Mtoto aingia uwanjani, mechi yasimamishwa
Muktasari:
- Tukio hilo lilitokea zikiwa zimesalia takribani sekunde 90 kabla ya mchezo kumalizika, wakati mwamuzi aliposimamisha mchezo baada ya kupewa taarifa kupitia kifaa chake cha mawasiliano kwamba kuna mvamizi asiye wa kawaida ameingia uwanjani.
SAN JOSE, MAREKANI: MECHI kati ya San Jose Earthquakes na Minnesota United ilisimama kwa muda katika dakika za nyongeza baada ya mtoto mdogo kuingia uwanjani na kusababisha tukio la kushangaza.
Tukio hilo lilitokea zikiwa zimesalia takribani sekunde 90 kabla ya mchezo kumalizika, wakati mwamuzi aliposimamisha mchezo baada ya kupewa taarifa kupitia kifaa chake cha mawasiliano kwamba kuna mvamizi asiye wa kawaida ameingia uwanjani.
Mtoto huyo alionekana akitembea ndani ya uwanja huku akitabasamu, kabla ya mmoja wa walinzi kumchukua na kumrudisha haraka kwenye jukwaa.
Msichana mdogo, ambaye inaaminika huenda alikuwa dada yake, alikimbia kuelekea uwanjani na kujaribu kumchukua mtoto huyo kumrudisha sehemu salama.
Baadaye, mwanamke mmoja, anayedhaniwa kuwa mama wa mtoto huyo, alifika na kuchukua jukumu la kumrudisha mtoto huku akionekana kushangazwa na kilichotokea.
Kwa wakati huo, Minnesota United ilikuwa tayari ikiongoza kwa mabao 5-1, hivyo tukio hilo likawa kama burudani ya mwisho kabla ya mchezo kumalizika.
“BORA KULIKO RACCOON”
Tukio hilo liliwakumbusha mashabiki tukio lingine lililotokea Mei 2024 katika uwanja huo huo, ambapo mchezo ulisimamishwa baada ya raccoon kuingia uwanjani na kusababisha tafrani.
Mnyama huyo aliyepewa jina la utani “Raquinho” aliwahi kuvamia uwanja wa PayPal Park wenye uwezo wa kuchukua mashabiki 18,000.
Mmoja wa wachambuzi wa mchezo huo alicheka na kusema: “Huyu ni bora zaidi kuliko raccoon.”
Kisha akauliza kwa mshangao: “Wamewezaje kufika mpaka kule? Walikuwa pembeni ya eneo la mita 18.”
Baada ya mchezo, akaunti rasmi ya Minnesota United kwenye mtandao wa X ilitania tukio hilo kwa kuandika: “Ni kama kuchukua pesa kwa mtoto.”
Klabu hiyo pia iliongeza ujumbe mfupi uliosomeka: “Mtoto > raccoon.”
Kocha wa Minnesota United, Cameron Knowles, alipoulizwa kuhusu tukio hilo, alicheka kabla ya kusema:
“Uliweza kusikia kelele, kisha unaanza kuangalia ni kitu gani. Nilifikiri, jamani, ni mapema sana kupata marufuku ya maisha kutoingia uwanjani.”