Jux afunguka kuhusu mwonekano wake, mkewe abadili jina
Muktasari:
- Mabadiliko ya mwili wa Jux yamekuwa gumzo katika mitandao ya kijamii, hasa baada ya kuonekana akiwa mwembamba zaidi tofauti na hapo awali ilivyozoeleka.
BAADA ya mashabiki kuanza kuhoji afya ya msanii Juma Jux kutokana na kupungua kwa mwili wake, mwanamuziki huyo amesema hakuna shida yoyote huku akibainisha kwamba ameridhishwa na mwonekano alionao sasa.
Mabadiliko ya mwili wa Jux yamekuwa gumzo katika mitandao ya kijamii, hasa baada ya kuonekana akiwa mwembamba zaidi tofauti na hapo awali ilivyozoeleka.
Baadhi ya mashabiki wameingiwa na wasiwasi, wakitaka kujua kama kuna tatizo lolote la kiafya, wakati wengine wakianza kujiuliza kama msanii huyo anafanya project au maandalizi yanayomtaka kupunguza mwili. Hata hivyo, Jux mwenyewe ameamua kulijibu suala hilo.
Akizungumza na Mwanaspoti, Jux alipoulizwa kuhusu afya na mwonekano wake, ikiwa amejipunguza kwa ajili ya project fulani au kuna sababu nyingine iliyosababisha mabadiliko hayo, amesema ameridhishwa kabisa na hali yake ya sasa.
“Nimeridhishwa kabisa na mwonekano wangu wa sasa. Sina mpango wa kurudi kwenye umbo langu la zamani,” amesema Jux.
Kauli hiyo imekuja wakati ambapo picha na video zake za hivi karibuni zimeendelea kuibua mijadala, huku baadhi ya mashabiki wakisema amepungua kwa kiwango kinachowafanya kuwa na wasiwasi kuhusu afya yake.
Msanii huyo anaonekana kulichukulia suala hilo kama sehemu ya mwonekano anaoufurahia sasa, badala ya jambo linalompa hofu. Ripoti nyingine za hivi karibuni pia zimeripoti kuwa Jux ameeleza kupungua kwake kama uamuzi wa makusudi na kwamba anapenda mwonekano wake wa sasa.
Hata hivyo, kauli hiyo haikutosha kumaliza mjadala, badala yake, mitandao ikaongeza moto.
‘Free Jux’ yashika kasi
Baada ya mashabiki kuona mabadiliko ya mwili wa Jux, baadhi yao wakaanza kuandika ujumbe wa kumtaka mke wake, Priscilla Ojo, amwachie Jux.
Ndipo kauli “Free Jux” ilipoanza kushika kasi, huku baadhi ya mashabiki wakihusisha kupungua kwa msanii huyo na maisha yake ya ndoa.
Wengine waliingia moja kwa moja kwenye kurasa za Priscilla, wakimwambia amwachie msanii huyo, wakidai hawajafurahishwa na namna Jux anavyoonekana kwa sasa.
Kampeni hiyo imekuwa kubwa kiasi cha kuvuka mitandao ya Tanzania na kuingia pia kwenye mijadala ya Nigeria, ambako Priscilla ana umaarufu mkubwa.
Wakati mashabiki wakimwambia Priscilla “Free Jux”, mume mwenyewe alikuwa tayari amesema ameridhishwa na mwonekano wake.
Priscilla ajibu kwa staili yake
Badala ya Priscilla kuingia kwenye mabishano marefu na mashabiki waliokuwa wakimshambulia kwenye mitandao, ameamua kujibu kwa staili ambayo imeongeza utamu kwenye sakata hilo.
Mke huyo wa Jux amebadilisha jina/bio yake kwenye Instagram na kujiita “Mrs Free Jux.”
Hatua hiyo imeonekana kama jibu la moja kwa moja kwa kampeni ya mashabiki iliyokuwa ikisema #FreeJumaJux, huku Priscilla akigeuza kauli hiyo kuwa sehemu ya utambulisho wake mwenyewe.
Jux hana presha na maneno ya mashabiki
Pamoja na kelele hizo, Jux hajaonyesha dalili za kuingia kwenye mzozo na mashabiki kuhusu mwonekano wake, badala yake, msimamo wake umeendelea kuwa kwamba anaupenda mwili alionao sasa.
Kwa upande mwingine, baadhi ya watu wameendelea kuhoji kwa nini mabadiliko hayo yametokea kwa haraka, huku wengine wakisisitiza kwamba mwili wa msanii huyo ni suala lake binafsi na si lazima kila mabadiliko ya mwonekano yawe ishara ya ugonjwa.
Ndoa iliyogeuka gumzo
Jux na Priscilla wamekuwa miongoni mwa wanandoa wanaofuatiliwa zaidi katika burudani za Tanzania na Nigeria.
Uhusiano wao ulipewa uzito mkubwa baada ya uchumba wao na baadaye kufuatiwa na sherehe mbalimbali za ndoa mwaka 2025, zikiwemo sherehe za jadi zilizofanyika Lagos, Aprili 17, 2025.
Ndoa yao imeendelea kuvuta macho kwa sababu ya mchanganyiko wa umaarufu wa Jux Tanzania na familia ya Priscilla Nigeria.
Sasa, mwaka 2026, mjadala mpya umeibuka, safari hii si kuhusu harusi, mapenzi wala muziki. Ni kuhusu mwili wa Jux.