Huyu nd'o bingwa mpya LaLiga 2026/27
Muktasari:
- Soka la juu nchini Hispania linarejea mwishoni mwa wiki hii, huku msimu wa La Liga 2026/27 ukianza, ambapo Barcelona inaingia ikiwa bingwa mtetezi, lakini mpinzani mkubwa Real Madrid ana kocha anayefahamiana vyema na ushindani, jambo ambalo bila shaka litaongeza msisimko katika mechi za El Clasico na mbio za kuwania ubingwa.
SEVILLA, HISPANIA: NANI atatwaa ubingwa wa Ligi Kuu Hispania (La Liga) msimu wa 2026/27? Ni timu zipi zitafuzu Ligi ya Mabingwa Ulaya? Na ni zipi zitashuka daraja? Maswali yote hayo muhimu yanajibiwa kupitia utabiri uliofanywa na supercomputer ya Opta.
Soka la juu nchini Hispania linarejea mwishoni mwa wiki hii, huku msimu wa La Liga 2026/27 ukianza, ambapo Barcelona inaingia ikiwa bingwa mtetezi, lakini mpinzani mkubwa Real Madrid ana kocha anayefahamiana vyema na ushindani, jambo ambalo bila shaka litaongeza msisimko katika mechi za El Clasico na mbio za kuwania ubingwa.
Wakati huohuo, timu tatu zinazofahamika zimerudi La Liga baada ya kutokuwepo kwa muda mrefu, huku zote tatu zikiwa zimewahi kushuka hadi daraja la tatu. Lakini, unaionaje vita ya ubingwa, mbio za kufuzu Ligi ya Mabingwa na vita ya kutoshuka daraja? Supercomputer ya Opta imefanya utabiri wake na haya ndiyo matokeo yake.
VITA YA UBINGWA
Je, Barcelona itatwaa ubingwa wa ligi mara tatu mfululizo? Supercomputer ya Opta inaamini hivyo. Barca ilitumia kikamilifu msimu uliopita uliokuwa na misukosuko kwa Real Madrid na kufanikiwa kutetea taji, tena kwa mtindo wa kuvutia ikiwafunga wapinzani wake hao katika El Clasico iliyochezwa Camp Nou Mei 10 na kuthibitisha ubingwa ikiwa imesalia michezo mitatu.
Mwisho wa msimu, Barcelona ilimaliza ikiwa na tofauti ya pointi nane dhidi ya wapinzani wao hao wakubwa na kutwaa ubingwa wa Hispania kwa mara ya 29. Lakini, kutwaa ubingwa mara tatu mfululizo msimu ujao kutaipa taji lake la 30 la La Liga, huku ikiendelea kuifukuzia Real Madrid yenye mataji 36. Barca katika utabiri uliotolewa inatabiriwa kubeba ubingwa kwa asilimia 45.6 ikiwa juu ya timu zote.
Real Madrid imefanya juhudi kubwa kurekebisha mambo msimu huu. Baada ya kumteua Xabi Alonso, ambaye alikuwa kocha mpya mwenye mvuto msimu uliopita, safari hii wamechagua njia ya "kuaminika na iliyojaribiwa" kwa kumteua Jose Mourinho kwa mara ya pili kuwa kocha.
Kocha huyo Mreno ni mmoja wa makocha wakubwa katika historia ya soka, ingawa amekuwa nje ya kilele cha soka kwa muda. Timu zake tatu za mwisho alizofundisha ni Roma, Fenerbahce na Benfica. Ingawa ni kubwa, Real Madrid iko katika kiwango kingine kabisa.
Inaaminika Mourinho amepewa jukumu la kudhibiti wachezaji wenye majina makubwa katika chumba cha kubadilishia nguo cha Madrid na kutobadilisha kwa kiasi kikubwa mfumo wa uchezaji wa timu. Mtazamo wake wa kiutendaji na wenye nidhamu unaweza kuendana zaidi na mastaa waliopo kikosini.
Kulikuwa na matukio kadhaa ya migongano ndani ya klabu msimu uliopita, hivyo inaeleweka kwa nini viongozi waliamua kumteua kocha mwenye mamlaka na anayeheshimika badala ya anayejulikana zaidi kwa ubunifu wa kiufundi. Mkakati kama huo uliwahi kuifanikisha Madrid chini ya Carlo Ancelotti. Je, "Special One" anaweza kuwabeba? Inawezekana. Katika simulizi za supercomputer ya Opta, Real Madrid inapewa ubingwa kwa asilimia 31.0. Hata hivyo, Barcelona huenda ikawa na nafasi kubwa katika kuamua hilo kama ilivyo kwa Mourinho mwenyewe.
KUFUZU LIGI YA MABINGWA
Unaweza kudhani kwa kiasi kikubwa kwamba nafasi mbili za Ligi ya Mabingwa zitakwenda kwa Barcelona na Real Madrid, zikitarajiwa kumaliza ndani ya nne bora kwa zaidi ya asilimia 81 kabla hata ya kuzingatia uwezekano wa nafasi ya tano tena kutoa tiketi ya kufuzu Ligi ya Mabingwa.
Bila kushangaza, Atletico Madrid ndiyo timu inayofuata kuwa na uwezekano mkubwa wa kumaliza ndani ya nne bora kwa asilimia 48.6. Atletico haijawahi kumaliza nje ya nne bora tangu 2011/12. Baada ya hapo, mambo yanakuwa magumu zaidi kutabirika.
Supercomputer inaipa Villarreal asilimia 29.5 na Real Betis 23.0 zikitarajiwa kushiriki kutokana na kumaliza katika nafasi ya tatu na ya tano, mtawalia msimu uliopita. Hata hivyo, Villarreal iko katika kipindi cha mabadiliko. Kocha Marcelino aliondoka mwishoni mwa msimu uliopita na ingawa mrithi wake, Inigo Perez anaheshimika baada ya kufanya kazi nzuri Rayo Vallecano, hakuna uhakika kwamba kila kitu kitakwenda vizuri.
Kwa upande wa Betis, haijashiriki Ligi ya Mabingwa tangu 2004/05. Itakuwa vigumu kutabiri namna itakavyosawazisha na kufuzu. Kuna timu nyingine tano ambazo zimepewa angalau asilimia 10 ya uwezekano wa kufuzu Ligi ya Mabingwa kupitia kumaliza ndani ya nne bora.
Valencia inapewa asilimia 17.7 ndiyo inayofuata, jambo ambalo huenda likawashangaza baadhi ya watu. Tangu ilipomaliza nafasi ya nne 2018/19, Valencia imekuwa ikibadilisha kati ya kumaliza nafasi ya tisa na nusu ya chini ya msimamo kila msimu. Msimu uliopita ilimaliza nafasi ya tisa. Kwa kufuata mwenendo huo, inatarajiwa kumaliza nusu ya chini msimu ujao, lakini huenda huu ukawa msimu wa kuvunja mwenendo huo.
Baada yake ni Rayo Vallecano (16.7%), ambayo ilifika fainali ya UEFA Conference League msimu uliopita, lakini ikafungwa bao 1-0 na Crystal Palace. Kama ilivyoelezwa, Rayo ilimpoteza kocha Perez ambaye alihamia Villarreal, huku pia kukiwa na sintofahamu kuhusu uwanja ambao timu hiyo itautumia kwa mechi zake za nyumbani. Mwezi uliopita, mamlaka za Jiji la Madrid zilisimamisha kwa muda matumizi ya Rayo ya uwanja wake wa Vallecas baada ya ukaguzi kubaini "matokeo ya kukatisha tamaa kuhusu matengenezo ya uwanja".
Awali, kulikuwa na taarifa kwamba uwanja huo unaweza kufungwa kwa muda wa miezi miwili hadi sita, hali ambayo rais wa Rayo alisema ingeweza kuifanya timu ishuke daraja. Hata hivyo, hali hiyo imebadilika baada ya klabu kufungua uwanja ili kuanza usafi. Pamoja na hayo, inaonekana siyo rahisi Vallecas kuwa tayari kuandaa mchezo wa kwanza nyumbani Agosti 20 kutokana na matatizo hayo.
Kucheza muda mrefu nje ya uwanja wa nyumbani bila shaka kunaweza kuathiri uwezo wa Rayo kupata pointi, lakini supercomputer haikuweza kuzingatia suala hilo katika utabiri wake. Kwa uhalisia, timu kama Celta Vigo (16.7%), iliyomaliza nafasi ya sita msimu uliopita, Athletic Club (11.7%) na Real Sociedad (10.9%) zinaweza kuwa na matumaini zaidi ya kufuzu michuano ya Ulaya kuliko Rayo.
KUEPUKA KUSHUKA DARAJA
Vita ya kutoshuka daraja imekuwa kali katika misimu miwili iliyopita ya La Liga, ambapo 2024/25, timu tano zilimaliza zikiwa na tofauti ya si zaidi ya pointi mbili dhidi ya timu tatu za mwisho. Msimu uliopita, Sevilla iliyomaliza nafasi ya 13 ilikuwa na tofauti ya pointi moja tu dhidi ya Mallorca iliyokuwa katika nafasi ya mwisho ya kushuka daraja.
Mallorca ilishuka daraja licha ya kukusanya pointi 42. Ni mara moja tu kabla katika msimu wa La Liga wenye mechi 38 ambapo timu ilishuka ikiwa na zaidi ya pointi hizo, bila kuhesabu timu zilizoshuka kupitia mchujo. Ni mapema kusema kwamba utashuhudia hali kama hiyo tena, lakini vita nyingine kali ya kutoshuka daraja kwa msimu wa tatu mfululizo haitakuwa jambo la kushangaza kutokana na yaliyotokea misimu miwili iliyopita. Na supercomputer ya Opta inaamini huenda kukawa na timu kubwa itakayoshuka.
Sevilla ilihusika katika vita ya kutoshuka daraja katika misimu miwili iliyopita, na ule wa 2024/25, ilinusurika kwa shida baada ya kukusanya pointi 41, ikiwa mbele ya Leganes iliyokuwa na 40. Kama Leganes ingeifunga Sevilla kwenye Uwanja wa Ramon Sanchez-Pizjuan katika mchezo wa 34 wa msimu huo jambo ambalo ilipaswa kulifanya, timu hizo zingebadilishana nafasi.
Sevilla ilionekana kuelekea moja kwa moja kushuka daraja katika nusu ya pili ya msimu uliopita, lakini ilishinda michezo minne kati ya sita kuanzia Aprili 11 na hivyo kupata nafasi ya kupoteza mechi zake mbili za mwisho bila kushuka. Hata hivyo, supercomputer inaamini huenda safari hii isinusurike. Sevilla ina uwezekano wa kushuka daraja kwa asilimia 27.7, jambo linaloifanya kuwa timu ya tatu yenye uwezekano mkubwa zaidi wa kushuka. Ukizingatia pia matatizo yake makubwa ya kifedha, ilikuwa na kiwango cha pili cha chini zaidi cha mishahara La Liga kwa mujibu wa takwimu za mwisho za Machi 2026, migogoro katika uongozi wa klabu na uwezekano wa kulazimika kuwapandisha wachezaji wengi kutoka timu yake ya vijana ambayo yenyewe ilishuka hadi daraja la nne msimu uliopita, mustakabali wao unaonekana kuwa mgumu zaidi.
DEPORTIVO LA LIGA
Timu nyingine inayofahamika vizuri kwa hali ngumu baada ya vipindi vya mafanikio ni Deportivo La Coruna au Deportivo A Coruna kama inavyojulikana sasa kwa kurejea jina la jiji hilo katika lugha ya Kigalisia.
Deportivo imerejea La Liga tangu 2017/18 iliposhuka na tangu wakati huo imetumia miaka minne katika daraja la tatu. Ilipanda daraja msimu uliopita baada ya kumaliza nafasi ya pili Segunda maarufu pia kama La Liga 2. Hata hivyo, supercomputer inaiona kuwa timu inayopewa zaidi nafasi ya kushuka daraja, ikiwa na uwezekano wa asilimia 29.2.
Deportivo ilimaliza nyuma ya mabingwa wa Segunda, Racing Santander, ambao nao walikuwa wamekaa muda mrefu zaidi nje ya La Liga.
Racing ilicheza La Liga mara ya mwisho 2011/12 na msimu uliofuata ilishuka tena hadi daraja la tatu, lakini tangu ishuke La Liga miaka 14 iliyopita imetumia muda mwingi daraja la tatu yaani misimu saba sawa na muda iliyotumia Segunda, ambayo pia ni misimu saba.
Supercomputer inaipa Racing asilimia 26.9 za uwezekano mdogo wa kushuka kuliko Sevilla, Deportivo na Elche inazozipa 28.4. Hata hivyo, kwa kuwa imepewa nafasi ya nne kwa uwezekano mkubwa wa kushuka inatarajiwa kuwa katika vita kali ya kuwania nafasi ya kubaki ligi kuu.
MALAGA NDANI
Malaga ndiyo timu ya tatu na ya mwisho iliyopanda daraja, baada ya kufanikiwa kupitia mechi za mchujo dhidi ya Almeria.
Nayo imehitimisha kipindi kirefu bila kucheza ligi kuu, ikiwa ilicheza La Liga mara ya mwisho wakati iliposhuka daraja pamoja na Deportivo msimu wa 2017/18. Malaga ilikuwa bado inacheza daraja la tatu msimu wa 2023/24.
Kwa mujibu wa supercomputer, Malaga ndiyo iliyoshuka mara chache zaidi kati ya timu tatu zilizopanda daraja, ikiwa na uwezekano wa asilimia 25.3. Espanyol (26.5%) nayo inao uwezekano mkubwa wa kushuka daraja zaidi kuliko Los Boquerones. Hata hivyo, kila timu, kwa mujibu wa kompyuta hiyo inapewa nafasi ya kushinda ubingwa angalau mara 140. Kwa hiyo, bado kila timu ina nafasi!