KISIWA CHA MAUTI - 8
ILIPOISHIA
Nikaipokea.
“Shikamoo mkuu” nikamwamkia.
“Marahaba. Mbona hujaonekana tangu jana”
Nikamueleza kile kilichotokea.
“Kwani wewe uko wapi?”
“Sipendi niseme niko wapi lakini nipo hapa Dar”
“Hizo taarifa tumeshazipata, sasa nataka uje hapa ofisini”
“Sitaweza kuja. Bado nafikiria nifanye nini”
SASA ENDELEA...
“Sikiliza Masha. Njoo hapa ofisini tushauriane. Bado utakuwa na hiyari ya kwenda polisi au kutokwenda”
“Mkuu naomba uniache tu…”
“Utakuwa kama umekusudia kufanya hilo tukio. Sisi tuna maswali ambayo tunajiuliza ambayo yanaweza kukusaidia wewe. Najua umetaharuki lakini ni vizuri uje hapa ofisini”
“Sawa. Nitakuja”
Mhariri akakata simu. Sikuwa na nia kwenda tena ofisini. Nilimjibu kuwa nitakwenda ili kukatisha yale mazungumzo tu. Nilipokata simu niliamua nivae nguo niende nyumbani, nichukue vitu vyangu muhimu kisha nijue pa kwenda. Nilihisi huenda polisi walikuwa hawajafika nyumbani.
Nilitoa pikipiki nikaanza safari ya kuelekea mtaa ninaoishi. Wakati naendesha, picha ya yule msichana ilinijia mbele ya macho yangu. Nilikuwa kama ninayemuona akinimiminia bia kwenye bilauli na kuniambia ‘karibu’ huku uso wake ukiwa na tabasamu.
Picha iliendelea kunijia wakati akinitajia jina lake. Mara nyingi msichana wa kimjini unapoanza kujuana naye hupenda kuficha jina lake na kutaja jina la uongo. Lakini yeye alinitajia jina lake la kweli aliponiambia anaitwa Edda. Alikuwa msichana mpole sana na mwenye kuthamini mahusiano.
Wakati ile picha ikiendelea kunijia, nilijihisi nilikuwa mwenye hatia kuitoa roho ya msichana yule kwa sababu ya ulevi. Niliamini ni kwa sababu ya ulevi kwakuwa alishanirusu nifike kwake kwa maongezi zaidi.
Baada ya dakika chache tu nikaingia katika mtaa niliokuwa ninaishi. Tangu nikiwa mbali niliona gari limesimama mbele ya nyumba niliyokuwa nimepanga chumba. Nilipolikazia macho gari hilo nikagundua kuwa lilikuwa gari la polisi.
Nikasimamisha pikipiki haraka. Niliona polisi wakiingia na kutoka mle ndani. Nikageuza pikipiki na kurudi. Nilijua kuwa wale polisi walikuwa wamenifuata mimi wakijua nitakuwa nyumbani kwangu.
Kama ningerudi nyumbani mapema polisi hao wangenikuta na kunikamata.
Nikiwa nimeikoleza pikipiki nikirudi, nikaona simu yangu inaita. Kwanza nilitaka nihakikishe kuwa niko mbali na ule mtaa ninaoishi, ndipo nisimamishe pikipiki na kuona ni nani aliyekuwa ananipigia.
Niliporidhika kuwa mahali nilipofika nilikuwa salama nikasimamisha pikipiki na kutoa simu.
Simu ilikuwa imeacha kuita lakini niliona namba ya Edda, yule msichana niliyemuua kule hoteli!
Nikashituka na kujiuliza, huyu msichana ni yule yule au ni mwingine?
Kwa kutaka kujua nikaipiga ile namba. Ikapokelewa. Sikusema kitu. Nikasikia sauti ya mwanamke ikisema.
“Vipi Masha, habari ya tangu jana?”
Sikuwa na shaka yoyote kuwa ilikuwa sauti ya Edda. Nikajiuliza nilikuwa naota au niko katika maisha halisi?
Nikajiambia kama naota au niko katika maisha halisi nitajua.
“Nzuri. Habari yako?” nikamsalimia.
“Nzuri. Leo sijafika kazini. Nina mapumziko”
“Nazungumza na Edda au…?”
“Ndiyo, mimi Edda”
“Wewe ni Edda?”
“Ndiyo. Si nilikupa namba yangu jana kule hoteli”
“Ndiyo ulinipa. Lakini sikumbuki tulivyoachana”
“Mimi nilimaliza zamu yangu nikaondoka, nikakuacha unaendelea kunywa”
“Nilikuwa nikihudumiwa na nani?”
“Na mhudumu mwingine msichana mwenzangu”
Nikajiuliza kimoyo moyo huyo mwenzake ndiye niliyemuua kule chumbani?
“Hakuna taarifa zozote ulizopata kutoka huko Hoteli?”
“Kuhusu nini?”
“Kuhusu mimi”
“Sijapata taarifa yoyote, kwani hukuonana na Bosi?”
“Sikuonana naye”
“Yule mzee atakusumbua, yuko bize sana”
“Wewe uko wapi muda huu?”
“Nilikuwa nimekwenda saluni. Hivi sasa ninarudi, niko kwenye kibajaj”
“Unarudi wapi?”
“Nyumbani”
“Mimi nakuja huko huko”
“Njoo, utanikuta”
“Sawa”
Nikakata simu. Nilikuwa nimezima pikipiki, nikaiwasha haraka na kuondoka. Nilitaka kwenda nyumbani kwa msichana huyo ili nithibitishe kwamba ndiye yeye Edda kweli.
Hapo sikufikiria tena habari ya polisi. Nikaelekea katika mtaa huo. Nilipokata kona tu kuingia katika mtaa huo, nyumba aliyonielekeza Edda niliiona. Ilikuwa ya pili mkono wa kushoto.
Vile natokea tu nikaona bajaj inasimama mbele ya nyumba hiyo. Nikamuona msichana anashuka kwenye bajaj hiyo na kuagana na dereva wa bajaj.
Nilishituka na kushangaa nilipogundua alikuwa Edda! Nikataka nimuwahi kabla hajaingia ndani. Nilipoifikia nyumba hiyo Edda alikuwa amefunguliwa mlango.
Nikafunga breki barazani na kumuita.
“Edda…!”
Edda akageuka na kunitazama.
“Ah… Masha!” akasema huku akitabasamu kisha akaongeza.
“Inaonekana ulikuwa karibu”
“Wakati nazungumza na wewe nilikuwa nyumbani kwangu. Mimi pia naishi hapa Kinondoni”
Wakati namwambia hivyo nilikuwa najiuliza, huyu msichana si nimemuua, mbona yuko hai?
“Ulivyoniambia ninakuja sikuamini. Nilijua unanitania tu” Msichana akaniambia.
Sasa niligundua kuwa niliyemuua alikuwa msichana mwingine.
“Kwanini nikutanie wakati tumekubaliana?”
“Basi karibu ndani”
Nikaiegesha vyema pikipiki kisha nikaizima”
Msichana alitangulia kuingia ndani. Nikamfuata.
Chumba chake kilikuwa cha kwanza cha mkono wa kulia.
Alitoa funguo akafungua mlango wa chumba hicho kisha akaingia ndani. Nilibaki mbele ya mlango wa chumba hicho mpaka alipotoa kichwa na kuniambia.
“Karibu ndani”
Nikaingia.
Kilikuwa chumba kidogo kama vilivyo vyumba vya nyumba nyingi za Dar es Salaam zilizojengwa kibiashara. Kilienea kitanda cha futi sita kwa sita. Kabati dogo la nguo lililokuwa na kioo cha kujitazamia na sofa moja kubwa.
“Karibu ukae” akaniambia.
Nikakaa kwenye lile sofa
Alifunua pazia la dirisha lililokuwa upande wa nje. Mwanga ukaingia ndani. Baada ya hapo alikwenda kuketi kwenye kitanda.
“Nakuona umependeza!” nikamwambia huku nikimtazama kichwani. Nywele zake zilikuwa zimewekewa dawa na kuwekwa katika mtindo maalum.
Msichana akaminya midomo yake kutabasamu. Alipofanya hivyo mashavu yake yaliunda vishimo na kuufanya uso wake uonekane wa kupendeza zaidi.
“Asante” akaniambia na kuongeza.
“Si unajua leo nina mapumziko. Naweza kutoka”
“Unaweza kutoka uende wapi? Halafu mgeni wako umuachie nani?” nikamuuliza. Nusu ulikuwa mzaha, nusu ilikuwa kweli.
“Kwani utashinda hapa kwangu?”
“Naweza, kwani kuna tatizo?”
“Hakuna tatizo, ni wewe tu”
“Nitakuwa nimekuvunjia safari zako?”
“Hapana. Kama utakuwa hapa sitatoka”
Ili kumpa moyo na aone kuwa nitakuwa naye kama nilivyomwambia nilitia mkono mfukoni mwangu nikatoa pochi yangu. Niliifungua na kutoa noti mbili nyekundu. Nina maana noti za elfu kumi kumi. Nikampa.
“Mgeni njoo mwenyeji apone. Nenda sokoni ufanye maandalizi ya msosi wa mchana” nikamwambia.
Edda alizipokea zile pesa huku akicheka.
“Unasemaje, mgeni njoo mwenyeji apone? Sasa maana yake nini?”
“Maana yangu ni kuwa leo hutatumia pesa yako”
“Kweli?”
“Nimekuja kikamilifu baada ya yale mazungumzo yetu ya jana”
“Tena kama umegundua, leo nina mapumziko”
“Ndio hapo sasa, ukae tuzungumze”
“Sasa subiri basi niende sokoni nifanye maandalizi ya chakula”
“Sawa. Wewe nenda. Mimi nipo”
“Sijui ungependa chakula gani mgeni wangu?”
“Chochote tu unachopenda wewe”
“Mimi napenda ndizi”
“Sawa”
“Ninunue ndizi na nini, nyama au samaki?”
“Samaki”
“Subiri niende mara moja”
Edda alipotoka nikaanza kuwaza. Nilijiuliza ni msichana gani niliyemuua? Msichana ambaye nilimuona pale chini amekufa alikuwa ni Edda na ndiye aliyekuwa akinihuduumia pale hoteli.
Isitoshe nilikiona kitambulisho chake kilichokuwa kimeanguka. Alikuwa ni Edda na hakuwa msichanna mwingine.
Sasa kama Edda yuko hai, ule mwili niliouona pale chini, ulikuwa wa nani?
Nikakumbuka kwamba Edda aliniambia aliniacha nikihudumiwa na msichana mwingine. Nikajiuliza huyo msichana mwingine ndiye niliyemuua?
Niliendelea kujiuliza, kama niliyemuua alikuwa msichana mwingine, mbona taarifa nilizoziona kwenye blogy zinaonesha kuwa aliyeuawa alikuwa Edda!
Hapo nilishindwa kupata jibu. Nikajiambia ni vizuri Edda atakaporudi niendelee kumdadisi. Huenda nikagundua yule msichanna alikuwa nani.
Lakini pia nilijiuliza, kwanini Edda hakuwa na habari ya tukio lilotokea hapo hoteli ambako anafanya kazi? Hata kama si yeye niliyemuua, kwanini asijue kilichotokea?