Matola aihofia Prisons, Kibu nje
KOCHA msaidizi wa Simba Seleman Matola amesema timu yoyote itakayotumia vyema dakika 90 katika mchezo wa kesho ndiyo itapata pointi tatu.
Simba kesho ni mwenyeji wa Tanzania Prisons mchezo wa raundi ya 14 wa Ligi Kuu Tanzania Bara utakaopigwa katika uwanja wa Benjamin Mkapa Dar es Salaam.
Matola amesema kila timu imejipanga na kutokana na ushindani uliopo yoyote atakayezitumia vyema dakika hizo ndiye atapata pointi katika mchezo huo.
Aidha Matola amesema haijalishi wapinzani wao kuburuza mkia katika msimamo wa Ligi kutawafanya wabweteke bali watahakikisha wanapambana dakika zote.
"Tanzania Prisons ni miongoni mwa timu nzuri japokuwa wanashika mkia katika msimamo ila ni mchezo ambao tunatakiwa kupambana mwanzo mwisho kupata matokeo, "
Matola amesema katika mchezo wa kesho atakosekana mshambuliaji wao Kibu Denis ambaye ana majeruhi mpaka sasa bado hajarejea uwanjani isipokuwa Jonas Mkude yeye ameanza mazoezi jana.
Simba inashika nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi ikiwa na pointi 25 ikishinda mechi saba sare nne na kupoteza michezo miwili huku Prisons pointi 11 kashinda tatu sare mbili na kupoteza michezo nane.