Doumbia aweka tena, Simba yaichapa Al Merrikh Kigali
Muktasari:
- Ushindi huo unakuwa sehemu ya maandalizi ya kikosi hicho kinachotarajiwa kurejea Tanzania kesho, Jumatano baada ya kumaliza kambi yaaandalizi yao hapa nchini Rwanda baada ya kumaliza ushiriki wake katika Kombe la CECAFA Kagame 2026.
KIGALI: SIMBA SC imeendelea kuonyesha dalili nzuri kuelekea msimu mpya wa 2026/27 baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Al Merrikh ya Sudan katika mchezo wa kirafiki uliochezwa leo, Jumanne saa nne asubuhi kwenye Uwanja wa FERWAFA, Kigali, Rwanda.
Ushindi huo unakuwa sehemu ya maandalizi ya kikosi hicho kinachotarajiwa kurejea Tanzania kesho, Jumatano baada ya kumaliza kambi yaaandalizi yao hapa nchini Rwanda baada ya kumaliza ushiriki wake katika Kombe la CECAFA Kagame 2026.
Bao la kwanza la Wekundu wa Msimbazi lilifungwa na Libasse Guaye kipindi cha kwanza, kabla ya Ibrahim Doumbia kuongeza la pili kipindi cha pili na kuendelea kuonyesha makali yake mbele ya lango.
Kwa Doumbia, hilo ni bao la pili katika mechi za maandalizi baada ya kufungua akaunti yake ya mabao kwenye ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Singida Black Stars katika mchezo wa mwisho wa hatua ya makundi wa Kombe la CECAFA Kagame.
Kocha wa Simba, Steve Barker, alitumia mchezo huo kuwapa nafasi wachezaji tofauti huku kila kipindi kikichezwa kwa dakika 35, hatua iliyomwezesha kuendelea kutathmini kikosi chake kabla ya msimu mpya kuanza.
Katika kipindi cha kwanza Barker alianza na kikosi tofauti kilichotawala sehemu kubwa ya mchezo na kufanikiwa kupata bao kupitia Guaye huku kipindi cha pili akifanya mabadiliko kadhaa yaliyoongeza kasi na nguvu ya timu.
Doumbia aliitumia vyema nafasi aliyopewa kwa kufunga bao la pili kupitia pasi ya Morice Abraham lililoihakikishia Simba ushindi, huku akiendelea kujenga kujiamini na kuwapa matumaini mashabiki kwamba anaweza kuwa mmoja wa silaha muhimu za timu msimu huu.