Simba yaleta kocha mpya, Mreno ayeyuka

SIMBA hatanii. Kwani baada ya kumpeleka jijini Mwanza, aliyekuwa kocha msaidizi wa timu hiyo waliye mbioni kumpandisha daraja kuwa Mkurugenzi wa Ufundi, Seleman Matola, mabosi wa klabu hiyo wapo hatua ya mwisho kumshusha kocha mkuu mpya atakayeisimamia timu kwenye Kombe la Mapinduzi 2023.
Awali, Simba ilikuwa ikimpigia hesabu kocha wa Kireno aliyekuwa akiinoa klabu ya Petro de Luanda ya Angola, Alexandre Santos, lakini dili hilo limekufa rasmi kwa kilichoelezwa kuna mambo yalikwama wakati wakidili naye chini ya Mtendaji Mkuu anayeondoka, Barbara Gonzalez.
Kutokana na dili hilo kukwama, Simba ilishaanza kumfuatilia kocha wa Vipers ya Uganda, Roberto Oliveira aliyewahi kutajwa kutakiwa na Yanga wakati vuguvugu la kutaka kumpiga chini kocha Nasreddine Nabi mara baada ya kung’olewa na Al Hilal ya Sudan katika Ligi ya Mabingwa Afrika.
Tayari mabosi wa Simba walishawasiliana na kocha huyo wa Vipers, lakini mambo hayakwenda vizuri na sasa imekamilisha dili la kumleta kocha mpya kutoka barani Afrika ambaye atakuja kabla ya safari ya kwenda Zanzibar kwenye michuano ya Kombe la Mapinduzi 2023.
Simba itaondoka jijini Dar es Salaam baada ya mchezo wao wa Ijumaa ijayo dhidi ya Tanzania Prisons utakaopigwa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa na kupumzika kwa siku moja kabla ya Mwaka Mpya, yaani Januari Mosi na itashuka uwanjani Januari 3 kuvaana na Mlandege.
Mmoja wa vigogo wa Simba, aliliambia Mwanaspoti jana kuwa, kabla ya kikosi chao kupanda boti kwenda Zanzibar kwa ajili ya michuano hiyo ya Mapinduzi tayari kocha huyo atakuwa ameshatua ili kuungana na Juma Mgunda aliyekaimu nafasi hiyo tangu Zoran Maki atimkie Misri.
Kigogo huyo wa juu aliyekataa kutajwa, aliwathibitishia Mwanaspoti kwamba wakati mashabiki wa timu hiyo wakiwa kwenye maandalizi ya kusherehekea Sikukuu ya Krismasi na Mwaka Mpya mabosi wa timu hiyo watakuwa wamekamilisha mchakato wa kumpata kocha mpya.
“Kuna kocha mmoja raia wa Afrika amefundisha timu mbalimbali ngazi ya klabu Ulaya na Afrika na timu za taifa, tupo hatua ya mwisho kumalizana naye na atakuja kuungana na timu kabla ya Mapinduzi inayoanza Januari Mosi,” alisema kigogo huyo na kuongeza;
“Kwa sasa ni ngumu kumtaja jina lake na timu anayotokea kwa sasa kwani yupo kwenye mkataba, tunataka kumalizana naye kila kitu na baada ya hapo itakuwa sahihi kumuweka wazi, ila mchakato huu unakamilika kabla ya wiki ijayo kwani tupo kwenye hatua nzuri.”
Japo kigogo huyo ameficha jina la kocha huyo wanayemalizana naye, lakini taarifa kutoka ndani ya Simba zinasema, huenda akawa ni Lamine N’Diaye wa Senegal ambaye walimtamani kabla hata ya kumleta Zoran aliyepo Al Ittihad ya Misri. N’Diaye kwa sasa ni kocha wa AC Horoya ya Guniea amewahi kuzinoa Maghreb Fez ya Morocco, TP Mazembe na Al Hilal na kwa timu ya taifa ameshawahi kuinoa timu ya taifa ya Senegal.
Kuhusu dili za makocha wa awali ambao walitajwa na Mwanaspoti kuhakikishwa wanakuja, alifafanua; “Unajua huu mchakato wa kuleta kocha mpya ungekuwa umekamilika muda mrefu, kwani tulimpata kocha mmoja kutoka Afrika ya Kaskazini jina lake nimelisahau ila kipindi tunataka kumchukua alikuwa amepata dili lingine jipya na akaenda huko.”
Alipotafutwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Simba, Salim Abdallah ‘Try Again’ juu ya ishu hizo za kocha na usajili, alisema muda ukifika kila kitu kitawekwa wazi.