Ridhiwani achukua mikoba ya Mwigulu Yanga
Muktasari:
- Uteuzi huo wa Ridhiwani unamfanya kuungana na wajumbe wengine wa baraza hilo ambalo ni Mama Fatma Karume, Antony Mavunde na Tarimba Abbas, huku mwenyekiti wao akiwa mwenyekiti wa baraza hilo, George Mkuchika.
Yanga imefanya mabadiliko ya bodi yake ya wadhamini, ikiridhia kumuweka kando Waziri Mkuu, Dk Mwigulu Nchemba katika eneo la ujumbe, nafasi yake ikichukuliwa na Ridhiwani Kikwete.
Akitangaza kwenye mkutano Mkuu wa Yanga unaofanyika leo Agosti 2, 2026 kwenye Ukumbi wa The Super Dome uliopo Masaki jijini Dar es Salaam, rais wa klabu hiyo, Injinia Hersi Said amesema baada ya Dk Mwigulu kuteuliwa na Rais wa Tanzania, Dk Samia Suluhu kuwa Waziri Mkuu, ameomba kwa ridhaa yake kuwa nje ya baraza hilo.
Hersi amesema baada ya maombi hayo ya Dk Mwigulu, kamati ya utendaji ilikutana na kutafuta mrithi wake na kumchagua Ridhiwani Kikwete kuwa Mjumbe mpya wa baraza hilo.
"Kwa mujibu wa katiba yetu, tukimaliza kufanya uteuzi tunatakiwa kuleta jina hilo kwenu ili mtoe baraka za uteuzi huo na nitawahoji kama mmeridhia," amesema Hersi.
Baada ya kuwahoji wanachama hao, wakabariki uteuzi huo na rasmi Ridhiwani Kikwete ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, sasa ni mjumbe wa baraza hilo.
Uteuzi huo wa Ridhiwani unamfanya kuungana na wajumbe wengine wa baraza hilo ambalo ni Mama Fatma Karume, Antony Mavunde na Tarimba Abbas, huku mwenyekiti wao akiwa mwenyekiti wa baraza hilo, George Mkuchika.