Black Sailors yataka pointi tatu kwa Wembe
Muktasari:
- Timu hiyo iliyoanza msimu huu ikicheza dhidi ya Chipukizi, mchezo uliochezwa Agosti 31, 2026 na kumalizika bila kufungana, sasa imesema inazitaka pointi tatu kutoka kwa Wembe watakapokutana leo Alhamisi kwenye Uwanja wa Mao B, Unguja.
BAADA ya kuanza Ligi Kuu Zanzibar kwa suluhu, Black Sailors imesema imerudi uwanja wa mazoezi kujitathmini na kuboresha maeneo ambayo hayakuwa vizuri ili kuyaweka sawa kwa lengo la kupata matokeo bora mchezo ujao.
Timu hiyo iliyoanza msimu huu ikicheza dhidi ya Chipukizi, mchezo uliochezwa Agosti 31, 2026 na kumalizika bila kufungana, sasa imesema inazitaka pointi tatu kutoka kwa Wembe watakapokutana leo Alhamisi kwenye Uwanja wa Mao B, Unguja.
Akizungumza na Mwanaspoti, Kocha wa Black Sailors, Mohamed Hilali ‘Tedy’ alisema pointi moja sio ndogo kuipata kwenye Ligi Kuu Zanzibar hususani kwa mchezo wa kwanza wakiwa ndio wamepanda daraja.
Alisema, timu hiyo imefanya mabadiliko makubwa ya kikosi, hivyo wanahitaji kukaa pamoja ili kuifanya timu icheze kwa pamoja.
“Yapo makosa ambayo yalijitokeza kwenye mechi iliyopita, tumerudi uwanja wa mazoezi kurekebisha makosa hayo yasijirudie,” alisema.
Kocha huyo alisema kikosi chake kimekamilisha mchezo huo salama bila kupata majeraha kwa wachezaji, jambo ambalo linampa matumaini katika maandalizi ya mechi inayofuata. Alisema hali hiyo inawapa nafasi kubwa ya kuendelea na programu ya mazoezi bila changamoto na wachezaji wanaweza kuwatumia kusaka ushindi wao wa kwanza.
Alibainisha kuwa, wataendelea kuwafuatilia wachezaji kwa ukaribu ili kuhakikisha wanakuwa katika hali nzuri ya kiafya na kimwili kabla ya mchezo huo.