Kiungo Fountain ajiunga Simba
Muktasari:
- Siyame bado ana mkataba wa miaka mitatu na Fountain Gate Princess, lakini taarifa ambazo Mwanaspoti imezipata ni kwamba Simba inataka kumsajili kiungo huyo kwa muda maalumu ili aweze kuitumikia timu hiyo katika mashindano ya kimataifa kabla ya kurejea kwenye kikosi chake.
KIUNGO mshambuliaji wa Fountain Gate Princess, Mary Siyame amejiunga na Simba Queens kwa mkopo wa miezi minne ili kuongeza nguvu kwenye safu ya ushambuliaji kuelekea kwenye michuano ya CECAFA kufuzu Ligi ya Mabingwa Afrika.
Siyame bado ana mkataba wa miaka mitatu na Fountain Gate Princess, lakini taarifa ambazo Mwanaspoti imezipata ni kwamba Simba inataka kumsajili kiungo huyo kwa muda maalumu ili aweze kuitumikia timu hiyo katika mashindano ya kimataifa kabla ya kurejea kwenye kikosi chake.
Mratibu wa Simba, Selemani Makanya, pamoja na kocha mkuu Mussa Hassan ‘Mgosi’ wanadaiwa kuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha wanapata saini ya Siyame, ambaye amekuwa na kiwango bora akiwa na uwezo wa kucheza nafasi zote za ushambuliaji.
“Simba inamtaka Siyame kwa sababu wanahitaji kuongeza nguvu kwenye kikosi kitakachoshiriki Ligi ya Mabingwa Afrika, lakini kinachoweka ugumu ni kwamba Fountain Gate inataka fedha nyingi kama mchezaji huyo ataondoka moja kwa moja,” kilisema chanzo chetu.
Kwa mujibu wa chanzo hicho, Siyame mwenyewe anatamani kuvaa jezi ya Simba kwa sababu anataka kupata nafasi ya kucheza Ligi ya Mabingwa Afrika, jambo ambalo limekuwa sehemu kubwa ya mazungumzo yanayoendelea kati ya pande hizo mbili.
“Yeye anatamani kucheza Simba ili apate nafasi ya kushiriki Ligi ya Mabingwa Afrika. Ndiyo maana wamefikia mpango wa kumtoa kwa mkopo badala ya kuvunja mkataba wake,” kiliongeza chanzo hicho.
Kutokana na hali hiyo, Fountain Gate Princess imekubali kumruhusu Siyame kwenda kwa mkopo wa miezi minne mpaka michuano ya kimataifa itakapotamatika na baada ya hapo kiungo huyo atarejea kwenye kikosi cha Fountain Gate Princess kuendelea na mkataba wake.