Mchora katuni Mwananchi King Kinya afariki dunia
Muktasari:
- Kinya alihudumu kama mchora katuni katika magazeti yanayochapishwa na Kampuni ya MCL
MFANYAKAZI wa Idara ya Habari ya kampuni ya Mwananchi Communications (MCL), Kinyagulo Tuzo maarufu kama King Kinya, amefariki dunia leo, Septemba 17, 2026 baada ya kuugua kwa kipindi kifupi.
Taarifa iliyotolewa Ofisi ya Rasilimali watu MCL imethibitisha kutokea kifo cha King Kinya aliyehudumu kwa miaka 17 kama mchora katuni wa magazeti yanayochapishwa na kampuni hiyo.
Akizungumza na Mwananchi kaka wa marehemu, Kiondo Tuzo Mjema, amesema King Kinya alianza kuugua akiwa nyumbani Tabata mwanzoni mwa Julai 2026, hali iliyomfanya kukaa ndani kwa muda kabla ya kupelekwa Morogoro.
Amesema akiwa Morogoro hali yake ilizidi kuwa mbaya na baadaye alipelekwa hospitalini, ambako alilazwa kwa takribani wiki moja kabla ya kuruhusiwa kurejea nyumbani.
“Alipotoka hospitali aliambiwa arudi tena kwa ajili ya ufuatiliaji. Juzi alirudi hospitalini baada ya kusumbuliwa na tumbo, kuharisha na kutapika, akapewa dawa na kuruhusiwa kurudi nyumbani,” amesema.
Kwa mujibu wa Kiondo, hali ya marehemu ilizidi kuwa mbaya usiku wa kuamkia jana Septemba 15, 2026, akilalamikia maumivu makali ya tumbo na kichwa pamoja na kutapika na kuharisha.
Kiondo amesema msiba upo Kimara Kona na mazishi yanatarajiwa kufanyika kesho saa 10 jioni katika makaburi ya Mwananyamala.