Safari ya ajabu Argentina ikipambana kutetea taji lake
Muktasari:
- Kitu kinachoelezea zaidi safari ya La Albiceleste kuelekea mchezo wa mwisho ni kwamba katika mechi zake zote za hatua ya mtoano, haijawahi kuingia dakika ya 90 ikiwa mbele kwenye matokeo.
ARGENTINA imeandika sura ya kipekee katika historia ya Kombe la Dunia 2026 baada ya kufanikiwa kufika fainali kwa njia ambayo imekuwa ya kusisimua, yenye presha na kuvunja rekodi mbalimbali.
Kitu kinachoelezea zaidi safari ya La Albiceleste kuelekea mchezo wa mwisho ni kwamba katika mechi zake zote za hatua ya mtoano, haijawahi kuingia dakika ya 90 ikiwa mbele kwenye matokeo.
Badala yake, mabingwa hao watetezi wa dunia wamekuwa wakipambana hadi dakika za mwisho, wakitumia nguvu ya uzoefu, ubora wa Lionel Messi na uwezo wa kutengeneza matokeo katika mazingira magumu.
Katika mechi saba za hatua ya mtoano walizocheza katika Kombe la Dunia zilizopita na hili, Argentina imefika muda wa nyongeza mara nne, huku mbili kati ya hizo zikitokea katika safari hii ya mwaka 2026.
Sasa macho yote yanaelekezwa kwenye fainali dhidi ya Hispania itakayopigwa Jumapili hii Julai 19, 2026 kwenye Uwanja wa New York New Jersey, mchezo ambao utaanza saa 4:00 usiku kwa muda wa Afrika Mashariki.
Fainali hiyo tayari imeweka historia kwani itakuwa mara ya kwanza kwa timu mbili zilizopo nafasi ya kwanza na ya pili katika viwango vya FIFA kukutana kwenye mchezo wa kuwania ubingwa tangu mfumo huo ulipoanzishwa mwaka 1992.
Pia itakuwa mara ya kwanza kwa bingwa wa Ulaya kukutana na bingwa wa Copa América katika fainali ya Kombe la Dunia.
MESSI AANZA KWA NGUVU
Argentina ilianza kampeni yake kwa kishindo baada ya kuichapa Algeria mabao 3-0, huku Lionel Messi akiwa shujaa wa mchezo huo kwa kufunga hat-trick yake ya kwanza katika historia ya Kombe la Dunia.
Mabao hayo yalimfanya Messi kuwa mchezaji wa kwanza mwenye umri mkubwa zaidi kufunga hat-trick katika mashindano hayo akiwa na miaka 38 na siku 357, akivunja rekodi ya Cristiano Ronaldo.
Pia alifikisha rekodi nyingine baada ya kuwa mchezaji wa pili kufunga katika Kombe la Dunia tano tofauti, akimfuata Ronaldo.
Messi pia aliweka rekodi ya kuwa mfungaji mdogo zaidi na mkubwa zaidi wa Argentina katika Kombe la Dunia baada ya kufunga akiwa na miaka 18 mwaka 2006 na akiwa na miaka 38 mwaka huu.
AUSTRIA YAONA UBABE WAKE
Katika mchezo wa pili wa makundi dhidi ya Austria, Messi alikosa penalti mapema lakini alirekebisha makosa yake kwa kufunga mabao mawili na kuipa Argentina ushindi wa mabao 2-0.
Ushindi huo uliwafanya kufuzu hatua inayofuata wakiwa vinara wa Kundi J.
Messi alifikisha mabao 18 katika historia ya Kombe la Dunia, akiwa mchezaji wa kwanza kufikia idadi hiyo.
Pia akawa mchezaji wa pili kufunga mabao manne au zaidi katika Kombe la Dunia tatu tofauti baada ya Miroslav Klose.
Baada ya kufuzu mapema, kocha wa Argentina alifanya mabadiliko katika kikosi dhidi ya Jordan, lakini bado timu hiyo iliendelea kuonyesha ubora wake.
Giovani Lo Celso alifunga bao la kwanza lisilo la Messi katika mashindano hayo, kabla Lautaro Martínez hajaongeza jingine. Messi aliingia kipindi cha pili na kuonyesha ubora wake kwa kufunga kwa mpira wa adhabu, bao lililokuwa la sita kwake katika hatua ya makundi.
Bao hilo lilimfanya Messi kuongeza rekodi yake ya kuwa mfungaji bora wa muda wote wa Kombe la Dunia kwa kufikisha mabao 19 na pia kufunga katika mechi saba mfululizo.
PRESHA YA CAPE VERDE
Katika hatua ya 32 bora, Argentina ilinusurika dhidi ya Cape Verde baada ya mchezo huo kuhitaji muda wa nyongeza.
Messi aliitanguliza Argentina dakika ya 29, lakini Cape Verde ilisawazisha dakika ya 59 na kuleta hofu kwa mabingwa hao.
Argentina iliongoza tena dakika ya 92, lakini Sidny Lopes Cabral alisawazisha tena kabla ya bao la kujifunga la Cape Verde kuipa Argentina nafasi ya kusonga mbele.
Ushindi huo ulikuwa karibu kuwa moja ya vichapo vikubwa zaidi katika historia ya Kombe la Dunia kutokana na tofauti ya viwango vya FIFA kati ya timu hizo.
Messi pia alifikisha mabao 20 katika historia ya Kombe la Dunia, rekodi ambayo haijawahi kufikiwa na mchezaji mwingine.
COMEBACK YA KIHISTORIA
Mchezo dhidi ya Misri ulikuwa moja ya vipindi vigumu zaidi kwa Argentina.
Misri ilikuwa mbele kwa mabao 2-0 hadi dakika ya 79, lakini Argentina ilifanya mabadiliko makubwa ndani ya dakika 13 za mwisho na kushinda mabao 3-2.
Cristian Romero alianza kurejesha matumaini baada ya kufunga dakika ya 79 akitumia pasi ya Messi.
Messi mwenyewe alisawazisha dakika nne baadaye, kabla Enzo Fernández hajafunga bao la ushindi dakika ya 90+2.
Ilikuwa mara ya kwanza Argentina kushinda mchezo wa Kombe la Dunia baada ya kuwa nyuma kwa mabao mawili.
Kwa mujibu wa takwimu za Opta, Argentina ilikuwa na nafasi ya asilimia 0.6 pekee ya kushinda mchezo huo dakika ya 78.
USWISI, ENGLAND ZAKWAMA
Katika robo fainali dhidi ya Uswisi, Argentina ililazimika kupambana hadi dakika za mwisho. Alexis Mac Allister aliifungia Argentina dakika ya 10, lakini Uswisi ilisawazisha kupitia Dan Ndoye.
Mchezo ulionekana kuelekea kwenye mikwaju ya penalti kabla Julián Álvarez hajafunga bao la ushindi dakika ya 111, huku Lautaro Martínez akifunga la tatu dakika ya 120+1.
Katika nusu fainali dhidi ya England, Argentina ilionekana kuwa katika hatari baada ya kufungwa bao dakika ya 55. Lakini Messi aliongoza tena mapambano hayo baada ya kutoa pasi mbili za mabao yaliyofungwa na Enzo Fernández dakika ya 85 na Lautaro Martínez dakika ya 90+2. Ushindi huo uliihakikishia Argentina nafasi ya kucheza fainali yake ya saba ya Kombe la Dunia.
MESSI NA NDOTO YA TIKETI YA HISTORIA
Argentina sasa inakwenda kwenye fainali ikiwa na rekodi nyingi nyuma yake.
Timu hiyo imefunga mabao mawili au zaidi katika mechi 13 mfululizo za Kombe la Dunia, ikiwa rekodi mpya katika historia ya mashindano hayo.
Pia imefanya ushindi wa mechi 14 mfululizo katika mashindano yote na haijapoteza mechi 13 mfululizo za Kombe la Dunia.
Kwa Messi, safari hii imekuwa ya kuvunja rekodi zaidi. Nyota huyo amehusika moja kwa moja katika mabao katika mechi 11 mfululizo za Kombe la Dunia, rekodi ambayo haijawahi kufikiwa tangu takwimu za pasi za mabao zilipoanza kurekodiwa mwaka 1966.
Sasa Argentina inasubiri dakika 90 za mwisho dhidi ya Hispania, ikiwa na matumaini ya kuongeza taji lake la pili la Kombe la Dunia baada ya kushinda 2022 nchini Qatar na kumpa Lionel Messi kile ambacho dunia ya soka imekuwa ikisubiri kwa muda mrefu.