Maproo katika safari ya pili Bongo
Muktasari:
- Mwanaspoti linawachambua baadhi ya waliorejea na kuna waliofanya vyema na waliochemka hata baada ya kutarajiwa kufanya makubwa. Je, waliorejea sasa itakuaje?
BAADA ya mapro kurejea Yanga, Simba na Azam FC, wanasubiriwa kujitetea wenyewe kwa mashabiki ambao wanawatarajia watakuwa na kiwango kama walichokuwa nacho mwanzo kabla ya kuondoka katika timu hizo.
Mwanaspoti linawachambua baadhi ya waliorejea na kuna waliofanya vyema na waliochemka hata baada ya kutarajiwa kufanya makubwa. Je, waliorejea sasa itakuaje?
KIPRE JUNIOR-AZAM FC
Kiungo mshambuliaji Kipre Junior amethibitisha kuondoka siyo mwisho wa safari na msimu wa 2023/24 akiwa Azam FC, Kipre alimaliza kinara wa asisti (9) na mabao (9), akiboresha rekodi yake ya msimu wa 2022/23 na alifunga mabao mawili tu.
Baada ya kiwango hicho, alitimkia Algeria kujiunga na MC Alger 2024/25 ambao aliisaidia kuchukua ubingwa wa ligi na sasa amerejea kuendeleza kile alichokifanya kabla hajaondoka.
STEPHANE AZIZI KI-YANGA
Kiungo mshambuliaji wa Yanga, Stephane Aziz Ki katika msimu wa 2024/2025 ambao hakuumaliza na kwenda kujiunga na Wydad Casablanca alifunga mabao tisa, asisti saba, nyuma yake 2023/2024 alikuwa kinara wa mabao 21, asisti nane.
Wydad Casablanca hakuwa tegemeo kikosi cha kwanza na timu hiyo ilimaliza nafasi ya tano, huku bingwa ikiwa ni Maghreb Fès.
Aziz Ki baada ya kuachana na Wydad alikwenda kujiunga na Al-Ittihad Tripoli Januari 24, 2026 na katika msimu wa 2026/27 ametangazwa kuwa sehemu ya kikosi cha Yanga, swali linabakia atarejea yule ambaye alitikisa katika usajili wake na utambulisho wake.
GIBRIL SILLAH - AZAM FC
Mshambuliaji Gibril Sillah aliyerejea Azam FC kuwa sehemu ya kikosi hicho msimu wa 2026/27 kwa mara ya kwanza kucheza ligi ya Tanzania akiwa na kikosi hicho 2023/24 alifunga mabao manane.
Sillah alifunga mabao manane dhidi ya Yanga (Yanga 3-2, Oktoba 2023 ),(Azam 2-1 Yanga, Machi 13), (Azam 5-0 KMC, Desemba 7, 2023),(KMC 0-4 Azam, Septemba 19), timu nyingine alizozifunga ni Geita Gold, Mashujaa na Mtibwa Sugar.
Msimu wa mwisho wa 2024/25 wakati anakwenda kujiunga na ES Sétif ya Algeria iliyomaliza nafasi ya 10, alifunga mabao 11 na asisti mbili, amerejea tena katika kikosi hicho na atatakiwa kutegua mtego wake mwenyewe wa kuonyesha kiwango chake cha mwanzo.
Wakati anarejea Azam katokea nchini Libya alikoichezea Al-Ahly.
HAWA WALIWAHI KUFANYA HIVYO
CLATOUS CHAMA
Baada ya kiungo mshambuliaji Clatous Chama, kufanya vizuri 2020/21 aliyomaliza kinara wa asisti 15, mabao manane kiwango chake kiliivutia RS Berkane ya Morocco kumsajili kwa mkopo, ingawa aliporudi kikosini hakuanza na kasi ileile.
Msimu wa 2023/2024 alimaliza na mabao saba, asisti sita, 2024/2025 mabao sita, tatu akiwa na Yanga, msimu uliopita aliporejea Simba kamaliza na mabao manane na asisti saba, bado ameendelea kuwa msaada katika kikosi cha Wanamsimbazi.
LUÍS MIQUISSONE
Msimu wake wa kwanza kuichezea Simba wa 2020/2021 alifunga mabao mabao 13, asisti 15, kisha akanunuliwa na Al Ahly kwa mkataba wa miaka mitatu kuanzia 2021 hadi 2023 ikamtoa kwa mkopo baada ya kukosa nafasi ya kucheza katika timu ya Abha, Simba alirejea msimu wa 2023/24 hakuwa kwenye kiwango kile cha kwanza kisha akaondoka na sasa yupo katika klabu ya UD Songo ya nchini kwao Msumbiji.
TUISILA KISINDA
Baada ya winga Tuisila Kisinda kuonyesha kiwango cha hali ya juu akiwa na Yanga msimu wa kwanza kucheza Ligi ya Tanzania 2020/2021 kisha akatimkia katika klabu ya RS Berkane baada ya kurejea tena kwa Wanajangwani 2022/23 hakuwa na makali kama ya mwanzo na msimu uliopita alikuwa na ya Al-Quwa Al-Jawiya.
EMMANUEL OKWI
Mshambuliaji wa zamani wa Simba, Emmanuel Okwi ambaye kwa sasa amestaafu kucheza uwanjani kwa mara ya kwanza kucheza katika kikosi hicho ilikuwa 2009-2013, kisha akaondoka kwenda kujiunga na Étoile du Sahel mwaka 2013.
Okwi alirejea tena kwa mara nyingine Simba msimu wa 2014/2015 akaondoka kujiunga na SønderjyskE aliporudi mara ya mwisho 2017 hadi 2019 alikuwa kinara wa mabao 20 (2017/18) kabla ya Meddie Kagere kuchukua utawala wa kuibuka na mabao 23 2018/19.
HERITIER MAKAMBO
Msimu wake wa kwanza kuichezea Yanga 2018/19, mshambuliaji Herieter Makambo alifunga mabao 17 hakumaliza msimu akaenda kujiunga na Horoya AC ambako hakuwa na msimu mzuri hata baada ya kurejea kwa Wanajangwani 2021/22 bado hakuweza kufurukuta mbele ya Fiston Mayele aliyemaliza na mabao 16 nyuma ya George Mpole, kabla ya kunyakua kiatu cha ufungaji bora msimu uliopita wa 2022/23 kwa mabao 17, aliyokuwa amegongana na Saido Ntibazonkiza.