Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Arsenal yaanza kutetea taji kwa kishindo ikiichapa Coventry 3-0 Emirates

Muktasari:

  • Hii ilikuwa Arsenal yenye ukali wa kutisha na yenye ufanisi katika kila eneo lililohitajika. Kama Micky Quinn wa mwaka 1993 angeitwa na Coventry City kuja kusaidia, kuna uwezekano mkubwa angeishia kuangushwa chini pamoja na wachezaji wengine wa Frank Lampard.

Jana ilikuwa ni siku ya ufunguzi wa msimu, bado kuna mechi ngumu zaidi mbele ya Arsenal, lakini kila kilichoonekana katika mchezo huu kinaashiria kuwa kuridhika kupita kiasi hakutakuwa miongoni mwa mapungufu yao katika harakati za kutetea taji lao.

Hii ilikuwa Arsenal yenye ukali wa kutisha na yenye ufanisi katika kila eneo lililohitajika. Kama Micky Quinn wa mwaka 1993 angeitwa na Coventry City kuja kusaidia, kuna uwezekano mkubwa angeishia kuangushwa chini pamoja na wachezaji wengine wa Frank Lampard.

Kwa kawaida, bado hakuna haja ya kufanya hitimisho la haraka kuhusu maana halisi ya matokeo haya, isipokuwa kusema kwamba kikosi cha Mikel Arteta kilianza kampeni hii ya Premier League kwa kutimiza malengo yake mawili makuu ushindi na kutowacha mianya ambayo wapinzani wanaoweza kuitumia kujipa matumaini.

Kwa mtazamo mpana, ushindi huo ulipatikana kupitia mabao ya Kai Havertz, Bukayo Saka na Martin Odegaard, lakini maelezo ya ndani ya mchezo ndiyo muhimu zaidi. Na miongoni mwa mambo hayo ni Christos Tzolis.

Kuna mashabiki wa Norwich ambao huenda miaka yote hiyo walimuona winga wao huyo Mgiriki kama mchezaji wa kawaida tu; lakini labda “farasi wa Trojan” ndilo jina lililomfaa zaidi. Akicheza mechi yake ya kwanza katika ligi hii tangu mwaka 2022, mchezaji huyo mpya wa Arsenal aliyesajiliwa kutoka Brugge kwa ada ya pauni 33 milioni aling’ara katika mchezo huu.

Ni kweli kwamba nguvu zake zilipungua kipindi cha pili, lakini kufikia wakati huo alikuwa tayari ameiangusha safu ya ulinzi ya Coventry kwa mashambulizi mfululizo kutoka upande wa kushoto.

Umuhimu wa jambo hilo uko wazi. Endapo ataendelea kucheza kwa kiwango hicho, Arsenal itakuwa tatizo kubwa katika pande zote mbili za uwanja. Hilo litamfurahisha sana Arteta, kama ambavyo pia atafurahishwa na viwango vya Saka na Martin Odegaard.

Mmoja alikuwa tishio lisilokoma, mwingine alikuwa DJ wa muziki wa Arsenal, na kwa pamoja waliwatesa kwa namna tofauti wachezaji wa Coventry waliokuwa wakubwa kimwili. Kwa kifupi, waliwazungusha huku na kule.

Mtazamo wa jambo hili ni rahisi – alikuwa Coventry. Na mchezo ulikuwa kwenye uwanja wa Arsenal. Lakini pia ilikuwa ni sherehe iliyoendelea, huku haikuvurugwa hata na taarifa za mapema siku hiyo kwamba Bruno Guimaraes anaweza kukaa nje kwa wiki kadhaa kutokana na majeraha madogo.

Kabla ya mchezo kuanza, fataki zililipuka angani, bendi ya shaba ikipiga muziki mitaani na mabango yakining’inia kwenye kila ukuta kuwakumbusha wageni kwamba mabingwa wanaishi Emirates Stadium.

Yote hayo huenda Coventry wangeyavumilia kama si kipigo cha upande mmoja kilichofuata.

Kwa Lampard, huu ulikuwa mwanzo mgumu wa kurejea kwenye jukwaa kubwa. Angalau hawezi kulaumiwa kwa kuwapuuza wachezaji waliowezesha timu hiyo kupanda daraja. Au si mara moja, angalau.

Kati ya wachezaji 11 aliowachagua kwa mchezo wake wa kwanza wa ligi kuu baada ya robo karne, wanane walikuwa sehemu ya kikosi kilichopigania kupanda daraja, huku Caleb Yirenkyi, Loum Tchaouna na Aurele Amenda wakiwa sehemu ya usajili wa pauni milioni 130 alioufanya Coventry.

Hilo lilikuwa jambo moja lililobaki kuwa na mwendelezo kwa Coventry. Jambo jingine lilikuwa nguvu zao za mwili – vijana wakubwa waliwasaidia kupanda daraja na vijana wakubwa hao hao ndio wanaotarajiwa kuwasaidia kubaki ligi kuu.

Wachezaji wasiopungua saba wa kikosi cha Lampard katika mchezo huu walikuwa na urefu wa zaidi ya futi sita. Na tusisahau kwamba msimu uliopita Lampard alisimamia timu iliyofunga mabao mengi zaidi kupitia mipira iliyokufa kuliko Arsenal ya Arteta.

Kwa sababu hiyo, kulikuwa na hali ya mshangao kwa muda mfupi wakati Coventry walipopata kona ndani ya sekunde 30 za kwanza. Kwamba mpira huo haukuweza kumpita Riccardo Calafiori kwenye nguzo ya karibu ulikuwa tayari ni ishara mbaya.

Kuanzia hapo, Coventry walikabiliwa na kile ambacho kingeweza kuitwa kifo cha taratibu kupitia pasi fupi elfu moja.

Arsenal walikuwa wepesi, wenye tamaa ya kushambulia na wasioweza kutabirika, huku kupitia Tzolis na Saka wakitawala pande zote mbili za uwanja.

Mechi ngumu zaidi zinahitajika kabla ya kutoa hukumu kamili kuhusu Tzolis, lakini namna alivyomrarua beki wa kulia wa Coventry, Milan van Ewijk, ni ishara nzuri kwa wale waliohisi kwamba matoleo ya awali ya timu za Arteta yalikuwa yakitegemea zaidi upande mmoja.

Kwa kweli, Tzolis ndiye aliyepata nafasi ya kwanza ya Arsenal, lakini shuti lake lilipaa juu ya lango baada ya shambulizi la kushtukiza lililoanzishwa kwa kasi na Saka pamoja na Odegaard.

Kisha akahusika katika nafasi ya pili, iliyotokana na mpango mpya wa kona fupi uliopendelea mpira wa chini badala ya kupeleka mpira hewani. Saka, Ben White na Myles Lewis-Skelly walifuata mpira huo kwa ustadi kabla ya shuti la Tzolis kuzuiwa mwishoni mwa shambulizi hilo.

Katika hatua hii, kuna jambo moja la kuongeza Odegaard, ambaye kwa kiasi kikubwa alikuwa akicheza namba 10, ambako tunatarajia pia kumwona akicheza mara tu Guimaraes atakapokuwa fiti, alikuwa ndiye mchezaji wa timu kama alivyofanya kwenye Community Shield.

Akiwa na Declan Rice na Lewis-Skelly nyuma yake katika mfumo wa 4-2-3-1, safu hiyo iliwazungusha wachezaji wakubwa wa Coventry katikati ya uwanja.

Kama kulikuwa na jambo la kushangaza, ni kwamba udhibiti huo mkubwa wa mchezo ulizaa mabao mawili tu katika kipindi cha kwanza.

Bao la kwanza, lililofungwa na Havertz baada ya dakika 15, lilianza pale Tzolis alipomshinda Van Ewijk katika pambano la mpira wa juu, kabla Calafiori kutoa pasi ya haraka na ya chini iliyomfikia Mjerumani huyo.

Umaliziaji wa Havertz ulionyesha wazi kwamba huenda ameanza kupata faida katika ushindani wake mdogo na Viktor Gyokeres kuhusu nafasi ya kuongoza safu ya ushambuliaji.

Bao la pili lilikuja dakika ya 23, wakati Rice na Odegaard walipoongoza shambulizi, huku Carl Rushworth akigeuza krosi ya Tzolis na mpira kuangukia miguuni mwa Saka.

Saka hakufanya makosa. Aliupiga moja kwa moja wavuni.

Lampard hakufanya mabadiliko wakati wa mapumziko, na wala hakukuwa na mabadiliko yoyote katika mwenendo wa mchezo.

Arsenal waliendelea kuwasakama, huku Coventry wakiendelea kupambana na hewa nyembamba, na ndani ya dakika chache tofauti ya mabao mawili ikawa matatu.

Tena, shambulizi hilo liliendeshwa kwa kasi, safari hii Rice na Saka wakipanga njia za kupita kabla Ben White kupanda kwa kasi upande wake na Odegaard kufunga kwa shuti lisilo la kuvutia zaidi lililompita Rushworth.