Tajiri miaka 16 atimua makocha 25
Muktasari:
- Tajiri huyo Marinakis pia ni mmiliki wa miamba ya Ugiriki, Olympiacos, pamoja na klabu ya Ureno, Rio Ave.
LONDON, ENGLAND: MMILIKI wa Nottingham Forest, Evangelos Marinakis amemfuta kazi kocha Jose Luis Mendilibar ikiwa ni mara ya 25 kwa mfanyabiashara huyo kubadilisha makocha katika kipindi cha miaka 16 tangu aanze kumiliki klabu mbalimbali.
Tajiri huyo Marinakis pia ni mmiliki wa miamba ya Ugiriki, Olympiacos, pamoja na klabu ya Ureno, Rio Ave.
Mendilibar, 65, ameondoka Olympiacos baada ya kuiongoza timu hiyo kutwaa taji la Conference Ligi mwaka 2024, kabla ya msimu uliofuata kushinda mataji matatu ya ndani.
Hata hivyo, baada ya Olympiacos kushindwa kufuzu Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu huu, uongozi umeamua kufanya mabadiliko katika benchi la ufundi.
Olympiacos ilithibitisha kuondoka kwa Mendilibar kupitia taarifa rasmi, ikimsifu kwa mafanikio aliyoyapata, lakini ikaeleza kuwa safari yake katika klabu hiyo imefikia mwisho.
Taarifa hiyo ilisema: “Katika soka, kama ilivyo katika maisha, kuna mizunguko ambayo hatimaye hufungwa. Lakini kinachobaki milele ni kile ulichokifanikisha.
“Shukrani, heshima na upendo wa familia ya Olympiacos vitakuwa pamoja nawe daima, Jenerali, pamoja na hisia kubwa zilizotuunganisha na zitakazodumu milele.
“Asante kwa kila kitu.”
Kuondoka kwa Mendilibar kunamfanya kuwa kocha wa 25 kuondolewa katika klabu zinazomilikiwa na Marinakis katika kipindi cha miaka 16.
Katika timu ya Nottingham Forest pekee, Marinakis amewatimu makocha kadhaa tangu alipoinunua klabu hiyo mwaka 2017, akiwemo Mark Warburton, Aitor Karanka, Martin O’Neill, Sabri Lamouchi, Chris Hughton na Steve Cooper.
Msimu uliopita ulikuwa wenye mabadiliko makubwa zaidi, ambapo Forest ilitumia makocha wanne. Nuno Espirito Santo alifutwa kazi mapema kabla ya Ange Postecoglou kuchukua nafasi yake, lakini naye akaondolewa baada ya mechi nane bila ushindi.
Sean Dyche, aliyewahi kuzifundisha Burnley na Everton, alipewa jukumu hilo, lakini naye alitimuliwa baada ya mechi 25.
Vitor Pereira alisaidia Forest kuepuka kushuka daraja, lakini klabu iliachana naye baada ya msimu kumalizika.
Wakati kwa timu yake ya Olympiacos kwa sasa inashiriki Europa Ligi na itaanza kampeni yake dhidi ya Jagiellonia Bialystok ya Poland.
Katika Ligi Kuu ya Ugiriki, Olympiacos imeanza vizuri ikiwa nafasi ya tatu baada ya mechi tatu, ikishinda mbili na kutoka sare moja.
Kuondoka kwa Mendilibar kumetangazwa siku moja tu baada ya Marinakis kwenda Ugiriki kumtembelea mshambuliaji wake Ayoub El Kaabi, ambaye amelazwa hospitalini baada ya kuvunjika mguu katika mchezo dhidi ya Volos Jumamosi.
Marinakis alifika hospitalini kumtakia mshambuliaji huyo raia wa Morocco “apate ahueni haraka na kurejea uwanjani”, huku pia akichapisha picha yao pamoja kwenye mitandao ya kijamii na ujumbe wa kumtia moyo.
Makocha waliopita katika klabu za Marinakis
NOTTINGHAM FOREST (tangu 2017 hadi sasa)
Mark Warburton – Alitimuliwa Desemba 2017
Aitor Karanka – Aliondoka Januari 2019
Martin O’Neill – Alitimuliwa Juni 2019
Sabri Lamouchi – Alitimuliwa Oktoba 2020
Chris Hughton – Alitimuliwa Septemba 2021
Steve Cooper – Alitimuliwa Desemba 2023
Nuno Espirito Santo – Alitimuliwa Septemba 2025
Ange Postecoglou – Alitimuliwa Oktoba 2025
Sean Dyche – Alitimuliwa Februari 2026
Vitor Pereira – Aliondoka Julai 2026
OLYMPIACOS (tangu 2010)
Ewald Lienen – Alitimuliwa Agosti 2010
Leonardo Jardim – Alitimuliwa Januari 2013
Michel – Alitimuliwa Januari 2015
Victor Sanchez – Alitimuliwa Agosti 2016
Paulo Bento – Alitimuliwa Machi 2017
Besnik Hasi – Alitimuliwa Septemba 2017
Takis Lemonis – Alitimuliwa Januari 2018
Oscar Garcia – Aliondoka Aprili 2018
Pedro Martins – Alitimuliwa Agosti 2022
Carlos Corberan – Alitimuliwa Septemba 2022
Diego Martinez – Alitimuliwa Desemba 2023
Carlos Carvalhal – Alitimuliwa Februari 2024
RIO AVE (tangu 2023)
Luis Freire – Alitimuliwa Novemba 2024
Petit – Aliondoka mwaka 2025