Timu Ndondo Cup zapata jezi
TIMU 14 za soka zinazoshiriki mashindano ya Ndondo Cup jijini Dar es Salaam zimepatiwa jezi za kutumia katika mashindano hayo msimu huu.
Timu zilizonufaika na jezi hizo ni Moro Warriors, Ujugu FC, Manzese Warriors, Keko Furniture, Kisa FC, Chuganism FC na Wagaigai FC.
Zingine ni Planet FC, Vigezo Combine FC, Mshikamo City, Chang’ombe Touth, Kigogo Fresh, Jaguar FC na Jet Lumo.
Akizungumza wakati akikabidhi jezi hizo, Meneja wa 10bet Tanzania, Kenan van Damme alisema wameamua kufanya hivyo ili kukuza thamani ya michezo ya ndani kwa jamii.
“Tunapenda sana michezo na kama raia tunaowajibika tunaelewa thamani ya michezo ya ndani kwa jamii. Tumejitolea kuendelea kusaidia jamii kupitia mipango endelevu ya michezo,” alisema Kenan ambao pia ndio wadhamini wa timu ya Dodoma Jiji inayoshiriki Ligi Kuu Bara.
Nahodha wa Keko Furniture, Rahim Kiana aliishukuru kampuni hiyo kuwawezesha kupata mavazi hayo ambayo watayatumia kuipigania timu yao uwanjani, akisema: “tumefarijika na msaada huu utakaongeza chachu na morali ya mashindano haya ya Ndondo Cup.”