Syllersaid Mziray 'Super Coach' afariki
Marehemu Syllersaid Mziray akiwa na kocha Phiri na Musa Mgosi
*Aliipa Tanzania Bara Chalenji 1994 Waandishi Wetu MMOJA wa makocha wasaidizi wa timu ya Simba, Syllersaid Kahema Mziray 'Super Coach' amefariki. Mziray alifariki jana saa 10 alifajiri katika hospitali ya Aga Khan. Habari zilizopatikana jana asubuhi hospitalini hapo zilisema kuwa alikuwa anasumbuliwa na figo. Kocha huyo mwenye misimamo na kusimamia kile anachokiamini, alilazwa kwa siku kadhaa kwenye hospitali hiyo na kuruhusiwa kabla ya kurudishwa na baadaye kukutwa na umauti huo. Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Chuo Kikuu Huria, OUT, Albert Memba aliiambia Mwananchi Jumapili jana kuwa taratibu zilikuwa zikiandaliwa kwa ajili ya mazishi ya Mziray aliyekuwa mhadhiri wa chuo hicho. Akimzungumzia Mziray aliyeleta Kombe la Chalenji 1994 kutoka Kenya, alisema kuwa Chuo kimempoteza mtu makini, rafiki, ndugu na si chuo pekee hata jamii na zaidi ni tasnia ya michezo. Alisema kuwa Mziray alikuwa msema kweli na alikuwa na misimamo yake ambayo aliamini ndiyo nguzo yake. "Ameleta heshima, kati ya makocha wenye historia nzuri, Mziray ni mmojawapo, kwa kweli ni pigo la aina yake na hatuwezi kupata mtu kama Mziray," alisema. Alisema kuwa kifo chake kimekuja wakati maandalizi ya kumpeleka India kwa ajili ya kufanyiwa upasuaji wa figo, yalikuwa yakifanyika. *Mazishi Baada ya kifo chake jana alfajiri, Mziray anatarajia kuzikwa kesho saa 10 jioni kwenye makaburi ya Kinondoni jijini Dar es Salaam. Akizungumza nyumbani kwa marehemu Tabata Magengeni jijini Dar es Salaam, kaka wa marehemu, Abdallah Mziray alisema kuwa kabla ya mazishi kutatanguliwa na shughuli ya kuuaga mwili wa marehemu zitakayofanyika Chuo Kikuu Huria kesho saa 4:00 asubuhi. Alisema kuwa uamuzi wa kumzika marehemu kesho unalenga kutoka nafasi kwa watu mbalimbali wakiwemo wadau wa soka na viongozi wa serikali kupiga kura leo na baada ya hapo wapate nafasi ya kumuaga mpendwa wao. "Kimsingi tulitaka kufanya mazishi kesho (leo)lakini baada ya kuangalia kwa umakini suala nyeti la kupiga kura tumeamua tufanye Jumatatu ili tusiwanyime nafasi watu mbalimbali wakiwemo wadau wa soka na viongozi wa serikali fursa ya kumuaga mpendwa wetu," alisema Abdallah. Kwa kujibu wa Abdallah, marehemu ameacha watoto wawili ambao ni Mariam na Robert. Wakati huo huo Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, kupitia kwa Kaimu Katibu Mkuu wake, Sunday Kayuni jana lilitoa taarifa likisema limepokea kwa mshituko taarifa za kifo cha Mziray na kutoa pole kwa familia ya marehemu. Katika taarifa yake TFF, Kayuni alisema kuwa marehemu Mziray alikuwa mtu muhimu katika maendekeo ya soka nchini . Katika hatua nyingine kikosi cha Simba ambacho kipo kambini jijini Mwanza kinatarajia kurejea Dar es Salaam leo. Mjumbe wa kamati ya fedha ya Simba Joseph Itang'are(Kinesi)alisema jana kuwa lengo la kukirejesha kikosi cha Simba Dar es Salaam ni kutoa fursa kwa wachezaji na viongozi wao kumuaga na kumzika kocha wao. *Mwandishi wa Mwananchi Jumapili afutiwa picha Katika hali isiyokuwa ya kawaida, ndugu na jamaa za marehemu aliyekuwa kocha msaidizi wa timu ya soka ya Simba, Syllersaid Mziray jana walimfanyia fujo na kumpora kamera na kutishia kumpiga Mwandishi wa Habari wa gazeti hili, Joseph Zablon kwa madai kuwa hana kibali cha kuripoti tukio hilo la msiba. Sakata hilo lilianza mara baada ya mwandishi huyo kufika nyumbani kwa marehemu Mziray eneo la Tabata Magengeni kuingia ndani kuwapa pole wafiwa kisha kuanza kupiga picha waombolezaji akiwemo mke wake ambaye alikuwa akifarijiwa na ndugu wengine. Mara baada ya kuwapiga picha waombolezaji aliamriwa na mmoja wa waombolezaji akimtaka aondoke nyumbani hapo hadi pale atakapopata kibali cha wanafamilia na licha ya mwandishi kujitambulisha na kueleza kuwa marehemu ni mtu maarufu ambaye pia ana mchango mkubwa kwa taifa hivyo wengi wangependa kujua habari zake, hata hivyo walitaka mwandishi aondoke. "Nasema toka nje, unapiga picha kwa ruksa ya nani? alifoka mwanadada huyo na kuongeza kuwa hata waandishi wa ITV wamepiga simu hawajafika hapa na tumewaambia ni mapema mno," alisema mwanadada huyo na mwandishi alitoka nje kusubiri utaratibu mwingine. Dakika chache baadaye alifuatwa na mmoja kati ya watoto wawili wakubwa wa Mziray ambaye alifahamika kwa jina la Robert na kumtaka mandishi kutoa kamera. "Weee ndio ulikuwa unapiga picha uwani? alihoji na hata alipojibiwa kuwa hapana alimtaka mwandishi kumkabidhi kamera kwa usalama wake na muda mfupi baadae alitokea mtu mwingine aliyejulikana kwa jina moja la Lewis akiwa na jazba na kumvamia mwandishi, kumkunja na kutishia kumpiga. Mwanandugu huyo alihoji kibali cha kupiga picha msiba huo na kabla na kutishia kumtwanga kwa kipande cha tofali huku akimtaka aeleze alikopata kibali cha kupiga picha. "Nani kakupa kibali cha kupiga picha katika msiba huu" alifoka na hata alipoelezwa umuhimu wa marehemu, aling'aka kwa jabza na alitulizwa na mama mmoja ambaye alimuita kwa jina na kumtaka aichukue kamera na kuziharibu picha zilizomo. Wakati wote huo, mtoto wa marehemu Mziray, Robert alikuwa akihangaika kuikwapua kamera kutoka katika mkoba wa mwandishi "mjomba Lewis mwache, usimpige, mnyang'anye tu hiyo kamera uharibu picha, " alisema mama huyo na ndipo yakawa manusura ya mwandishi ambapo sasa mwanandugu huyo akawa anahaha kuhaaribu picha zilizomo. Zoezi hilo hata hivyo lilimshinda na ndipo alipomuita Robert na kumtaka amsaidie kuharibu picha ambayo ilikuwa imepigwa ya mke wa marehemu Mziray wakati akifarijiwa na waombolezaji waliofika nyumbani kwao hapo na baada ya kufanikisha uharibu huo walirdisha kamera kwa mwandishi na kumuamuru aondoke. *Makao Makuu klabu ya Simba Baadhi ya wanachama wa Simba na wadau wa mpira wa miguu hapa nchini wameelezea kusikitishwa na taarifa za kifo cha aliyekuwa kocha mshauri wa klabu hiyo, Syllersaid Mziray. Wakizungumza na Mwananchi Jumapili kwa nyakati tofauti wadau hao walikuwa na nyuso za huzuni kufuatia msiba huo wa ghafla walisema kifo hicho kimewashtua na kimemuondoa mtu muhimu katika sekta ya michezo. Mmoja wa wanachama hao, Ali Said Bia (no. 36) alisema Mziray ameweza kuisaidia Simba kwa kiasi kikubwa hasa zinapokutana na Yanga kwa kutoa hamasa na kuifanya ipate matokeo mazuri. "Ukweli msiba huu umetupunguzia mtu muhimu sana katika mchezo wa mpira wa miguu..hatutaweza kumsahau kwani amekua mchango mkubwa sana katika kuileta Simba mafanikio," alisema mwanachama huyo. Naye Rukia Juma (01284) amemwelezea Mziray kama mfano wa kuigwa na makocha wazalendo hapa nchini kwa uwajibikaji wake katika kuinua soka. Mbali na Simba, alizinoa klabu mbalimbali ikiwemo Yanga, Pilsner, African Sports, Tanzania Stars na kuzipa mafanikio katika medani ya soka. Akiwa kocha wa timu ya Tanzania iliyoshiriki Kombe la Chalenji Kenya 1994, akishirikiana na Charles Boniface walitwaa ubingwa wa Chalenji kwa kuifunga Uganda penalti 3-2. Katika dakika 120 za mchezo huo wa fainali, timu hizo zilifungana mabao 2-2. Mziray alianza kazi serikalini 1981 akiwa kama Afisa Lugha na Sanaa wa Wizara ya Utamaduni na Michezo kabla ya upandishwa cheo na kuwa Mtaalamu wa Soka Wizarani 1986. Alichukuliwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam sehemu ya Mlimani kama mhadhiri wa kitivo cha Elimu ya Viungo (Physical Education) lakini baadaye akaajiriwa na Chuo Kikuu Huria cha Tanzania akiwa ni mmoja wa wahadhiri wa masuala ya kijamii. Itakumbukwa alikuwa na ndoto za kuanzisha Chuo cha Soka, ili kuinua mchezo huo hapa nchini na mara zote alikuwa akilia na program za vijana. Mziray alizawaliwa Novemba 11 mwaka 1957 na kupata elimu ya msingi katika shule za Ifunda (Iringa), Lpw Academic (Iringa) Mpechi (Njombe), Songwe (Mbeya) Butimba (Mwanza) Lukajunge Karagwe) na kumalizia Wami (Morogoro) mwaka 1973. Alisoma Sekondari ya Malangali na kidato cha tano na sita alisoma Sekondari ya Mirambo mkoani Tabora na baada ya kuhitimu, alijiunga na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kambi ya Makutupora mkoani Dodoma iliyokuwa kwa mujibu wa sheria. Mwaka 1981, alikwenda kozi mbalimbali nchini Bulgaria na kuhitimu 1986 na alipata shahada ya pili ya viungo na utamaduni. Alikwenda Norway mwaka 1996 na 1997 kwa kozi nyingine na 2000 alikwenda Finland akiwa mwanafunzi wa Chuo cha Vuebamaki. *Imeandaliwa na Jesca Nangawe, Joseph Zablon na Sosthenes Nyoni.