Job, Mzize warudishwa Sauzi
Muktasari:
- Wachezaji hao wamekuwa nje kwa muda mrefu wakipitia matibabu na programu maalum za kurejea baada ya kusumbuliwa na majeraha ya goti yaliyowafanya kukosa sehemu kubwa ya msimu uliopita.
YANGA imeamua kwenda kwa tahadhari kubwa katika kuhakikisha nyota wake wawili, Dickson Job na Clement Mzize, hawarudi uwanjani kabla ya kuwa tayari kwa asilimia zinazohitajika, huku mipango ya kuwapeleka Afrika Kusini kwa vipimo maalum ikiwa sehemu ya hatua za mwisho za kuwarejesha kazini.
Wachezaji hao wamekuwa nje kwa muda mrefu wakipitia matibabu na programu maalum za kurejea baada ya kusumbuliwa na majeraha ya goti yaliyowafanya kukosa sehemu kubwa ya msimu uliopita.
Taarifa kutoka upande wa tiba wa Yanga zilisema kuwa: “Job na Mzize wanatarajiwa kufanyiwa vipimo vya mwisho Afrika Kusini ili madaktari kujiridhisha kwamba majeraha yao yamepona vizuri na kwamba miili yao iko tayari kubeba mzigo wa mechi za ushindani.”
“Benchi la ufundi halitaki kuharakisha kuwarejesha wachezaji hao kwa sababu lengo si kuwaona wakicheza mechi moja au mbili kisha kurejea tena kwenye chumba cha matibabu.
Kinachotafutwa ni kuhakikisha wanarudi wakiwa wamepona vizuri, wamejiandaa kimwili na wanaweza kuendelea na ratiba ya ushindani bila kupata tatizo jingine.”