Wajue wapinzani wa Simba, Yanga kimataifa

DROO ya raundi ya kwanza na pili ya mashindano ya Klabu Afrika msimu wa 2022/2023 imepangwa juzi huko Cairo, Misri ambapo timu zitakazoiwakilisha Tanzania zimeshafahamu wapinzani wake.

Ukiondoa Azam FC ambayo itaanzia raundi ya pili, Simba, Yanga, Geita Gold, KMKM na Kipanga zenyewe zitacheza katika raundi ya kwanza na ambayo kama zitapenye, zitatinga raundi ya pili ambayo hiyo pia imeshapangwa timu wanazoweza kukutana nazo.

Katika raundi ya kwanza, Yanga itakutana na Zalan ya Sudan Kusini, Simba itacheza na Nyasa Big Bullets ya Malawi, Geita Gold itaumana na Hilal Alsahil ya Sudan, KMKM itacheza na Al Ahli Tripoli ya Libya wakati Kipanga imepangwa kukutana na Hilal FC WAU ya Sudan Kusini.

Mwanaspoti linakuletea dondoo za timu hizo zuilizopangwa kukutana na wawakilishi wa Tanzania katika raundi ya kwanza ya mashindano ya klabu Afrika.


Zalan FC Rumbek

Ikitokea katika mji wa Rumbek uliopo katikati mwa nchi ya Sudan Kusini, timu ya Zalan haina umri mrefu tangu ianzishwe kulinganisha na wapinzani wao Yanga kwani yenyewe imeanzishwa mwaka 1999 na hii ni kwa mara ya kwanza inashiriki Ligi ya Mabingwa Afrika.

Wamekuwa wakitumia jezi zenye rangi nyeupe zenye michirizi na maandishi yenye rangi nyekundu na bukta nyekundu pindi wanapocheza mechi ya nyumbani na ugenini huwa wanatumia jezi nyeupe zenye ufito wa bluu au nyeupe na bukta nyeusi.


Kikosi

Timu hiyo inanolewa na kocha Mzawa, Mayor na baadhi ya nyota wake ni Willpower Makoi, Abraham Maker Justin Marial Mathok, Prince Makoi na Kaman Aparer Chut.


Nyasa Big Bullets

Timu hiyo ambayo makao yake makuu yapo katika jiji la Blantyre, inautumia Uwanja wa taifa wa Kamuzu unaoingiza jumla ya mashabiki 40,000.

Ilianzishwa mwaka 1967 wakati huo ikijulikana kama Bata Bullets baadaye ikaitwa Total Big Bullets na kabla ya jina la sasa iliwahi kujulikana kama Bakili Bullets.

Ndio klabu kubwa zaidi ya soka ambayo inaongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya mashabiki, idadi ya mataji pamoja na hali nzuri ya kiuchumi.

Katika mechi za nyumbani imekuwa ikitumia jezi za rangi nyekundu na ikiwa ugenini huvaa rangi nyeupe.


Kikosi

Idadi kubwa ya wachezaji wa timu ya taifa ya Malawi ambao huitwa kutokea kwenye Ligi ya ndani ni wale wanaotokea katika kikosi cha Nyasa Big Bullets.

Mfano wa nyota wanaounda kikosi hicho ni Sankhani Mkandawire, Yamikani Fodya, Chiukepo Msowoya, Righteous Banda na Erick Kaonga.

Timu hiyo inanolewa na kocha Callisto Pasuwa kutoka Zimbabwe.


Hilal Alsahil SC

Ni miongoni mwa klabu kongwe za soka nchini Sudan ikiwa imeanzishwa mwaka 1937 katika jiji la Port Sudan.

Uwanja inaoutumia ni Port Sudan unaoingiza mashabiki 7,000 na katika msimu uliopita ilimaliza ikiwa nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya Sudan.

Ni timu ambayo imeshiriki mashindano ya klabu Afrika mara tano na zote iliishia katika hatua za mwanzoni.

Katika mechi za nyumbani wamekuwa wakipendelea kutumia jezi za bluu na ugenini huwa wanavaa nyeupe


Kikosi

Kikosi cha Hilal Alsahil kinaongozwa na kocha Nadir Haboub na baadhi ya wachezaji wake tegemeo ni Hamza Abbas, Ibrahim Bilton, Mojahed Alageed, Raefat Mohamed na Maikel Aboji.


Al Ahli Tripoli

Ni miongoni mwa timu zenye mafanikio katika soka la Afrika na hapana shaka, KMKM wabna mlima mrefu wa kupanda ili kuitupa nje timu hiyo ya Libya ambayo ilianzishwa mwaka 1950 jijini Tripoli.

Msimu uliopita tu,ilitinga hatua ya nusu fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Ikiwa nyumbani hupendelea kutumia jezi za kijani na ugenini huwa inavaa jezi zenye rangi nyeupe.

Inatumia Uwanja wa Tripoli unaoingiza mashabiki 65,000.


Kikosi

Ahli Tripoli inanolewa na kocha raia wa Misri, Talaat Youssef na baadhi ya nyota wake tegemeo ni Mohamed El-Tarhouni, Saleh Al Taher, Mohammed El Fakih, Jihad Al-Ashhab, Badr Hassan na Mohammad Abu Zrayq


Hilal FC WAU

Hawa ni wapinzani wa Kipanga ya Zanzibar kwenye Kombe la Shirikisho Afrika na timu yao imeanzishwa mwaka

Timu hiyo inapatikana kusini mwa Sudan Kusini na inatumia Uwanja wa Wau unaoingiza jumla ya mashabiki 5,000.