Prime
Makocha matajiri kwa kuwa na pato kubwa Ulaya
Muktasari:
- Kutokana na klabu kutumia pesa nyingi kwenye kulipia ada za kunasa makocha, jambo hilo limewafanya makocha hao kulipwa mishahara mikubwa pia inayowafanya kuwa na mapato makubwa.
LONDON, ENGLAND: SOKA limeandikisha idadi kubwa ya wachezaji na makocha wenye utajiri mkubwa katika kipindi cha muongo wa karibuni. Siku hizi, wachezaji na makocha kwenye mchezo huo, wanapiga pesa ndefu sana kwa mwaka.
Kutokana na klabu kutumia pesa nyingi kwenye kulipia ada za kunasa makocha, jambo hilo limewafanya makocha hao kulipwa mishahara mikubwa pia inayowafanya kuwa na mapato makubwa.
Kutokana na hilo, kumeibuka orodha ya makocha matajiri kutokana na kupata vipato vikubwa. Unawajua?
10. Arsene Wenger
Utajiri: Pauni 39 milioni
Amefahamika zaidi kwa nyakati zake alizokuwa kocha wa Arsenal na aliiwezesha timu hiyo kubeba mataji matatu ya Ligi Kuu England na kuibadili timu hiyo kuwa ya viwango bora na kucheza soka matata kabisa.
Wenger aliifanya Arsenal kucheza msimu mzima bila ya kupoteza mechi kwenye ligi.
Kwa sasa ni bosi wa maendeleo ya soka duniani huko Fifa, huku akiripotiwa kuwa na pato la Pauni 39 milioni.
9. Carlo Ancelotti
Utajiri: Pauni 41.4 milioni
Kuna makocha wachache waliowahi kubeba mataji mengi kama ilivyo kwa Carlo Ancelotti.
Ancelotti ameshinda ubingwa wa ligi kwenye nchi zote zenye ligi tano kubwa za Ulaya, England, Hispania, Ujerumani, Italia na Ufaransa. Kwa sasa ni kocha wa Real Madrid na anafanya vizuri kwa miamba hiyo ya Los Blancos, huku jambo hilo likiandana na uchumi wake, akiripotiwa kuwa na pato la Pauni 41.4 milioni.
8. Jurgen Klopp
Utajiri: Pauni 41.8 milioni
Kuna makocha wachache sana wenye mashabiki wengi na ambao wamezibadili klabu na kuwa za mataji kama alivyofanya Jurgen Klopp katika klabu ya Liverpool.
Kabla hajatua Anfield, alikuwa kipenzi cha mashabiki huko Borussia Dortmund. Klopp amekuwa na uwezo mkubwa wa kutengeneza urafiki na mashabiki kwenye timu anazozinoa, huku akiwa vizuri pia kiuchumi, pato la Pauni 41.8 milioni.
7. Sir Alex Ferguson
Utajiri: Pauni 53.6 milioni
Kocha bora wa muda wote, gwiji kabisa kwenye soka, Sir Alex Ferguson ni miongoni mwa mabosi wa mabenchi ya ufundi matajiri. Mskochi huyo ndiye aliyewajibika kuibadili Manchester United na kuwa timu tishio England, Ulaya na duniani kwa jumla. Kwa sasa Man United yake ipo ovyo, lakini kwa upande wake mambo hayaendi vibaya, akiripotiwa kuwa na pato ya Pauni 53.6 milioni.
6. Steven Gerrard
Utajiri: Pauni 74.5 milioni
Mambo bado hayajakaa vizuri kwa Steven Gerrard kwenye kazi yake ya ukocha, lakini ni mmoja wa makocha matajiri kwenye mchezo huo, akiripotiwa kuwa na pato la Pauni 74.5 milioni.
Baada ya kuanza vyema kazi ya ukocha kwenye kikosi cha Rangers, Gerrard alienda Aston Villa alikochemsha kabla ya kutimkia Saudi Arabia kuinoa Al-Ettifaq.
5. Zinedine Zidane
Utajiri: Pauni 99 milioni
Zinedine Zidane maisha yake ya ukocha yamegawanyika kwenye zama mbili, lakini zote alikuwa kwenye kikosi cha Real Madrid, ambako aliweka rekodi ya kunyakua taji la Ligi ya Mabingwa Ulaya kwa misimu mitatu mfululizo.
Amekuwa hana kazi kwa muda mrefu sasa, lakini jambo hilo halimfanyi Zidane kutoka kwenye tano bora ya makocha wenye kipato kizuri, akiwa na utajiri wa Pauni 99 milioni.
4. Pep Guardiola
Utajiri: Pauni 100 milioni
Wakati Sir Alex Ferguson akiheshimika kama kocha bora zaidi kuwahi kutokea kwenye Ligi Kuu England, Pep Guardiola amepanda kwenye anga hizo na kuwa namba mbili.
Kwa kile alichofanya kwenye kikosi cha Barcelona, Bayern Munich na sasa Manchester City, Mhispaniola huyo ameliweka juu jina lake, huku jambo hilo likimpa pesa na kuwa na utajiri wa Pauni 100 milioni.
3. Jose Mourinho
Utajiri: Pauni 100 milioni
Akilingana na Guardiola kwa kuwa na utajiri wa Pauni 100 milioni, Jose Mourinho ni mmoja wa makocha wa soka wenye historia kubwa kwenye mchezo huo.
Kocha huyo aliyejipachika jina la Special One, amefanya kazi kwenye timu nyingi kuanzia FC Porto, Chelsea, Inter Milan, Real Madrid, Manchester United na Tottenham kwa kuzitaja kwa uchache na utajiri wake ni Pauni 100 milioni.
2. Diego Simeone
Utajiri: Pauni 107.7 milioni
Kwenye soka la kizazi kipya, hakuna kocha aliyejikita kwenye timu moja kwa muda mrefu kama Diego Simeone huko Atletico Madrid.
Muargentina huyo yupo Atletico tangu 2011 na amefanikiwa kuijenga timu hiyo katika misingi bora na kushindana na vigogo Real Madrid na Barcelona kwenye La Liga.
Ukocha umempa pesa nzuri na sasa anaripotiwa kuwa na utajiri wa Pauni 107.7 milioni.
- Wayne Rooney
Utajiri: Pauni 170 milioni
Bado anajitafuta hana alichokifanya cha maana tangu alipohamia kwenye ukocha, lakini ukweli utabaki kuwa ulivyo, ndiye kocha tajiri zaidi kwa waliopo kwenye soka la Ulaya kwa sasa, kutokana kuwa na utajiri wa Pauni 170 milioni.
Rooney kwenye kazi ya ukocha amezinoa Birmingham City, Plymouth Argyle na Derby County.