Simba yakaribia kubeba Mnigeria

Simba yakaribia kubeba Mnigeria

Muktasari:

  • MABOSI wa Simba wapo katika hatua za mwisho kuwabeba nyota wawili wa Coastal Union ya Tanga, kiungo Mnigeria Victor Akpan na Abdallah Suleiman ‘Sopu’.

MABOSI wa Simba wapo katika hatua za mwisho kuwabeba nyota wawili wa Coastal Union ya Tanga, kiungo Mnigeria Victor Akpan na Abdallah Suleiman ‘Sopu’.

Mwanaspoti limepenyezewa taarifa kutoka Simba kuwa Sopu anayecheza nafasi ya ushambuliaji na Akpan ambaye ni kiungo mkabaji wanahitajika kuongeza nguvu Msimbazi.

Ikumbukwe Simba ina washambuliaji wanne Kibu Denis, Chris Mugalu, Meddie Kagere na John Bocco huku viungo wakabaji wakiwa ni Mzamiru Yassin, Thadeo Lwanga na Jonas Mkude wengi wao mikataba inamalizika msimu huu na huenda baadhi wakatemwa.

Sopu katika Ligi Kuu amefunga mabao tisa, huku Kombe la Azam (ASFC) akifunga sita akitoa pasi nne na ni moja ya washambuliaji wazawa waliofanya vizuri.

Kaimu Katibu Mkuu wa Coastal Union, Jonathan Tito aliliambia Mwanaspoti kuwa, hata wao wamesikia taarifa juu ya Simba kuwahitaji nyota hao, lakini cha kushangaza hawajafika kwa uongozi. “Wachezaji wetu hawa wote wawili wana mikataba na Coastal Union siwezi kuweka wazi ya muda gani, hivyo Simba wanatakiwa kuja kwa uongozi na kufanya mazungumzo na sio kumfuata mchezaji mwenyewe. Sio sawa hata kidogo, tumesikia lakini kama wako tayari wanawahitaj waje tuongee,” alisema Tito.

Aliwataka Simba kujiepusha na kilichowakuta msimu uliopita kwa aliyekuwa nyota wao Bakar Mwamnyeto badala ya kuongea na uongozi walimfuata wakati ana mkataba. Mtu wa karibu wa Akpan aliiambia Mwanaspoti kuwa, tayari Simba wamemalizana naye.