Rapcha aachia albamu ya kwanza

Hatimaye msanii wa Hiphop anayewika  nchini Tanzania, Cosmas Paul Mfoy maarufu ‘Rapcha’ ameachia album yake ya kwanza iliyopewa jina la ‘Wanangu 99’.

Rapcha ameachia albam hiyo ndani ya kipindi cha miezi mitatu tu baada ya kuachia ngoma yake ya ‘Lissa’ ambayo inaendelea kufanya vizuri na kushika chati za juu za muziki wa Bongofleva.

Hadi sasa wimbo huo una zaidi ya watazamaji milioni 1.5 kwenye mtandao wa YouTube huku albamu yake mpya ikianza kupatikana kupitia streaming platform namba moja ya muziki barani Afrika, Boomplay.

Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa albam hiyo, Rapcha ambaye kwa sasa yupo chini ya usimamizi wa ‘Bongo Records’ alisema;

“Nyimbo zote zilizomo kwenye albamu yangu zinazungumzia baadhi ya vitu ambavyo mimi binafsi nimevipitia katika maisha yangu halisi. Kupitia albamu hii, nataka mashabiki zangu wamuelewe Rapcha ni nani, kitu ambacho kimenisukuma kutengeneza albam ambayo nina uhakika wa asilimia 100 mashabiki zangu wataipenda”.

Kwa upande wake, Muanzilishi na Mkurugenzi wa Lebo ya ‘Bongo Records’, Paul Matthysse maarufu P-funk ambaye pia ni Meneja wa msanii Rapcha alisema ana uhakika mashabiki zake wataipenda kazi hiyo.

“Katika kipindi kifupi sana, Rapcha ameweza kuwa moja ya wasanii wakubwa wa Hiphop nchini Tanzania, ameachia ngoma kali ambazo zimevunja rekodi ya chati mbalimbali za muziki wa Bongo. Nina uhakika kupitia albamu hii, Rapcha anaenda kuwa msanii namba moja wa Hiphop nchini Tanzania,”

Albamu ya ‘Wanangu 99’ ina jumla ya nyimbo kumi ambazo ni: Majani, Go Rapcha, Unaua vibe remix, Nitakucheki, Kama unae, Tunajimwaga, Wanangu, Mungu na masela, Lissa I na Lissa II.

Katika albam hiyo, Rapcha amewashirikisha wasanii wanne ambao ni Femi One, King Kaka, Mapanch BMB na Kid Golden pia  imesimamiwa na watayarishaji mbalimbali wanaofanya vizuri kwenye muziki wa Bongo akiwemoP-Funk-Majani, Cukie Day, Mr. International, Gachi B, Baddest Beats, Aloneym na Chizan Brain

Kwa sasa, albam hiyo yenye nyimbo 10 inapatikana katika streaming platform ya Boomplay tu kwa muda wa wiki mbili.