Matokeo mabaya yamuondoa kocha Mwenge
Muktasari:
- Kutokana na matokeo hayo, taarifa za ndani ya timu hiyo zinaeleza kuwa, uongozi umefikia makubaliano ya kuachana na kocha wa kikosi hicho, Msellem Sultan Hemed.
TIMU ya Mwenge iliyorejea Ligi Kuu Zanzibar msimu huu 2026-2027, imekuwa na hali ngumu kwenye ligi hiyo baada kupoteza mechi nne mfululizo ilizocheza.
Kutokana na matokeo hayo, taarifa za ndani ya timu hiyo zinaeleza kuwa, uongozi umefikia makubaliano ya kuachana na kocha wa kikosi hicho, Msellem Sultan Hemed.
Katika mechi nne ilizocheza timu hiyo, matokeo yalikuwa hivi; Mwenge 0-2 Muembe Makumbi, Mwenge 1-2 Raskazone, Uhamiaji 2-0 Mwenge na Black Sailors 2-1 Mwenge.
Inaelezwa kuwa, matokeo hayo hayajawaridhisha viongozi wa timu hiyo ndio sababu kubwa ya kuamua kuachana naye na kutafuta mwingine wa kuinoa Mwenge.
Akizungumza na Mwanaspoti, Mtendaji Mkuu wa Mwenge, Ali Said, amesema hawezi kulizungumzia suala hilo kwasasa kwani hawajakaa vikao kulitolea ufafanuzi. Amesema, katika kipindi hiki kuna vitu wanavishughulikia kwa lengo la kuiweka sawa timu, hivyo watatoa taarifa rasmi baada ya kukubaliana.
“Hatujaamua kutoa taarifa yoyote kwa sababu hatujakubaliana, kikao kitakachofanyika ndio kitatoa uamuzi, kwasasa kuna vitu ambavyo tunavishughulikia,” amesema.
Hiyo ni timu ya pili kutokea kisiwani Pemba kufikia makubaliano ya kuachana na kocha wake katika Ligi Kuu Zanzibar baada ya aliyekuwa Kocha Mkuu wa Wembe, Juma Pweka kuondolewa mapema baada ya kupokea kipigo cha bao 1-0 mechi ya kwanza dhidi ya Uhamiaji. Mwenge inaendelea kusalia mkiani mwa msimo wa ligi hiyo kwa kushindwa kukusanya pointi hata moja katika michezo minne iliyocheza.