Rooney na ishu ya sigara kambini
Muktasari:
- Carroll ameyafichua hayo kupitia kitabu chake kipya cha kumbukumbu za maisha ya soka, Owning It, akieleza kwa kina namna wachezaji walivyokuwa wakijiburudisha kambini wakati wa utawala wa kocha Fabio Capello.
LONDON, ENGLAND: MAMBO mazito yameibuka ndani ya kikosi cha zamani cha England baada ya mshambuliaji wa zamani wa timu hiyo, Andy Carroll, kufichua siri za kambi ya Three Lions, akidai nyota mwenzake Wayne Rooney alikuwa akivuta sigara na kunywa bia wakati wa majukumu ya timu ya taifa.
Carroll ameyafichua hayo kupitia kitabu chake kipya cha kumbukumbu za maisha ya soka, Owning It, akieleza kwa kina namna wachezaji walivyokuwa wakijiburudisha kambini wakati wa utawala wa kocha Fabio Capello.
Kwa mujibu wa Carroll, Rooney alikuwa miongoni mwa wachezaji waliokuwa wakitafuta namna ya kuvunja ukimya na uchovu wa maisha ya kambini.
Carroll anadai Rooney alikuwa akimpigia simu majira ya mchana na kumwambia: ‘Andy, njoo chumbani kwangu sasa. Alisema mara kadhaa alipofika chumbani kwa Rooney, alimkuta nyota huyo akiwa amelala kitandani akiangalia televisheni huku akivuta sigara na kunywa chupa ya bia.
Carroll pia anadai chumba cha Rooney kilikuwa na katoni za sigara, kreti za bia na chupa za mvinyo ambazo, kwa madai yake, Rooney aliagiza ziletwe na meneja wa hoteli. Hata hivyo, Carroll anasisitiza kuwa wachezaji hawakuwa wakilewa kupita kiasi.
ROONEY AKANUSHA
Lakini Rooney amepinga vikali madai hayo, akisema simulizi hiyo haina ukweli wowote.
Rooney, ambaye sasa ni mchambuzi wa televisheni, alisema ameamua kulizungumzia suala hilo kwa sababu anafahamu Carroll na yeye hawakuwa na uhusiano wa karibu kiasi cha kuhusisha matukio kama hayo.
Alisema: “Andy anajua kwamba mimi na yeye hatukuwahi kushirikiana sana kijamii. Tulikutana kwa bahati mara moja tukiwa kwenye likizo, lakini hilo ndilo.â€
Rooney akaongeza kuwa madai ya yeye kunywa pombe akiwa kwenye majukumu ya England ni ya kutungwa.
“Kuhusu hii hadithi kwamba nilikuwa nikinywa nikiwa kwenye majukumu ya England, ni uzushi kabisa. Sijui imetoka wapi. Inakatisha tamaa,”€ alisema.
UTANI WA ROONEY
Katika kitabu hicho, Carroll pia amesimulia tukio jingine la utani ambalo Rooney alilifanya dhidi ya mtaalamu wa tiba ya viungo wa England, Rod Thornley.
Carroll anasema baada ya kumweleza Rooney kuhusu mchezo wa kuwabeba wachezaji watatu, Rooney alisisimka na kusema walipaswa kumfanyia Thornley.
Kwa mujibu wa simulizi hiyo, Rooney alikaa juu ya Thornley aliyekuwa amelala kwenye meza ya matibabu.
Carroll anasema Thornley alikuwa akipiga kelele huku yeye na Steven Gerrard wakicheka sana, huku Rooney akionekana kufurahia utani huo.
Rooney aliichezea England mechi 120 na kufunga mabao 53, akiwa mmoja wa wachezaji muhimu zaidi katika historia ya Three Lions.
GOLDEN GENERATION’ ILIKUWA NA MIGOGORO
Carroll pia amefichua kuwa kizazi maarufu cha England kilichoitwa ‘Golden Generation’€ kilikuwa na mgawanyiko wa wachezaji kutoka kaskazini na kusini mwa England.
Katika kipindi hicho, England ilikuwa na mastaa kama Rooney, Steven Gerrard, Frank Lampard, John Terry, Ashley Cole, Joe Cole na Jamie Carragher, lakini ilishindwa kutwaa taji lolote kubwa.
Carroll anasema alipowasili kambini kwa mara yake ya kwanza, alikuwa na hofu kubwa kwa sababu aliwakuta mastaa aliokuwa akiwatazama kwa heshima.
Hata hivyo, anadai kulikuwa na makundi mawili ndani ya chumba cha wachezaji wale kutoka klabu za kaskazini upande mmoja na wale wa kusini upande mwingine.
Anasema hali hiyo ilifikia hatua ambapo baadhi ya wachezaji hawakuwa wakizungumza na wenzao na wengine walikuwa wakisita hata kupeana pasi mazoezini.
Carroll alisema alijikuta akiungana zaidi na kundi la wachezaji kutoka kaskazini.
CAPELLO NA SIMU
Carroll pia amesimulia namna kocha Fabio Capello alivyokuwa mkali kambini.
Anasema siku moja yeye na Ashley Young waliwasili kwenye kikao dakika 15 kabla ya muda. Carroll alikuwa ameketi sakafuni akitumia simu yake wakati Capello alipoingia, akaichukua simu hiyo na kumkaripia kwa hasira. Kwa mujibu wa Carroll, Capello alimwambia walikuwa wamekusanyika kwa ajili ya kufanya kazi na matumizi ya simu yalikuwa ni dharau.
Carroll anasema Capello alimtupia simu hiyo kifuani.
Pamoja na ukali huo, Carroll anadai Capello aliwaruhusu wachezaji kunywa glasi ya mvinyo pamoja na chakula cha mchana na cha jioni, huku wakiruhusiwa pia kula dessert kama keki ya chokoleti na ice cream.
Kilichomshangaza Carroll ni kwamba kocha huyo hakuruhusu wachezaji kutumia ketchup.
“Haikuwa na maana kwa nini mvinyo na dessert viruhusiwe lakini ketchup ikatwe?”€ Carroll amehoji.