Spurs kuitikisa Man United kwa Bryan Mbeumo

Muktasari:
- Mbeumo anadaiwa kuwa katika orodha ya mastaa ambao wanaweza kukamilisha uhamisho wa kujiunga na Man United muda wowote kwani ameshafikia makubaliano binafsi na timu hiyo.
KOCHA wa Brentford Thomas Frank, ambaye anatarajiwa kuchukua nafasi ya Ange Postecoglou kama kocha wa Tottenham, ameiambia timu hiyo kuwa anahitaji saini ya straika wa Brentford na timu ya taifa ya Cameroon, Bryan Mbeumo, 25, katika dirisha lijalo la majira ua kiangazi.
Mbeumo anadaiwa kuwa katika orodha ya mastaa ambao wanaweza kukamilisha uhamisho wa kujiunga na Man United muda wowote kwani ameshafikia makubaliano binafsi na timu hiyo.
Hata hivyo, Frank anamhitaji sana Mbeumo kwa sababu anafahamu uwezo wake kwani alionyesha kiwango chini yake katika kikosi cha Brentford kwa msimu uliopita.
Hata hivyo, licha ya ushawishi wake kwa staa huyu, ripoti zinadai klabu hiyo italazimika kuweka kiasi kikubwa cha pesa ili kuipuku ofa ya Man United.
Ingawa aliwahi kuchezea timu ya taifa ya vijana ya Ufaransa, Mbeumo aliamua kuiwakilisha Cameroon, na alicheza mechi yake ya kwanza ya kimataifa kwa timu hiyo mwaka wa 2022.
Mwishoni mwa mwaka huo, alijumuishwa kwenye kikosi cha Cameroon kilichoshiriki Kombe la Dunia la FIFA, na alicheza mechi tatu.
Joao Pedro
NEWCASTLE United iko katika harakati za kutaka kumsajili mshambuliaji wa Brighton na timu ya Brazil, Joao Pedro, mwenye umri wa miaka 23, kwa ajili ya kuboresha eneo lao la ushambuliaji.
Pedro ambaye msimu huu amecheza mechi 52 za michuano yote na kufunga mabao matano, mkataba wake unatarajiwa kumalizika mwaka 2029.
Milos Kerkez
BEKI wa kushoto wa AFC Bournemouth, Milos Kerkez, 21, ameondoka katika kambi ya timu ya taifa ya Hungary kwa ajili ya kukamilisha uhamisho wake wa kujiunga na Liverpool katika dirisha hili.
Kerkez ambaye msimu uliopita alicheza mechi 41 za michuano yote, mkataba wake wa sasa unatarajiwa kumalizika mwaka 2028.
Rafael Leao
WINGA wa AC Milan na timu ya taifa ya Ureno, Rafael Leao ameiambia timu yake kwamba anataka kuondoka klabuni hapo katika dirisha lijalo la majira ya kiangazi.
Inaelezwa Milan ipo tayari kumuuza staa huyu lakini kwa kiasi kisichopungua Pauni 59 milioni.
Timu kadhaa ikiwemo Bayern Munich zinahitaji saini yake.
Mike Maignan
CHELSEA inatarajia kurudi na ofa ya pili kwenda AC Milan kwa ajili ya kumsajili kipa wa timu hiyo na Ufaransa, Mike Maignan, mwenye umri wa miaka 29, baada ya ombi la kwanza kukataliwa.
Mabosi wa Milan walikataa ofa ya kwanza ya Chelsea kwa sababu haikuwa inafikia kiasi ambacho walikihitaji. Mkataba wake wa sasa unatarajiwa kumalizika mwaka 2026.
Leroy Sane
FENERBAHCE imeingia katika vita dhidi ya Galatasaray ya Uturuki katika harakati za kumsajili winga wa Bayern Munich na timu ya taifa ya Ujerumani, Leroy Sane, mwenye umri wa miaka 29, ambaye bado hajafikia makubaliano ya kusaini mkataba mpya wa kuendelea kusalia Allianz Arena.
Hadi sasa mazungumzo baina ya Sane na vigogo wa Bayern yanaendelea lakini bado hawajafikia mwafaka.
Randal Kolo Muani
JUVENTUS imefikia makubaliano na Paris Saint-Germain ya kumsajili kwa mkopo wa msimu mmoja mshambuliaji wa timu hiyo na Ufaransa, Randal Kolo Muani, mwenye umri wa miaka 26, ili aweze kuichezea timu hiyo ya Serie A katika Kombe la Dunia la Klabu la FIFA.
Katika msimu uliopita, Muani alicheza mechi 33 za michuano yote na kufunga mabao 10.
Jonathan Tah
BAYERN Munich imefikia makubaliano na Bayer Leverkusen kwa ajili ya kumsajili beki wa timu hiyo na Ujerumani Jonathan Tah, mwenye umri wa miaka 29, kabla ya mkataba wake kumalizika Juni 30 ili aweze kucheza kwenye Kombe la Dunia la Klabu la FIFA.
Tah ambaye awali alidaiwa kwamba anaweza kuondoka akiwa mchezaji huru, msimu uliopita alicheza mechi 49.