Real Madrid kuwaachia Camavinga, Tchouameni
Muktasari:
- Kwa mujibu wa ripoti kutoka Hispania, miamba hiyo ya La Liga inatafuta njia ya kuongeza nguvu eneo la kiungo na inamwona Rodri, mwenye umri wa miaka 30, kuwa chaguo bora kwa mipango yao ya baadaye.
REAL Madrid ipo tayari kuwauza viungo wake wawili wa kimataifa wa Ufaransa, Eduardo Camavinga na Aurelien Tchouameni, ili kupata fedha za kufanikisha usajili wa kiungo na nahodha wa Hispania wa Manchester City, Rodri.
Kwa mujibu wa ripoti kutoka Hispania, miamba hiyo ya La Liga inatafuta njia ya kuongeza nguvu eneo la kiungo na inamwona Rodri, mwenye umri wa miaka 30, kuwa chaguo bora kwa mipango yao ya baadaye.
Ili kufanikisha mpango huo, Madrid inaweza kuwaruhusu Camavinga (23) au Tchouameni (26) kuondoka, huku wachezaji hao wawili wakitajwa kuwa miongoni mwa malengo ya Manchester United katika dirisha hili la usajili.
United imekuwa ikisaka kiungo mwenye uwezo wa kucheza nafasi ya ulinzi na kusambaza mipira, jambo linalowafanya Camavinga na Tchouaméni kuwa miongoni mwa majina yanayovutia kutua ndani ya Old Trafford.
Iwapo Real Madrid itaamua kuuza mmoja au wote wawili, Manchester United inaweza kupata nafasi nzuri ya kuwashawishi kuhamia Ligi Kuu England.
Hata hivyo, hadi sasa hakuna ofa rasmi iliyowasilishwa, huku Real Madrid ikiendelea kupima uwezekano wa kukusanya fedha zitakazowezesha kufanya usajili wa Rodri kutoka Manchester City.
Franjo Ivanovic
HULL City inakaribia kukamilisha usajili wa mshambuliaji wa Benfica, Franjo Ivanovic, baada ya mazungumzo kati ya klabu hizo kuingia hatua nzuri. Ripoti zinaeleza nyota huyo wa Croatia, 22 anatarajiwa kujiunga kwa mkopo, huku kipengele cha usajili wa kudumu kikijadiliwa. Hull inaamini Ivanovic ataongeza nguvu katika safu ya ushambuliaji.
Lewis Hall
MANCHESTER United imeingia kwenye mbio za kumsajili beki wa kushoto wa Newcastle United, Lewis Hall. Ripoti zinaeleza kuwa klabu hiyo ipo tayari kutoa pauni milioni 60 kwa ajili ya nyota huyo. Hata hivyo, Newcastle haitaki kumuachia kirahisi kutokana na umuhimu wake ndani ya kikosi cha kwanza.
Morgan Gibbs-White
MANCHESTER United inamfikiria kiungo mshambuliaji wa Nottingham Forest, Morgan Gibbs-White, kuwa mbadala wa Bruno Fernandes iwapo ataondoka Old Trafford. Nyota huyo alivutia kutokana na kiwango chake bora msimu uliopita, akifunga mabao 18 na kutoa pasi saba za mabao katika mashindano mbalimbali.
Joel Veltman
WEST Ham United imekamilisha usajili wa beki wa kimataifa wa Uholanzi, Joel Veltman, baada ya kuachana na Brighton. Nyota huyo amesaini mkataba wa mwaka mmoja wenye kipengele cha kuongeza mwingine. Tayari amefanyiwa vipimo vya afya na anatarajiwa kuanza kuitumikia West Ham katika mechi zijazo za mashindano.
Matthias Jaissle
KOCHA mpya wa Newcastle United, Matthias Jaissle, amesema ana hamasa kubwa ya kuiongoza klabu hiyo kuelekea mafanikio. Ameeleza kuwa mazungumzo yake na viongozi yalikuwa ya wazi na yenye kuaminiana, jambo lililomshawishi kukubali kazi hiyo. Jaissle sasa anaanza maandalizi ya msimu mpya akiwa na matarajio makubwa.
Jeremy Monga
KIPAJI cha England, Jeremy Monga (17), amesema alikataa kujiunga na Arsenal na kuchagua Manchester City kwa sababu anaamini atapata nafasi nzuri ya kuendelea kukua. Mshambuliaji huyo wa zamani wa Leicester City alikiri Arsenal ilikuwa karibu kumsajili, lakini alibadili uamuzi wake kabla ya kukamilisha dili.
Ezri Konsa
ARSENAL inaendelea na harakati za kumsajili beki wa Aston Villa na England, Ezri Konsa (28). The Gunners wanajiandaa kuwasilisha ofa mpya baada ya mazungumzo ya awali kutofanikiwa. Hata hivyo, Aston Villa imeanza mazungumzo ya kumpa nyota huyo mkataba mpya ili kumbakisha Villa Park kwa muda mrefu zaidi.
Darwin Nunez
Trabzonspor ya Uturuki inamuwania mshambuliaji wa Uruguay, Darwin Nunez, ili aungane tena na Mohamed Salah. Nyota huyo wa Al-Hilal mwenye miaka 27 anatajwa kuwa lengo kuu la klabu hiyo baada ya usajili wa Salah. Trabzonspor inaamini wawili hao wataimarisha safu yao ya ushambuliaji msimu ujao.
Ibrahim Mbaye
LIVERPOOL imeanza kufanya uchunguzi wa kina kuhusu uwezekano wa kumsajili winga chipukizi wa Paris Saint-Germain (PSG), Ibrahim Mbaye, mwenye umri wa miaka 18. Mabingwa hao wa England wanaendelea na mpango wa kuimarisha kikosi chao kwa kuwekeza kwa wachezaji vijana wenye vipaji vikubwa.