Athari ya dawa kwenye nywele
Muktasari:
- Wataalamu wa ngozi wamekuwa wakionya kuhusu matumizi ya dawa za kulainisha na kunyoosha nywele, hasa zinapotumiwa mara kwa mara au bila kufuata maelekezo. Utafiti wa mwaka 2016 wa madaktari wa ngozi kutoka Chuo cha Tiba cha Georgia kilichopo Marekani umeonyesha kuwa dawa hizo zinaweza kupunguza uimara wa nywele na kuzifanya ziwe rahisi kukatika na kuwa nyembamba.
KUNA watu wanaingia saluni na kusema, “Nataka nywele zikae hivi,” bila hata kuuliza dawa inayowekwa kichwani inaweza kufanya nini baada ya muda. Uzuri wa nywele unapendeza, lakini wakati mwingine kile kinachofanya nywele zionekane laini na nzuri leo kinaweza kuwa chanzo cha kukatika, kuwasha na hata kupotea kwa nywele kesho.
Wataalamu wa ngozi wamekuwa wakionya kuhusu matumizi ya dawa za kulainisha na kunyoosha nywele, hasa zinapotumiwa mara kwa mara au bila kufuata maelekezo. Utafiti wa mwaka 2016 wa madaktari wa ngozi kutoka Chuo cha Tiba cha Georgia kilichopo Marekani umeonyesha kuwa dawa hizo zinaweza kupunguza uimara wa nywele na kuzifanya ziwe rahisi kukatika na kuwa nyembamba.
NYWELE KUKATIKA
Moja ya madhara yanayoweza kuonekana ni nywele kuanza kukatika. Kemikali zinazotumika kulainisha au kunyoosha nywele hubadilisha muundo wa nywele. Zikitumiwa kupita kiasi, nywele zinaweza kupoteza nguvu yake na kuwa dhaifu.
Daktari Vanessa Richardson anaeleza; “Dawa hizo zinaweza kupunguza uimara wa nywele na kuongeza uwezekano wa nywele kukatika na kuwa nyembamba.”
Hujawahi kukutana na mtu ambaye nywele zake za mbele zimekatika kabisa au kama ana upara hivi, mara nyingi utasikia mtu analalamika ni uzazi au kunyonyesha lakini wengi ni dawa zimewakataa.
NYWELE KUPUNGUA
Mtu anaweza kuanza kuona nywele zake zinapungua taratibu, hasa kama dawa inatumika mara nyingi. Tatizo linaweza kuonekana zaidi kwenye maeneo ambayo tayari nywele zake ni dhaifu (mbele).
Utakuwa shahidi kwamba, mtu anapokuwa na nywele za asili huwa na ujazo tofauti kabisa na zile za dawa ulishawahi kuwaza kwa nini nywele hata ziwe nyingi zikiwekwa dawa zinanywea na huwa zinaenda wapi, hiyo ndio nguvu ya kemikali na ikitokea ikazidi basi zitakatika.
NGOZI YA KICHWA KUUNGUA
Dawa inapowekwa kichwani kwa muda mrefu kuliko inavyotakiwa, inaweza kusababisha muwasho au hata kuunguza ngozi.
Hali hii inaweza kuwa mbaya zaidi ikiwa ngozi tayari ina kidonda au imechubuka.
Madaktari wanaonya kuwa matumizi yasiyo sahihi yanaweza kusababisha ngozi kuwasha na kuungua kwa kemikali.
Katika hali kali, jeraha hilo linaweza kuhusishwa na upotevu wa nywele unaoacha makovu.
NYWELE KUPOTEZA MWONEKANO
Dawa inapozidi kutumiwa, nywele zinaweza kupoteza ulaini na uimara wake. Badala ya kuonekana zenye afya, zinaweza kuwa kavu, dhaifu na kukatika kirahisi.
Mara nyingi watu wenye nywele za asili huwa na rangi moja (nyeusi)lakini mtu ambaye anatumia dawa kwa muda mrefu utaona zinabadilika rangi na kuanza kuwa na uwekundu hivi kwa mbali hasa dawa hiyo inapoanza kuisha.
WATAALAMU WANAONYA
Wataalamu wanashauri mtu asitumie dawa kwa mazoea bila kuangalia hali ya nywele na ngozi ya kichwa.
Muhimu pia ni kufuata muda uliowekwa kwenye dawa na kuepuka kuendelea kuitumia ikiwa inasababisha maumivu makali au kuungua.
Kwa kifupi, nywele nzuri si lazima ziwe nywele zilizowekewa dawa nyingi. Uzuri unaokwenda pamoja na afya ni ule unaolinda nywele na ngozi ya kichwa kwa muda mrefu.
USHAURI
Jamani unapofanya jambo leo jiulize madhara yake wengi wanaotumia kemikali kwenye nywele ni kama wanacheza bahati nasibu kwa sababu mwanzoni anakuwa hajui ipi itamkubali au hiyo iliyomkubali ni lini itadunda.