Mwandaaji Shoo ya Werrason achimba mkwara tiketi feki Dar

Shoo ya msanii Werrason iliyofanyika jana jijini Mwanza imeingia dosari baada ya mashabiki kuingia mitini, na kusababisha mwanamuzi huyo kushindwa kupanda jukwaani, huku mwandaaji wake akisema watapambana na mashabiki watakaoghushi tiketi Dar es Salaam.

Mwandaaji  huyo wa Shoo ya Werrason, Lengos VIP amesema kuwa amechukizwa na mashabiki wa Mkoa wa Mwanza kutojitokeza kwa wingi na kuapa hatarudia kupeleka wasanii mkoani humo.

Alisema kuwa alimgharamia Werrason na aliamini watapata watu ukumbini, lakini ilikuwa tofauti na matarajio yake hivyo naye kuamua kuondoka ukumbini.

"Sitarudia, nasema hivi sitarudia tena kuleta msaniii yeyote Mwanza. Nilitumia gharama kubwa takribani 30 milioni, lakini hata 2 milioni sikuiona" amesema VIP na kuongeza

 

Lengos alisema, "Nilimwambia hata yeye 'Werrason' kwamba aachane na shughuli unajua wale wasanii wakubwa wanafanya kazi kwa kuona watu wametosha ukumbini, tofauti na hapo ni bure," amesema.

Rais huyo wa Wakongo nchini, amebainisha kuwa amebaini sababu ya kutoitikia kwa mashabiki na kusababisha changamoto kwa msanii wake kufanya au kutokufanya shoo ni kutokana na kukosa matangazo.

Kuhusu utaratibu wa tiketi kwa wakazi wa Jiji la Dar es Salaam kwenye shoo la leo,VIP amesema kuwa watakagua hizo tiketi na wale watakaokuwa nazo zikiwa bora wataruhusiwa kuingia.

"Tutakagua tiketi kwa wale watakaokuwa nazo bora wataingia, lakini atakayekuja kwa kughushi tunamlaza polisi," amesema mwandaaji huyo.