbe kuwa tayari timu hiyo imepokea ofa ya Dola 200,000 za Yanga hivyo wenyewe Simba wanataka kusogea hadi Dola 150,000 ili wampate nyota huyo na Wydad waachane na dili la Yanga.

Hata hivyo, mmoja wa mabosi wa Simba aliamini ni mchezo tu unachezwa na hakuna dili kama hilo, hivyo alimwambia mchezaji huyo hawawezi kuongeza zaidi ya dau la mwanzo na kama timu yake inataka basi imtumie tiketi ya ndege staa huyo arudi Morocco.

Kuona hivyo, mazungumzo kati ya Mwalimu na uongozi wake Morocco yaliendelea na mwisho saa 3:00 usiku mchezaji huyo alibeba mabegi yake, akawaaga waalimu wake na kuwaeleza ametakiwa kwenda Uwanja wa Ndege, akiwa njiani Mwalimu alipokelewa na watu wa karibu wa Yanga na alipandishwa ndege saa 6:00 usiku na kutua Dar saa 7:10 na alisaini mkataba wa mkopo wa msimu mmoja na Yanga na saa 12 asubuhi jana akatangazwa. Mambo yakaishia hapo na jana saa 8:00 mchana alitua Zanzibar kuungana na Yanga.


ANAKWENDA KUONGEZA KITU

Mwalimu anakwenda Yanga ambayo tayari ina washambuliaji wengi wakubwa Hussein Mihambo, Peter Shalulile, Cheikh Toure, Clement Mzize uwepo wake kwenye kikosi hicho unakwenda kuongeza ushindani wa namba, pia akipata nafasi itakuwa ni faida kubwa kwa kocha wa Yanga kuwa na washambuliaji wengi bora.

Kwa upande wa Simba ni pigo kubwa kwa kuwa sasa timu hiyo italazimika kuingia soka siku tatu zilizobaki kuhakikisha kuwa inapata mshambuliaji mahiri kwa kuwa imebaki na mmoja tu, Ibrahim Douambia, lakini kocha wa timu hiyo ana faida kwa kuwa anaweza kuipanga timu yake bila mshambuliaji.


ANAKUWA WA TANO

Huyu anakuwa mchezaji wa tano wa Simba kuibukia Yanga ndani ya msimu mitano ambayo Yanga imetawala soka la Bara. Ilianza na Jonas Mkude, baadaye ikamchukua Jean Baleke kabla ya kuinasa saini ya Clotous Chama na baadaye beki imara wa kushoto, Mohamed Hussein.

Hata hivyo ni Tshabalala pekee amefanikiwa kuwashawishi mashabiki wa timu hiyo.