Ninju apelekwa kwa mkopo
Muktasari:
- Yanga imefanya umauzi huo ikiwa ni sehemu ya mpango wa kumsaidia kinda huyo kuweza kucheza mara kwa mara kwani kwenye eneo lake kuna ushindani wa namba.
BEKI kinda wa Yanga, Abubakar Nizar ‘Ninju’, ametolewa kwa mkopo wa msimu mmoja kwenda Polisi Tanzania kwa ajili ya kupata nafasi zaidi ya kucheza na kuendelea kujenga uwezo wake.
Yanga imefanya umauzi huo ikiwa ni sehemu ya mpango wa kumsaidia kinda huyo kuweza kucheza mara kwa mara kwani kwenye eneo lake kuna ushindani wa namba.
Eneo analocheza Ninju kuna mabeki wenye uzoefu akiwemo Ibrahim Bacca, Bakari Mwamnyeto na Dickson Job, ambaye kwa sasa bado hajarejea uwanjani. Pia Yanga ina Farouk Komara, aliyesajiliwa msimu huu, lakini bado hajapata nafasi ya kucheza katika kikosi hicho.
Kutokana na hali hiyo, Yanga imeona kumpeleka Ninju kwa mkopo kuwa ni njia nzuri ya kumpa nafasi ya kuonyesha uwezo wake katika mazingira ambayo anaweza kupata muda wa kutosha wa kucheza.
Uongozi wa Yanga unaamini kuwa kupata nafasi ya kucheza mara kwa mara kutamsaidia Ninju kuongeza kujiamini, kujenga uzoefu na kukuza zaidi kipaji chake kabla ya kurejea katika kikosi cha Yanga akiwa na ushindani mkubwa zaidi.
“Kule atazidi kuimarika na kujiamini zaidi tunaamini kwenye uwezo lakini kukaa benchi mara kwa mara sio afya nzuri kwa kijana ambaye alikuwa na muendelezo mzuri kabla haiajiunga na Yanga,” alisema mmoja wa viongozi wa timu hiyo.
Kabla ya kujiunga na Yanga, Ninju alikuwa JKU ya Zanzibar kwa mkopo akitokea Azam FC ambako alikuwa na kiwango bora.