Rais wa LaLiga amtaka Infantino ajiuzulu
Muktasari:
- Tebas, ambaye alikuwa Marekani kushuhudia Hispania ikitwaa Kombe la Dunia 2026, amesema viongozi wengi wa soka wanapinga uamuzi ya Infantino, lakini hawathubutu kuyasema hadharani.
MADRID, HISPANIA: RAIS wa LaLiga, Javier Tebas, amemtaka rais wa FIFA, Gianni Infantino, kujiuzulu, akidai uongozi wake unaharibu tasnia ya soka kwa uamuzi yanayoweka maslahi ya mashindano ya Kombe la Dunia mbele ya maendeleo ya mchezo huo.
Akizungumza na gazeti la Italia la La Gazzetta dello Sport, Tebas amesema anaamini muda wa Infantino kuiongoza FIFA umefika mwisho.
"Kwa maoni yangu, ndiyo. Nafikiri muda wake umeisha," amesema Tebas.
Hata hivyo, alikiri kuwa Infantino bado anaungwa mkono na mashirikisho mengi ya soka duniani, huku akiitaja mfumo wa uchaguzi wa FIFA kuwa na dosari kubwa.
"Hakuna anayethubutu kugombea kwa sababu kila mtu anaamini atashindwa. Hapaswi kuendelea kubaki madarakani, lakini mazingira yaliyopo yanaifanya iwe vigumu kuondoka."
Aikosoa FIFA kwa uamuzi wa Kombe la Dunia
Tebas, ambaye alikuwa Marekani kushuhudia Hispania ikitwaa Kombe la Dunia 2026, amesema viongozi wengi wa soka wanapinga uamuzi ya Infantino, lakini hawathubutu kuyasema hadharani.
"Nimekutana na watu wengi wanaopinga anachofanya Infantino, lakini wanabaki kimya. Wanafahamu madhara yanayosababishwa kwa soka, lakini hawachukui hatua."
Sakata la Balogun
Moja ya hoja alizozitolea mfano ni uamuzi wa FIFA kusitisha adhabu ya mshambuliaji wa Marekani, Folarin Balogun, kabla ya mchezo wa hatua ya 16 bora dhidi ya Ubelgiji.
Tebas amesema tukio hilo lilikuwa zito na lingeweza kumgharimu Infantino nafasi yake kama Marekani isingeondolewa na Ubelgiji.
"Walikuwa na bahati Marekani ilitolewa. Kama wangeendelea mashindanoni, suala hilo lingeweza kumgharimu Infantino urais wake. Kilichotokea ni sehemu ndogo tu ya matatizo yaliyopo."
UEFA pia ilikosoa uamuzi huo, ikiuita wa "kushangaza, usioeleweka na usio na msingi."
Apinga Kombe la Dunia la timu 64
Tebas pia alipinga wazo la FIFA la kuongeza idadi ya timu zinazoshiriki Kombe la Dunia hadi 64.
Kwa mujibu wake, soka haliwezi kuzunguka Kombe la Dunia pekee huku ligi za ndani zikipuuzwa.
"Kuongeza idadi ya timu hakina mantiki. Sekta ya soka si Kombe la Dunia pekee."
Ameongeza:"Ligi za ndani ndizo zinazolisha na kuendesha soka kila siku. Zinatoa maelfu ya ajira, lakini zinawekwa pembeni kwa ajili ya mashindano yanayodumu siku 40 pekee."
Kwa mtazamo wake, suluhisho ni kupunguza mechi za kimataifa na kulinda zaidi mashindano ya ndani.
Asema mapumziko ya maji ni kisingizio
Rais huyo wa LaLiga pia alikosoa uamuzi wa FIFA kuweka mapumziko ya lazima ya kunywa maji katika kila mechi ya Kombe la Dunia, akidai hayakuwa kwa ajili ya ustawi wa wachezaji bali kuongeza muda wa matangazo ya biashara.
"Mapumziko hayo ni uongo. LaLiga tunayatumia pale tu kunapokuwa na joto kali."
Amesema katika viwanja kama vile Dallas, Los Angeles na Atlanta kulikuwa na mifumo ya kupooza hewa kiasi kwamba hata mashabiki walihitaji kuvaa makoti.
"Ilikuwa mapumziko ya matangazo, si ya maji."
Ashambulia pia burudani ya mapumziko
Tebas hakufurahishwa pia na burudani ya mapumziko ya fainali ya Kombe la Dunia iliyowashirikisha wasanii wakubwa akiwemo Shakira, Madonna, BTS na Justin Bieber, iliyofanya mapumziko ya kawaida ya dakika 15 kuongezeka hadi zaidi ya dakika 27.
"FIFA hufanya inachotaka kwa maslahi yake yenyewe, si kwa maslahi ya soka. Kama wanataka mapumziko ya dakika 27 kwa ajili ya burudani au matangazo, wanafanya hivyo bila kujali athari zake."
Kwa kauli hizo, Tebas ameongeza presha kwa uongozi wa FIFA, huku akiitaka dunia ya soka kutetea maslahi ya ligi za ndani badala ya kuruhusu maamuzi yanayolenga kuikuza Kombe la Dunia pekee.