Prime
Aubameyang 'kaiba' pesa za mafuta amerudi nyumbani
DAMU yetu sisi Waafrika haina jambo dogo. Haijawahi kuacha uhuni. Jumatatu usiku nilikuwa namtazama mhuni mwenzetu, Pierre-Emerick Aubameyang. Marseille walikuwa wanacheza na PSG. Nilitabasamu. Nilimkumbuka ghafla rafiki yangu Pierre-Emerick Aubameyang.
Alikuwa katika fomu nzuri tu. Nikakumbuka kwamba mwishoni mwa msimu uliopita alikwenda zake Saudi Arabia kukipiga klabu ya Al-Quadsiah. Ilikuwa Julai, mwaka jana. Yeye na wakala wake inaonekana walikuwa na mpango mmoja tu. Kwamba pesa za Waarabu zisiwapite. Auba, kama ninavyopenda kumuita akasaini mkataba mnono wa Euro milioni nane kwa mwaka.
Kipi bora kuliko pesa? Nadhani akili ya Auba na wakala wake ilikuwa kutopitwa na pesa za Waarabu. Akaenda kule kubeba noti zao. Alikuwa na msimu mzuri kwa mujibu wa viwango vya mpira wa Uarabuni. Alifunga mabao 17 katika mechi 32. Siyo mbaya sana ingawa pia siyo nzuri sana. Haya mabao angefunga akiwa England au Hispania yangehesabika kuwa mengi zaidi.
Kitu cha msingi ni kwamba Waarabu wamelipa mshahara wa Euro milioni nane kwa ajili ya mabao 17. Auba hakutaka kuona pesa za Waarabu zinampita bila ya kuzinyakua. Na baada ya kuzipata ameamua kurudi zake Ufaransa kucheza Ligi Kuu. Lakini pia anacheza katika michuano ya Ligi ya Mabingwa wa Ulaya. Alikwenda tu kukwapua pesa zilizozagaa na kisha akageuza zake nyumbani.
Kuna mambo naanza kuyahisi kuhusu soka la Waarabu. Kuna wachezaji wanakosa maisha wanayoyapenda kwa sababu ya tabia zao za ovyo ambazo Waarabu hawana. Ni kama Auba tu. Aliamua afuate pesa kwa kipindi kifupi kisha arudi nyumbani. Lakini kuna maisha ambayo aliyakosa. Kuishi katika JiJi la Marseille ni tofauti na kuishi Riyadh.
Aliamua kuvumilia miezi michache tu ya kukosa uhuru wa kunywa pombe na kwenda klabu za usiku ili apate pesa nyingi za kuzurura katika kasino za Marseille, Paris, Lyon na kwingineko. Baada ya kuona kiasi cha pesa kimetimia katika akaunti akaamua kumwambia wakala wake wafunge mizigo warudi zao Ufaransa.
Auba ni miongoni mwa wachezaji ambao wamerudi kutoka Saudi Arabia kwa sababu pesa siyo kila kitu. Kuna maisha mengine ambayo wachezaji kama wanadamu wamekulia katika tamaduni zao na labda wanaona hawaendi sawa na tamaduni za Saudia na wanashindwa kuishi.
Kuna baadhi ya wachezaji nawaelewa. Sioni kama Saudia itawapa shida. Cristiano Ronaldo Saudia haiwezi kumpa shida. Ni mmoja kati ya wachezaji wenye nidhamu duniani ndiyo maana mpaka katika umri wa miaka 41 bado anaendelea kupambana wakati huu Wayne Rooney mwenye umri mdogo kwake akiwa amenenepa kwa kula kitimoto huku akiwa amefukuzwa timu ya nne katika kazi yake ya ukocha.
Sadio Mane anaweza kuishi maisha ya Saudia kwa sababu ni ustaadhi ambaye anaweza kuishi maisha yote. Hana mambo mengi. Vitu viwili anaweza kuvimudu kwa urahisi tu katika staili ya maisha yake. Uwanja wa kuchezea mpira na msikiti. Kama vyote vinapatikana Saudia Arabia, basi Sadio anaweza kuishi kwa miaka hata 20 ijayo hana tatizo.
Tatizo lipo kwa ndugu zetu kina Auba. Wale wazee wa kukesha katika klabu za usiku. Kama unakumbuka ni kwamba sababu ya msingi ya Aubameyang kuondoka Arsenal ilikuwa ni utovu wa nidhamu. Baada ya kudai kwamba alikuwa na matatizo ya kifamilia nyumbani kwake Paris, Aubameyang aliondoka London kwa ruhusa nzuri tu ya Mikel Arteta, lakini akaongeza siku zake za starehe na kuchelewa kurudi London.
Na sasa nimeanza kuhisi kwamba hata kasi ya wachezaji kwenda Saudia imeanza kupungua. Wale wachezaji wa aina ya Aubameyang wameanza kukacha mapema kwenda Saudia tofauti na misimu miwili iliyopita. Katika dirisha kubwa lililopita hakuna mchezaji mkubwa ambaye amekwenda Saudia.
Hakuna mchezaji anayesumbua Ulaya ambaye ghafla ametuambia anakwenda Saudia. Nadhani wameanza kuambiana kwamba aina ya maisha ya Saudia siyo mazuri tofauti na vile ambavyo wamekuwa wakijiachia katika miji mbalimbali ya Ulaya wanakocheza soka kisha usiku wakaenda katika baa kulewa na kucheza kamari.
Binafsi niliamini kwamba mchezaji kama Kevin De Bruyne angeishia Saudia baada ya kuagwa pale Ettihad mwishoni mwa msimu uliopita. Matokeo yake akaamua kwenda Napoli katika mji wa wahuni ambao ulimfaa zaidi Diego Maradona kutokana na tabia zake za kupenda kuvuta bangi na kutumia cocaine.
Nilidhani pia mchezaji mwenye jina kubwa kama Mo Salah angeamua kwenda zake Saudia, lakini akaamua kubaki katika Ligi Kuu England. Kifupi sijaona kama kuna mchezaji mwenye jina kubwa katika ligi kuu za Ulaya ambaye aliamua kufuata nyayo za kina Ronaldo kwenda Saudia Arabia. Inawezekana mambo hayapo sawa.
Inanikumbusha wakati ule Wachina walipoanzisha ligi ya kufikirika katika vichwa vyao. Mchezaji wa kwanza kuvutika na noti zao alikuwa Oscar wa Chelsea. Hatukuamini. Katika umri wa miaka 26 tu Oscar akaamua kwenda zake kwa Wachina huku dunia ikiamini kwamba alikuwa katika njia ya kuwa mmoja kati ya viungo bora duniani. Wengine tulidhani angekuwa mrithi wa Kaka. Haikuwezekana.
Baadaye wachezaji walitimka zao China. Na baadaye mradi mzima wa kuifanya Ligi Kuu China iwe kama ya England ukafa. Mpaka sasa hausikii kama kuna wachezaji wa timu mbalimbali kubwa na ndogo wanatiririka China. Siyo kweli. Mradi ulikufa na nahisi kwamba hata mradi huu wa Saudia unaweza kufa kifo cha mende.
Na katika hayo mfano wa Auba unatia hofu pia. Kwamba msimu mmoja aliocheza kule ameona kwamba imetosha. Amecheza miezi 12 amevuta pochi lake ameamua kutulia katika Jiji la Marseille. Anatamani tu aishi anavyojisikia. Watoto wa Kifaransa ndivyo walivyo. Unawakumbuka kina Samir Nasri, Karim Benzema, Hatem Ben Arfa walivyokuwa wanaishi?