Jentrix Shikangwa aanza kukiwasha Misri
Muktasari:
- Shikangwa alikuwa miongoni mwa wafungaji wa FC Masar katika ushindi huo wa mabao 21-0, akionesha mapema uwezo wake wa kufumania nyavu ambao aliuonyesha akiwa na kikosi cha Simba Queens misimu mitatu aliyoitumikia Ligi Kuu ya Wanawake Tanzania.
MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Kenya, Jentrix Shikangwa anayekipiga FC Masar, ameanza vizuri maisha yake mapya kwenye Ligi Kuu ya Wanawake ya Misri baada ya kufunga mabao matano katika mchezo mmoja uliomalizika kwa ushindi wa mabao 21-0.
Shikangwa alikuwa miongoni mwa wafungaji wa FC Masar katika ushindi huo wa mabao 21-0, akionesha mapema uwezo wake wa kufumania nyavu ambao aliuonyesha akiwa na kikosi cha Simba Queens misimu mitatu aliyoitumikia Ligi Kuu ya Wanawake Tanzania.
Mshambuliaji huyo ameanza ukurasa mpya baada ya kuondoka Simba Queens, ambako alitengeneza rekodi nzuri katika kipindi chake cha miaka kadhaa nchini.
Shikangwa alijiunga na Simba Queens Septemba 2022 akitokea Vihiga Queens ya Kenya, na katika kipindi chake cha kuitumikia klabu hiyo ya Tanzania alifanikiwa kufunga jumla ya mabao 69 katika Ligi Kuu ya Wanawake. Mabao hayo na kiwango chake vilimfanya kuwa miongoni mwa wachezaji wa kigeni walioacha alama katika soka la wanawake Tanzania, huku akisaidia Simba Queens kutengeneza historia katika mashindano ya ndani na kimataifa.
Katika kipindi chake Simba Queens, Shikangwa alifanikiwa kushinda mataji mawili ya Ligi Kuu ya Wanawake Tanzania, yaliyokuja katika misimu ya 2023-2024 na 2025-2026.
Mbali na mataji hayo ya ligi, mshambuliaji huyo pia alifanikiwa kubeba taji la CECAFA, huku Simba Queens ikipata nafasi ya kushiriki Ligi ya Mabingwa Afrika kwa Wanawake msimu wa 2023-2024. Baada ya kuacha rekodi ya mabao 69 Tanzania, Shikangwa sasa ameanza ukurasa mwingine Misri, akiwa na kazi ya kuendelea kuthibitisha ubora wake katika ligi mpya.