Himid Mao aipongeza Tanzanite Queens Kombe la Dunia
Muktasari:
- Tanzania ambayo ni mara yao ya kwanza kushiriki mashindano hayo ipo mkiani mwa kundi B baada ya kucheza mechi mbili na kupoteza dhidi ya Brazil kwa mabao 5-1 na England 4-1.
KIUNGO wa Azam FC, Himid Mao amewapongeza wachezaji wa timu ya Taifa ya wanawake U-20, Tanzanite Queens, kwa kuifikisha Tanzania kwenye hatua ya Kombe la Dunia la vijana, Poland.
Akizungumza na Mwanaspoti, Mao amesema licha ya Tanzanite Queens kutopata matokeo mazuri katika mechi zao za mwanzo, ushiriki wao kwenye mashindano hayo ni hatua kubwa kwa soka la wanawake nchini.
Amesema timu za Taifa za wanawake zimekuwa zikionyesha uwezo katika mashindano ya kimataifa na mara kadhaa kufika hatua za mbali, hivyo wadau wanapaswa kuendelea kuwekeza katika eneo hilo.
“Licha ya Tanzania kutokuanza vizuri, wadau wanapaswa kulipiga jicho soka la wanawake kwa sababu ni eneo ambalo limekuwa likifanya vizuri kwenye mashindano ya kimataifa,” amesema Mao.
Kiungo huyo amesema mafanikio ya soka la wanawake hayapaswi kuangaliwa kwa matokeo pekee, bali pia hatua ambazo timu hizo zimepiga kwa kufika kwenye michuano mikubwa kama Kombe la Dunia na kucheza WAFCON mara nyingi.
Ameongeza uwekezaji mkubwa katika timu za wanawake unaweza kusaidia kuongeza ushindani, kuibua vipaji vipya na kuifanya Tanzania kuendelea kushiriki mashindano makubwa ya kimataifa.
Tanzania ambayo ni mara yao ya kwanza kushiriki mashindano hayo ipo mkiani mwa kundi B baada ya kucheza mechi mbili na kupoteza dhidi ya Brazil kwa mabao 5-1 na England 4-1.