Nyota Pamba Jiji atuliza presha
Muktasari:
- Kibailo ambaye amekuwa na kiwango bora, hakusita kufichua kinachombeba akieleza kuwa kujituma na kufuata maelekezo ya benchi la ufundi ndio siri ya mafanikio yake akibainisha kuwa mpira ndio kazi yake.
PAMOJA na kukiri ugumu wa ligi, nyota wa Pamba Jiji, Hassan Kibailo amesema upepo mbaya walioanza nao ni sehemu ya matokeo ya mechi, akiahidi mapumziko waliyonayo watarejea wakiwa imara.
Hata hivyo, amesisitiza kuwa hakuna tatizo lolote ndani au nje ya uwanja linalowafanya kutokuwa na matokeo mazuri, akiwatoa hofu mashabiki wasikate tamaa badala yake waendelee kuwasapoti.
“Hatuna tatizo lolote linalotuchanganya kwa matokeo haya, huu ni upepo mbaya umetuangukia na tunajua muda mwingine mpira unagoma, lakini hatujakata tamaa na tunaomba mashabiki waendelee kutusapoti.
“Kwa muda huu wa mapumziko tutajitathimini na kufanya masahihisho sehemu yenye tatizo na kufuata maelekezo ya benchi la ufundi kuhakikisha tunaporejea uwanjani tunafanya vizuri,” amesema Kibailo.
Pamba Jiji haijawa na mwanzo mzuri baada ya kucheza mechi sita ikiambulia pointi moja, huku ikiwa imeruhusu mabao 13 na kufunga manne ikishika nafasi ya mwisho kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara.
Kibailo ambaye amekuwa na kiwango bora, hakusita kufichua kinachombeba akieleza kuwa kujituma na kufuata maelekezo ya benchi la ufundi ndio siri ya mafanikio yake akibainisha kuwa mpira ndio kazi yake.