Prime
Mbio za ubingwa zamkosha Barker Simba, amtaja Chama
KOCHA wa Simba, Steve Barker amesema ushindi wa mabao 4-0 dhidi ya Tanzania Prisons walioupata kwenye Uwanja wa KMC Complex, Dar, umeonyesha namna kikosi chake kilivyoelewa falsafa yake.
Huku pia akisisitiza bado wana kazi kubwa ya kuhakikisha wanamaliza msimu kwa nguvu ileile waliyoionyesha katika mchezo huo ambao umewafanya kufikisha pointi 49 katika nafasi ya pili.
Barker amesema moja ya vitu vilivyomfurahisha zaidi ni namna timu hiyo ilivyocheza mchezo huo kwa utulivu mkubwa tangu dakika za mwanzo huku akieleza kuwa mazingira mazuri ya uwanja yaliwasaidia kucheza aina ya soka wanayoitaka ya kushambulia na kumiliki mchezo.
“Tulicheza kwenye uwanja mzuri ambao haukuwa mbaya wala wenye matuta mengi, hivyo hilo lilitusaidia sana. Tulianza mchezo vizuri sana, tulikuwa tunautawala mchezo, tulicheza kwa nguvu kubwa na intensiti ya hali ya juu,” amesema Barker.
Kocha huyo raia wa Afrika Kusini amesema Simba ilionyesha uthubutu mkubwa wa kushambulia tangu mwanzo wa mchezo na hata baada ya kupata bao la kuongoza ambalo lilifungwa na Morice Abraham, bado waliendelea kuwabana wapinzani wao badala ya kurudi nyuma kulinda matokeo.
Barker amesema ubora wa Simba haukuonekana tu kwenye umiliki wa mpira, bali hata namna walivyokuwa wakitengeneza nafasi za kufunga kwa utulivu na mipango maalumu.
Kwa mujibu wa kocha huyo, mabao manne waliyopata huku yakifungwa na Morice, Clatous Chama, Seleman Mwalimu na Ismael Toure yalikuwa ni matokeo ya kazi kubwa waliyoifanya.
“Tulipofunga mabao yetu, nafikiri yalikuwa mabao yaliyostahili kabisa kutokana na namna tulivyocheza. Tulikuwa tunautawala mchezo na kuwafanya wapinzani washindwe kupata nafasi ya kutuchezea,” amesema.
Kocha huyo amesema pamoja na kutaka ushindi mkubwa zaidi lakini walilazimika pia kufikiria ratiba ngumu iliyopo mbele yao kutokana na mechi nyingi zilizobaki ndani ya muda mfupi.
“Wakati mwingine unatamani kupata mabao sita au zaidi lakini pia lazima ujue namna ya kuusimamia mchezo na kutotumia nguvu nyingi sana. Bado tuna michezo mitano ndani ya siku 14 au 15 zijazo, hivyo tulihitaji kuwa makini,” amesema.
Baada ya kumalizana na Prisons Alhamisi ya Mei 14, 2026, Simba itakuwa Kigoma kucheza dhidi ya Mashujaa kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika.
Katika hatua nyingine, Barker amesema ushindi huo uliwapa nafasi nzuri ya kuwapumzisha baadhi ya mastaa wake ambao wamekuwa wakicheza karibu kila mchezo tangu kuanza kwa mzunguko wa pili wa ligi.
Mbali na ushindi huo mnono, Barker amesema kitu kingine kilichomfurahisha ni namna safu yake ya ulinzi ilivyomaliza mchezo bila kuruhusu bao, jambo ambalo amesema ni muhimu katika mbio za ubingwa.
“Tulitimiza malengo yetu yote kwenye mchezo huu. Tumeweka ‘clean sheet’, tumefunga mabao mazuri na tumepata ushindi mzuri. Hilo ni jambo muhimu sana kwetu,” amesema.
Kocha huyo pia alimwaga sifa Chama ambaye ameendelea kuonyesha kiwango bora tangu ajiunge na Simba katika dirisha dogo la usajili la Januari.
Barker amesema mchezaji huyo amekuwa moja ya silaha kubwa ndani ya kikosi chake kutokana na ubora wake wa kiufundi na uwezo wa kutengeneza nafasi za kufunga.