Chipukizi yatamba kuikaribisha Black Sailors
Muktasari:
- Ofisa Habari wa Chipukizi, Kheri Kidema, amesema wamejipanga hususani kupambania nafasi nzuri kwenye msimamo na sio kushindana isishuke daraja kama ilivyozoeleka.
TIMU ya Chipukizi yenye Makao Makuu kisiwani Pemba, imesema imefanya usajili kuhakikisha inafanya vizuri kwenye Ligi Kuu Zanzibar 2026-2027, huku ikitamba kuikaribisha Black Sailors kwa kipigo.
Ofisa Habari wa Chipukizi, Kheri Kidema, amesema wamejipanga hususani kupambania nafasi nzuri kwenye msimamo na sio kushindana isishuke daraja kama ilivyozoeleka.
“Kikosi kimeshawasili kisiwani Unguja na kimeingia kambini kujiandaa na mchezo wetu wa kwanza dhidi ya Black Sailors tunataka kuanza na ushindi,”.
Alieleza kuwa, timu hiyo ipo tayari kwa mchezo huo na wanatambua kuwa sio rahisi licha ya kuwa ni timu ambayo imepanda daraja msimu huu.
Amesema, kwa kawaida timu ambazo zinapanda daraja huwa na ari na hamasa ya kuonesha kile walichonacho.
“Tunawaheshimu wapinzani, hivyo tumejidhatiti kuhakikisha hawafanyi makosa,” amesema.
Hivyo, Ofisa huyo amewaomba mashabiki wa timu hiyo waiunge mkono kwa sababu msimu wa 2026-2027 wamedhamiria kufanya makubwa.
Chipukizi ilimaliza nafasi ya 12 katika msimamo wa Ligi Kuu Zanzibar msimu uliopita 2025-2026 ikikusanya pointi 40, ikiizidi pointi tatu timu iliyokuwa chini yake, New King ambayo ni miongoni mwa zilizoshuka daraja.